Monday 21 July 2014

Dua za Mtume Muhammad s.a.w


Du’aa katika Sunnah ziko nyingi sana. Aghlabu ya du’aa za Mtume (صلى الله عليه وسلم) zilikuwa za mukhtasari wa maneno kwa maana kauli zake fupi lakini zenye maana tele na hikma kama alivyosema mwenyewe katika usimulizi ufuatao:

عَنْ أَبِي هُرَيْرَةَ (رضي الله عنه) أَنَّ رَسُولَ اللَّهِ (صَلَّى اللَّهُ عَلَيْهِ وَسَلَّمَ) قَالَ: "فُضِّلْتُ عَلَى الأَنْبِيَاءِ بِسِتٍّ: أُعْطِيتُ جَوَامِعَ الْكَلِمِ, وَنُصِرْتُ بِالرُّعْبِ, وَأُحِلَّتْ لِيَ الْغَنَائِمُ, وَجُعِلَتْ لِيَ الأَرْضُ طَهُورًا وَمَسْجِدًا, وَأُرْسِلْتُ إِلَى الْخَلْقِ كَافَّةً, وَخُتِمَ بِيَ النَّبِيُّونَ

Imepokewa kutoka kwa Abu Huraryah (رضي الله عنه) kwamba Mtume (صلى الله عليه وسلم) amesema: ((Nimefadhilishwa juu ya Manabii kwa mambo sita; nimepewa ‘Jawaami’al-Kalimi’[1] na nimenusuriwa kwa [kutiwa] hofu [katika nyoyo za maadui] na nimehalalishiwa ghanima[2] na nimefanyiwa ardhi kuwa kitoharishi na masjid [mahali pa kuswali], na nimetumwa kwa viumbe wote, na Manabii wamekhitimishwa kwangu))[3]

Tunazigawanya Du’aa hizo katika maudhui mbali mbali na kutokana na hali zinazomkabili Muislamu:

-Du’aa Alizokuwa Akiomba Sana Mtume (صلى الله عليه وسلم )

Kuomba kheri za dunia na Akhera

رَبَّنَا آتِنَا فِي الدُّنْيَا حَسَنَةً وَفِي الأَخِرَةِ حَسَنَةً وَقِنَا عَذَابَ النَّارِ

Rabbaana aatinaa fid-dduniya hasanatan wafil Aakhirati hasanatan wa qinaa adhaaban-naari[4]

Mola wetu, tupe katika dunia mema na katika Akhera mema na Tukinge adhabu ya Moto[5]

Kuthibitika Katika Dini Na Utiifu

‏ يَا مُقَلِّبَ الْقُلُوبِ ثَبِّتْ قَلْبِي عَلَى دِينِك

Yaa muqallibal quluwbi, thabbit qalbiy ‘alaa Diynika

Ee Mwenye kupindua nyoyo, Thibitisha moyo wangu katika Dini Yako[6]

اللَّهُمَّ مُصَرِّفَ الْقُلُوبِ صَرِّفْ قُلُوبَنَا عَلَى طَاعَتِكَ

Allaahumma Muswarrifal quluwbi, swarrif quluwbanaa ‘alaa twaa’atika

Ee Allaah, Mwenye kugeuza nyoyo, zigeuzi nyoyo zetu katika utii Wako[7]

-Du’aa Za Maombi Ya Ujumla

‏ اللَّهُمَّ إِني أسْأَلُكَ مِنْ الْخَيْرِ كُلِّهِ عَاجِلِهِ وَآجِلِهِ مَا عَلِمْتُ مِنْهُ وَمَا لَمْ أعْلَمْ، وَأعُوذُ بِكَ مِنَ الشَّرِّ كُلِّهِ عَاجِلِهِ وَآجِلِهِ مَا عَلِمْتُ مِنْهُ وَمَا لَمْ ‏‏ أعْلَمْ، اللَّهُمَّ إِنِّي أسْأَلُكَ مِنْ خَيْرِ مَا سَألَكَ عَبْدُكَ وَنَبِيُّكَ، وَأعُوذُ بِكَ مِنْ شَرِّ مَا استعَاذَ بِكَ مَنْهُ عَبْدُكَ وَنَبِيُّكَ، اللَّهُمَّ إنِّي أسْأَلُكَ الْجَنَّةَ وَمَا قَرَّبَ إلَيْهَا مِنْ قَوْلٍ أوْ عَمَلٍ وَأعُوذُ بِكَ مِنْ النَّارِ وَمَا قَرَّبَ إِلَيْهَا مِنْ قَوْلٍ أوْ عَمَلٍ، وَأسْأَلُكَ أنْ تَجْعَلَ كُلَّ قَضَاءٍ قَضَيْتَهُ لِي خَيْرًا

