Sunday 29 June 2014

VIPI TUTAIPOKEA RAMADHANI


Makala imeandaliwa na Raudhwah Islamic Group

Kila sifa njema zinamstahikia Allah Mola wa viumbe vyote. Sala na salamu zimuendee Mtume wetu Muhammad (swalla Allahu alaihi wa sallam) na ahli zake na maswahaba wake.

Kwa hakika mwezi wa Ramadhani tayari umeshafika. Na baada ya muda mchache tutaingia katika mwezi huo mtukufu. Mwezi uliokuwa bora. Mwezi ambao ni shamba la watenda wema ili kuchuma mazuri yatakayowafaa kesho akhera. Ni mwezi wa kuomba tawba tukasemehewa dhambi zetu. Ila suala la muhimu kabisa ni vipi fursa hii ya Ramadhani tunaweza kuitumia? Ni lazima uweke maandalizi ambayo yatakuja kukufaa na kuyafanya ndani ya mwezi wa ramadhani.

Kwa nini tuuthamini mwezi huu wa Ramadhani? Na kwa nini inamlazimu muislamu kuwa na makusudio na jitihada maalum ndani ya Ramadhani. Kwanza tuangalie hadithi ya Mtume (swalla Allahu alayhi wasallam) inayosema “ Kutoka kwa Abdul rahmaan Bin Sakhar Al dausy (Abuu Huraira) (radhi za Allah ziwe juu yao)  amesema RASOUL  (swalla Allahu alayhi wasallam) “UMEPEWA UMMAH WANGU MAMBO MATANO KATIKA RAMADHANI HAUKUWAHI KUPEWA UMMAH WOWOTE KABLA YAKE.
1-HARUFU INAYOTOKA KWENYE KINYWA CHA ALIYEFUNGA INAPENDEZA ZAIDI MBELE YA ALLAH KULIKO HARUFU YA MISKI.
2- MALAIKA HUWAOMBEA MSAMAHA WAJA HAO MPAKA WAFTARI.
3- ALLAH HUIANDAA NA KUIPAMBA PEPO YAKE KILA SIKU NA HUIAMBIA JANNAH KWA WAKARIBIA WAKATI AMBAPO WAUMINI WATATUPULIA MBALI MITIHANI MIKUBWA YA DUNIA NA KUKUINGIA.
4-SHETANI HUFUNGWA MINYORORO ILI WASIWATIE UOVU KAMA AMBAVYO HUFANYA MIEZI MENGINE.
5-USIKU WA MWISHO WA RAMDHANI WAFUNGAJI HUSAMEHEWA MADHAMBI YAO”  (Imepokelewa na Ahmad na Baihaqi)

Ndani ya mwezi wa ramadhani kuna makumi matatu. Rasoul swalla Allahu alayhi wasallam anasema ya kwamba mwanzo wake ni rehma katika yake ni magh-firah na mwisho wake mja kuepushwa na moto.
Mwezi wenyewe ndio unakaribia kutufikia bila shaka mambo mazuri kama hayo kila mtu anahamu ayapate lakini unahitaji maandalizi sasa mimi na wewe je! vipi tutaweza kuupokea mwezi mtukufu wa ramadhani.

1-Kwanza kabisa muislamu ahakikishe anajua elimu kamili juu ya funga. Kuanzia  sharti za kusihi kwa wafunga, yanayobatilisha funga, nani anaruhusika kufungua au kutofunga, yaliyo sunna kwa mwenye kufunga na mengineyo.

Ikiwa muislamu atayajua hayo atakuwa na tahadhari ya kuichunga funga yake ili asije akawa anakaa na njaa ila hana chochote katika funga yake.

2- Kuchukua tahadhari zaidi na dhambi zinazotokana na ulimi. Katika viungo ambavyo Mtume (swalla Allahu alayhi wasallam) amesema yeyote atakaemdhamini viungo hivyo kwa maana kuvitumia katika kheri na akajiepusha na haramu basi anamdhamini pepo. Kutoka kwa Sahli bin Saad (Radhiya Allaahu anhu) amesema: Mtume (Swalla Allaahu alayhi wa aalihi wa sallam) amesema: "Atakayenidhaminia kilichomo baina ya taya zake [yaani ulimi] na kilichomo baina ya miguu yake (yaani tupu au sehemu za siri) nami nitamdhamini Pepo" (Al-Bukhaariy na Muslim)

Suali litakuja je ulimi unaweza kumfanya mtu asiwe na funga? Tuangalie hadithi ya Mtume (swalla Allahu alayhi wasallam) inayosema " Yule ambae haachi kusema uongo na haachi vitendo viovu. Allah (subhanahu wataala) hana haja na funga yake." Bukhari na Muslim.

