Sunday 29 June 2014

SHARTI ZA KUSIHI KWA FUNGA- SEHEMU YA PILI


Makala imeandaliwa na Raudhwah Islamic Group

3 – KUJIZUIA KUFANYA TENDO LA NDOA KWA MAKUSUDI NA KUJITOA MANII

Ikiwa mtu atafanya jimai bila ya kukusudia basi mtu huyo atakuwa amesameheka. Kwa kauli ya Allah: “Lakini ipo lawama katika yale ziliyo fanya nyoyo zenu kwa makusudi.” (Suratul Ahzaab : 5).

Ama yule ambae atafanya jimai kwa makusudi basi huyo funga yake itabatilika na itamlazimu kwake yeye kuilipa funga hiyo pamoja na kutoa kafara. Kafara kwa yule ambae atafanya tendo la ndoa katika mchana wa Ramadhani ni :

i. Kuacha huru mtumwa.
ii. Kufunga miezi miwili mfululizo.
iii. Alishe maskini 60 kila mmoja kibaba kimoja.

Ikiwa mke au mume mmoja wao amemlazimisha kwa nguvu mwenzake kufanya tendo la ndoa ndani ya mchana wa Ramadhan na wamo katika funga basi yule aliemlazimisha mwenzake ndio itamuwajibikia kutoa kafara.

Na mwanamke hatakiwi akubali kufanya tendo la ndoa wakati amefunga ndani ya Ramadhani. Na  maulamaa wengine wakaengeza kwa kusema hata ikiwa anaweza kupigana na mume wake basi ampige. Kuonesha uzito wa funga. Na wala mtu asitumie kivuli kuwa amelazimishwa kujitetea ajue kuwa Allah (subhanahu wata‘ala) anajua kila kilichomo ndani ya nafsi ya mja wake.

Ikiwa mtu atafanya tendo la ndoa hali ya kuwa amefunga ndani ya Ramadhani kwa siku mbili tofauti basi ni juu yake kafara mbili. Kila funga moja basi na kafara yake moja.

Pia ikiwa mtu anafanya tendo la ndoa na baadae ikambainikia kuingia kwa alfajiri basi kinachotakiwa ni kuacha tendo la ndoa hapo hapo akakoge janaba na aendelee na funga yake.

Je ni wakati gani jimai ya mchana wa Ramadhani inaruhusika?

Ikiwa mke na mume wote wana dharura za kisheria za kutofunga kwa mfano wote wamesafiri basi hakuna ubaya na hawatotoa kafara. Kwani awali ruhusa ya kutofunga ishakuwepo kwao wao.

Ikiwa mume amerudi safari na mke wake hakufunga siku hiyo kwa sababu ya hedhi na ametwaharika baada ya funga kuanza, basi tendo la ndoa kwao wao linaruhusika kwani mume hajafunga na mke hakufunga.

Ama kinyume na hali hizo wakifanya tendo la ndoa ndani ya mchana wa Ramadhani wakiridhia wenyewe basi kwa kila mmoja juu yake kafara ama mmoja amemlazimisha mwenzake basi yule aliyemlazimisha mwenzake ni juu yake kutoa kafara.

Kujitoa maniii kwa makusudi kunabatilisha funga. Hivyo basi yeyote ambae amefunga anatakiwa ajizuie na kujitoa manii kwa makusudi. Na mfano wa kujitoa manii kwa makusudi ni puunyeto, au kwa kumkumbatia au kumchezea mkewe au mwanamke mpaka akatokwa na manii.

1-SUALI
Walifanya jimai kabla ya kuanza kwa funga na baadae hawakuwahi kukoga janaba wakalala mpaka ikaingia alfajiri. Je nini hukmu ya funga yao?
JIBU
Ikiwa walitia nia ya kufunga basi funga yao itasihi. Kinachowalazimu ni kukoga janaba ili waweze kuswali na waendelee na funga yao. Na hili ni kwa ushahidi wa hadithi ya Bibi Aysha na Ummu Salamah (radhiya Allahu anhuma) “kwamba Mtume (Swalla Allahu alayhi wasallam) alikuwa akiamka na janaba kutokana na kukutana kimwili na wake zake, kisha anakoga na kufunga.” (Al Bukhariy na Muslim).

2-SUALI
Alifanya jimai bila ya kujua kwamba alfajiri imeingia. Na baadae akajua kuwa alifanya jimai wakati tayari alfajiri ishaingia. Nini hukmu yake?

Ikiwa wakati anafanya hajui kama wakati umeingia basi atakoga na ataendelea na funga yake. Kwani hakuna kosa kwa mtu kutojua.Ama akifanya kwa kusudi basi funga itabatilika funga yake na itamlazimu kutoa kafara na kuilipa funga hiyo.