Allaahumma inniy as-aluka minal-khayri kullihi ‘aajilihi wa aajilihi, maa ‘alimtu minhu wamaa lam a’lam. Wa a’uwdhu Bika minash-sharri kullihi ‘aajilihi wa aajilihi maa ‘alimtu minhu wamaa lam a’lam. Allaahumma inniy as-aluka min khayri maa saalaka ‘Abduka wa Nabiyyuka, wa a’uwdhu Bika min sharri masta’aadha Bika minhu ‘Abduka wa Nabiyyuka. Allaahumma inniy as-alukal-Jannata wamaa qarraba ilayhaa min qawlin aw ‘amal, wa a’uwdhu Bika minan-nnaari wamaa qarraba ilayhaa min qawlin aw ‘amal, wa as-aluka antaj-’ala kulla qadhwaai qadhwaytahu liy khayraa

Ee Allaah, hakika mimi nakuomba kheri zote zilizokaribu na mbali nizijuazo na nisizozijua. Najikinga Kwako shari zote za karibu na za mbali nizijuazo na nisizozijua. Ee Allaah, hakika nakuomba kheri alizokuomba mja Wako na Nabii Wako, na najikinga Kwako shari alizojikinga nazo mja Wako na Nabii wako. Ee Allaah, hakiki mimi nakuomba Pepo na yanayokaribisha kwayo katika kauli au amali, na najikinga Kwako Moto na yanayokaribisha kwayo katika kauli au amali, na nakuomba Ujaalie kila majaaliwa yangu [uliyonikidhia] yawe kheri[8]

‏ اللَّهُمَّ إِنِّي أسْألُكَ الْهُدَى وَالتُّقَى وَالْعَفَافَ وَالْغِنَى

Allaahumma inniy as-alukal-hudaa wat -ttuqaa wal ‘afaafa wal ghinaa

Ee Allaah hakika mimi nakuomba uongofu na ucha-Mungu na kujichunga[9] na kutosheka[10]

Kuomba Hidaaya:

اللَّهُمَّ اهْدِنِي وَسَدِّدْنِي, اللَّهُمَّ إِنِّي أَسْأَلُكَ الْهُدَى وَالسَّدَادَ

Allaahumma-hdiniy wasaddid-niy, Allaahumma inniy as-alukal-hudaa was-ssadaad

Ee Allaah, niongoe na nionyoshe sawasawa. Ee Allaah hakika mimi nakuomba hidaaya na unyofu[11]

Kuomba hesabu ya sahali Aakhirah Na Kuwa pamoja na Mtume (صلى الله عليه وسلم ) Peponi.

اللَّهُمَّ حَاسِبْنِي حِسَابًا يَسِيرًا

Allaahumma haasibniy hisaaban -yasiyraa

Ee Allaah nihesabie hisabu iliyo sahali[12]

اللَّهُمَّ إِنِّي أَسْأَلُكَ إِيمَانًا لاَ يَرْتَدُّ, وَنَعِيمًا لاَ يَنْفَدُ, وَمُرَافَقَةَ النَّبِيِّ صَلَّى اللَّهُ عَلَيْهِ وَسَلَّمَ فِي أَعْلَى غُرَفِ الْجَنَّةِ جَنَّاتِ الْخُلْدِ

Allaahumma inniy as-aluka iymaanan laa yartaddu, wa na’iyman laa yanfaddu, wa muraafqatan-Nabiyyi Swalla-Allaahu ‘alayhi wa sallam fiy a’-laa ghurafil-Jannah, Jannaatil-khuldi