Hadithi ya hapo juu inaonesha wazi ikiwa mtu hatofunga pamoja na kuuzuia ulimi wake na maasi basi hatokuwa na funga. Hivyo muislamu aupokee mwezi huu kwa kukusudia hasa kuwa mbali na dhambi kama za kusengenya,kusema uongo,matusi basi ajue Allah hana haja na funga yake na anakaa na njaa tu. Allah atujaalie wale ambao watazizuia ndimi zao na dhambi hizo na mfano wa hayo.

3- Muislamu aweke nia na azma ya kufunga ramadhani kwa uzuri na kwa kutaraji malipo kutoka kwa Allah (subhanahu wataala). Amesema Mtume (swalla Allahu alayhi wasallam) : "Atakayefunga Ramadhaan kwa imani na kutaraji malipo atasamehewa madhambi yake yaliyotangulia " Bukhaariy na Muslim.

4- Kuhakikisha muislamu kuwa anasali sala za faradhi kwa wakati na kujihimiza sana na kusali sala za sunna. Miongoni mwa sala za sunna ni rakaa 12 za sunna (Qabliya na Baadiyah), sala ya dhuha,sala ya witri na sala ya tarawehe.

5-Kushikamana na kusoma quran kwani mwezi wa ramadhani ndio ulioteremshwa Quraan. Allah (subhanahu wataala) anasema "Mwezi wa Ramadhani ambao imeteremshwa humo Qur'ani kuwa ni uwongofu kwa watu, na hoja zilizo wazi za uwongofu na upambanuzi. "(Baqara :185).

Hata Jibril alikua akishuka kila mwaka katika mwezi wa ramadhani kwa kumdurusisha Quraan Mtume (swalla Allahu alayhi wasallam)  sio kua hajui kusoma ila ni kuonesha ubora na umuhimu wa ibada hiyo ndani ya mwezi wa Ramadhani.

Kusoma Quraan kuna faida nyingi sana. Miongoni mwa faida hizo ni mtu kupata thawabu kwa kila herufi atakayoisoma. Imetoka kwa Abdullahi bin Masuud (Radhiya Allahu anhu) kwamba Mtume (Swalla Allahu alayhi wasallam) amesema: "Atakayesoma herufi moja katika kitabu cha Allaah atapata hasanah (jema) moja, na kila hasanah moja ni sawa na thawabu kumi, wala sisemi "Alif-Laam-Miym" ni herufi moja, bali Alif ni herufi moja na Laam ni herufi moja na Miym ni herufi moja))  At-Tirimidhiy.

Pia Quraan itakuwa kiombezi kwa watu wa Quraan. Watu waliokuwa wamedumu kusoma Quraan kwa mazingatio na kuifanyia kazi. Imetoka kwa Abu Umaamah (Radhiya Allahu anhu)  kwamba Mtume (Swalla Allahu alayhi wasallam)  amesema "Someni Qur-aan kwani itakuja siku ya Qiyaamah ikimuombea   mwenye kuisoma" Muslim.

Hivyo basi muislamu azidishe kusoma Quraan na ajitahidi aisome kwa mazingatio.

6- Kuhudhuria katika sehemu mbali mbali za kujifunza kama katika mihadhara na madarsa mbali mbali.  Jambo hili leo hii wengi wetu tumeliwacha na tumekuwa tukitumia muda wetu mwingi ndani ya whatsapp,facebook na mitandao mengineyo pamoja na vibaraza vyenye mazugumzo yasiyokuwa na manufaa. Na mtu anapoambiwa ahudhurie sehemu za kheri basi hutoa sababu zisizo na msingi ila yote hayo tumeghafilika na mauti na imetuhadaa dunia.
Sehemu za kujifunza na kukumbushana yaliyo mema ni nzuri sana katika kuufanya moyo wa mja uwe unaathirika na maneno ya Allah. Na hii itamfanya daima awe anakumbuka wajibu wake kama kiumbe wa Allah(subhanahu wataala) katika ulimwengu huu.

Mwisho kwa kumalizia tujitahidini kuyafanyia kazi haya tuayokumbushana kabla ya ramadhani ,ndani ya ramadhani na baada a ramadhani ili tuweze kuzitafuta radhi za Allah hapa duniani na kesho akhera.
Tunamuomba Allah (subhanahu wataala) atujaalie wale ambao watafika ramadhan na watafunga na kupata ujira mkubwa kutoka kwa Allah (subhanahu wataala) pamoja na kusamehewa dhambi zetu. Aaamin.

No comments:

Post a Comment