4-KUEPUKANA NA HEDHI NA NIFASI

Ni lazima kwa mwanamke anaetaka kufunga awe ametoharika kutokana na hedhi na nifasi. Na pindi mwanamke anapokuwa na hedhi au nifasi basi huwa ni wajibu kwake kuacha kufunga. Na hii ni amri kutoka kwa Allah (subhanahu wata‘ala) na mwanamke akitoharika ataendelea na kufunga. Pia siku ambazo ameziacha kwa kutofunga atakuja kuzilipa baada ya Ramadhani.

SUALI
Bado muda mdogo sana kumalizika kwa funga. Mwanamke akapatwa na hedhi. Je itahesabika funga yake ile?

JIBU
Hapana, haitohesabika funga ile kwa sababu wakati haujatimia. Na itamlazimu mwanamke huyo aje kuilipa funga hiyo baada ya kumalizika kwa Ramadhani.

SUALI
Mwanamke amepatwa na maumivu au dalili nyengine za kuonyesha atapatwa na hedhi ila hakupata wala hakutokwa na damu. Nini hukmu yake?
JIBU
Hatowajibika kuilipa na funga yake itakuwa sahihi.

SUALI
Ikiwa mwanamke siku zake za hedhi zimekaribia. Akaona matone ya damu ila damu haikutoka. Nini hukmu ya funga yake?
JIBU
Lazima ailipe funga hiyo kwani matone hayo ya damu yatahesabika kama ni damu ya hedhi.

SUALI
Miaka yote Ramadhan napata kufunga siku 10 tu au 11. Na zinazobaki nakuwa katika siku za hedhi. Sipati kufanya ibada ambazo zina fadhila kubwa kuliko miezi mingine. Nakuwa mnyonge kutokana na hali hiyo.
Je naweza kutumia vidonge vya kuzuia hedhi ?

JIBU
Kuhusu hedhi muda wake wajuu kabisa ni siku kumi na tano, zikizidi hapo huwa ni ugonjwa, kwa maelezo yako unakuwa ukitokwa na damu kwa takriban siku 20, hii inaonesha una tatizo jitahidi kutafuta tiba ya ugonjwa huo.
Ama ikiwa zitabaki siku 15 au chini ya hapo tutaizingatia kuwa ni hedhi, na kipindi unachokua ndani ya hedhi kuacha yale sheria iliokutaka kuyaacha ni ibada, hivyo ibada iliyokuzuilia kufanya ibada nyengine fadhila zake ni kubwa zaidi kwa wakati huo.
Pili.
Kuhusu kutumia vidonge vya hedhi wako maulamaa wanasema kuwa haifai kutumia vidonge hivyo kwani vimethibitika vina madhara.

Ama tukisema havina madhara basi ushauri wetu ni bora kuiacha hedhi katika utaratibu wake ndio bora zaidi kiibada na kiafya pia. Kwani ndio maumbile yake mwanamke alivyoumbwa na Allah (subhanahu wata‘ala). Na Allah ndie mjuzi zaidi.

SUALI
Ikiwa mwanamke amemaliza nifasi kwa siku chache mfano siku saba je anaweza kufunga?
JIBU
Ikiwa kweli imesita damu ya nifasi mwanamke huyo anaweza kufunga. Na Allah ni mjuzi zaidi.

SUALI
Ni ipi hukmu ya funga kwa mwanamke aliyeharibu mimba?
JIBU
Ikiwa mimba imeharibika kabla ya mtoto kuumbika basi damu hiyo si damu ya nifasi na mwanamke atakoga kujisafisha na kuendelea na funga yake.
Ikiwa mimba imeharibika baada ya mtoto kuumbika basi damu hiyo itakuwa ni ya nifasi na itambidi ajizuie kufunga mpaka pale itakaposita damu ya nifasi. Na Allah ni mjuzi zaidi.

SUALI
Mwanamke ametoharika kabla ya kuanza kwa alfajiri ya kweli. Akatia nia ya kufunga ila akachelewa kukoga josho. Je anaweza kufunga?
JIBU
Ndio anaweza kufunga. Kitakachomlazimu ni kukoga josho kabla ya kutoka kwa swala ya alfajiri ili asiache swala na ataendelea na funga yake. Na Allah ni mjuzi zaidi.

Hayo ndio masharti ambayo yanalazimika kutimizwa ili funga ya Muislamu isihi. Na kinyume cha masharti hayo ni kubatilika kwa funga hiyo. Na kama tulivyoeleza itamuwajibikia mtu huyo kulipa. Ama yule ambae kwa sababu ya kufanya tendo la ndoa yeye itamuwajibikia kulipa pamoja na kafara. Na Allah ni mjuzi zaidi.

No comments:

Post a Comment