Ee Allaah, hakika nakuomba imani isiyoritadi [isiyobadilika], na neema zisizoisha na kuambatana na Nabii Swalla-Allaahu ‘alayhi wa sallam katika vyumba vya ghorofa za juu kabisa Peponi, Pepo za kudumu milele[13]

-Kuomba Wingi Wa Iymaan, Taqwa Na Hifadhi

اللَّهُمَّ أَعِنِّي عَلَى ذِكْرِكَ وَشُكْرِكَ وَحُسْنِ عِبَادَتِكَ

Allaahumma a’inniy ‘alaa dhikrika, wa shukrika wa husni ‘ibaadatika

Ee Allaah nisaidie juu ya utajo Wako [kukudhukuru], na kukushukuru na uzuri wa ‘ibaadah Zako[14]

‏‏اللَّهُمَّ اقْسِمْ لَنَا مِنْ خَشْيَتِكَ مَا يَحُولُ بَيْنَنَا وَبَيْنَ مَعَاصِيكَ، وَمِنْ طَاعَتِكَ مَا ‏ ‏تُبَلِّغُنَا ‏بِهِ جَنَّتَكَ، وَمِنْ الْيَقِينِ مَا تُهَوِّنُ بِهِ عَلَيْنَا مُصِيبَاتِ الدُّنْيَا، وَمَتِّعْنَا بِأسْمَاعِنَا وَأبْصَارِنَا وَقُوَّتِنَا مَا أحْيَيْتَنَا, وَاجْعَلْهُ ‏الْوَارِثَ مِنَّا، وَاجْعَلْ ثَأرَنَا عَلَى مَنْ ظَلَمَنَا وَانْصُرْنَا عَلَى مَنْ عَادَانَا، ولا تَجْعَلْ مُصِيبَتَنَا فِي دِينِنَا، وَلا تَجْعَلْ الدُّنْيَا أكْبَرَ هَمِّنَا وَلا مَبْلَغَ عِلْمِنَا، وَلا تُسَلِّطْ عَلَيْنَا مَنْ لا يَرْحَمُنَا

Allaahumma-qsim-lanaa min khash-yatika maa yahuwlu baynanaa wa bayna ma’swiyk, wamin twaa’atika maa tuballighunaa bihi Jannatak, wa minal-yaqiyni maa tuhawwinu bihi ‘alaynaa muswiybaatid-duniya, wa matti’-naa biasmaa’inaa wa abswaarinaa wa quwwaatinaa maa ahyaytanaa waj-’alhul-waaritha minnaa waj-’al thaaranaa ‘alaa man dhwalamanaa wanswurnaa ‘alaa man ‘aadaana, walaa taj-’al muswiybatanaa fiy diyninaa, walaa taj-’alidduniya akbara hamminaa walaa mablagha ‘ilminaa, walaa tusallitw ‘alaynaa man-llaa yarhamunaa

Ee Allaah tugawanyie sisi hofu Yako itakayotenganisha baina yetu na baina maasi Yako, na utiifu utakaotufikisha katika Pepo Yako, na yaqini itakayotusahilishia misiba ya dunia, na tustareheshe kwa masikio yetu, na macho yetu, na nguvu zetu madamu Utatuweka hai, na yajaalie yawe ni urithi wetu na Jaalia iwe lipizo kwa anayetudhulumu, na tunusuru dhidi ya anayetufanyia uadui, na wala Usitufanyie msiba wetu ni Dini yetu, wala Usifanye dunia kuwa ndio hima yetu kubwa kabisa, na wala upeo wa elimu yetu, wala Usitusaliti kwa asiyetuhurumia[15]

Saturday 19 July 2014

HALI ZA WEMA WALIOPITA NDANI YA RAMADHAN

Makala imeandaliwa na Raudhwah Islamic Group

Kila sifa njema zinamstahikia Allah Mola wa viumbe vyote. Sala na salamu zimuendee Mtume wetu Muhammad (swalla Allahu alaihi wa sallam) na ahli zake na maswahaba wake.

Kutoka kwa Abi Hurayra (radhiya Allahu anhu), Amesema Mtume (swalla Allahu alayhi wasallam) ““Yoyote atakaefunga Ramadhan, kwa imani na kwa kutarajia malipo atasamehewa dhambi zake zilotangulia”. Bukhari na Muslim.

Katika makala hii leo tutaelezea vipi Mtume (swalla Allahu alayhi wasalla), maswahaba,matabiina na wema wengine waliopita walivyokuwa wakiuthamini mwezi wa Ramadhan. Na vipi walikuwa wakijitahidi katika kufanya ibada ndani ya Ramadhan ili waweze kufikia malengo ya Ramadhan pamoja na kupata ujira mkubwa kutoka kwa Allah (subhanahu wataala) ikiwemo kusamehewa dhambi zao zilizopita.

Wengi wetu tunafunga ila bidii inayotakiwa ambayo tuifanye ndani ya Ramadhan hatuioneshi au haitoshelezi na ndio maana kila mwaka tunafunga na hatuoni matunda ya funga zetu wala hatuoni raha ya mwezi mtukufu wa Ramadhan.

Mtume (swalla Allahu alayhi wasallam) alikuwa ni mwenye kuupokea mwezi mtukufu wa Ramadhan kwa kufunga sana ndani ya mwezi wa Shaaban. Pia unapoingia mwezi wa Ramadhan alikuwa ni mwingi wa kufanya ibada na zaidi huzidisha pale linapoingia kumi la mwisho pia hukaa iitikafu. Amesema Bibi Aisha (radhiya Allahu anha) "Zilipokuwa zikiingia siku kumi za mwisho (za Ramadhan), Mtume (swalla Allahu alayhi wasallam) alikuwa akiuhuisha usiku kwa kufanya ibada, akiamsha familia yake usiku, na akikaza Izaar yake (shuka inayovaliwa kiunoni makusudio hapa ni kuwa alikuwa akijibidiisha sana). Bukhari na Muslim.
Pia  imepokewa kutoka kwa Aisha (Radhiya Allaahu anhaa) kwamba: Mtume (swalla Allaahu alayhi wa sallam) alikuwa akifanya Itikaaf kila Ramadhaan siku kumi, ulipofika mwaka wake wa kuaga dunia alifanya Itikaaf siku ishirini" Bukhari

Pia  alikuwa Mtume (swalla Allahu alayhi wasallam) akisoma Quraan pamoja na kuja kusomeshwa Quraan na mwalim wake Sayydina Jibri. “Mtume (Swalla Allaahu alayhi waaalihi wasallam) alikuwa ni mbora (mwenye matendo mema) kwa watu, na alikuwa mbora zaidi katika Ramadhan kwa sababu Jibril alikuwa akimjia kila usiku wa Ramadhaan akimfundisha Qur-aan” Al-Bukhaari

Huyu ndie aliekuwa kipenzi cha Allah (subhanahu watala) akifanya matendo kama hao. Kipenzi ambae ameshasamehewa dhambi zake zilizopita na zijazo. Je vipi mimi na wewe?

Vipi yalikuwa mapokezi ya wema waliopita kwa ajili ya Ramadhan? Wema waliopita walikuwa wakiupokea mwezi wa Ramadhan kwa furaha pamoja na maandalizi mazuri na makubwa ya kuupokea mwezi mtukufu wa Ramadhan.  Anasema Muala Ibn Fadhwal “ Walikuwa watu wema miezi sita wakimuomba Allah (subhanahu wataala)  awafikishe Ramadhan ”

Wema waliopita walizifahamu hadithi hizi na ndio maana nao walijibidiisha katika kufanya mazuri ndani ya Ramadhan. Dua zao njema walizielekeza kwa Allah (subhanahu wataala) awafikishe mwezi wa Ramadhan wakiwa ni wazima ili waweze kufunga na kutekeleza ibada mbali mbali ndani ya Ramadhan. Pia walikuwa wakimuomba Allah (subhanahu wataala) daima wawe katika uongofu ili isije ikaingia Ramadhan na wao hawako katika utiifu wa Allah (subhanahu wataala). Pia wakimuomba Allah (subhanahu wataala) awatakabalie saumu zao watakazokuja kuzifunga.

Ukiangalia ni namna gani ambavyo walikuwa wakiuthamini mwezi huo. Mtu huanza kuupokea kwa dua za kumuomba Allah awafikishe miezi sita kabla ya kuingia Ramadhan na miezi iliyobaki hujibidiisha na kufanya Ibada. Sisi umma wa sasa tunasubiri karibu Ramadhan kufika ndio tunaanza kujiandaa nao tena kwa kuwaza vyakula tena kufanya israfu na sio vipi mtu atajipanga kwa ajili ya Ibada.

Wema waliopita waliitumia Ramadhan kwa kufanya matendo mema. Matendo yale yale ambayo alikuwa akiyafanya Mtume (swalla Allahu alayhi wasallam) kwani walifahamu kuwa kigezo chao ni Mtume Muhammad (swalla Allahu alayhi wasallam) na wakajibidiisha katika kumfuata.

Sasa tuangalie mifano hai vipi waliingia kwenye milango ya Kheri ya ndani ya Ramadhan :

Kusoma Quraan

Mwezi wa Ramadhan ni mwezi wa Quraan na ndio mwezi ambao imeteremshwa Quraan. Mtume(swalla Allahu alayhi wasallam) alikuwa mwingi wa kusoma Quraan ndani ya Ramadhan na  wema waliopita walitumia Ramadhan kwa kusoma Quraan.

Sayyidina Othmaan Ibn Affan alikuwa akimaliza msahafu kila sik umara moja.
Az zuhr mmoja ya wema waliopita wakati ilipokuwa ikiingia Ramadhan alikuwa akiacha kusoma hadithi na elimu nyengine alikuwa akiutumia muda wake wote kuisoma Quraan.

Qatadah alikuwa akimaliza kusoma Quraan kikawaida kila siku 7 mara moja lakini ndani ya Ramadhan kila baada ya siku 3 mara moja.

Kusali sala za Usiku

Kama tulivyoona kuwa Mtume (swalla Allahu alayhi wasallam) alikuwa ni mwenye kusali usiku na alikuwa akiwaamsha watu wake katika kumi la mwisho. Ummul Muuminina Aisha (Radhiya Allaahu anhaa):“Msiwache kuswali usiku (Qiyaamul Layl), kwani hakika Mjumbe wa Allah (Swalla Allaahu alayhi waaalihi wasallam) alikuwa hawachi kuswali usiku, na alikuwa Mjumbe wa Allaah (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) kama anaumwa au anaona uvivu huswali kwa kukaa.” Imepokelewa na Ahmad.

Hivyo hivyo na watu wema nao walimfuata Mtume (swalla Allahu alayhi wasallam). Amepokea Zayd bin Aslam kutoka kwa baba yake kuwa:“Alikuwa Umar bin Al-Khattwaab (Radhiya Allaahu anhu) akiswali usiku  Anavyomjaaliya Allah, hadi inapokuwa Aakhirul Layl -mwisho wa usiku– huwaamsha ahli zake kwa Swalah; huwaambia: Swalah Swalah, kisha husoma Aayah hii: “Na waamrishe watu wako Swalah, na ufanye subira kwa hayo. Sisi hatukuombi wewe riziki, bali Sisi ndio tunakuruzuku. Na mwisho mwema ni kwa mcha Mungu” (Twaahaa: 132). Imepokelewa na Maalik, katika Al-Muwattwa

Na katika Hadiyth ya nyengine ya Abdullaah bin Abi Bakr (Radhiya Allaahu anhu) amesema: Nimemsikia baba yangu Abu Bakr (Radhiya Allaahu anhu)- akisema:” Tulikuwa tukimaliza -Qiyaam- katika Ramadhaan basi tunawaharakisha wasaidizi kwa chakula kuchelea Alfajiri (isitukute)” Imepokelewa na Maalik katika Al-Muwattwa.

Kutoa Sadaka na Kumfturisha aliyefunga

Siku moja Mjumbe wa Allaah (Swalla Allaahu alayhi wa aalihi wasallam) aliulizwa Swawm ipi bora baada ya Ramadhaan? Akajibu: “Shaban… pakaulizwa Sadaka ipi bora? Akajibu: “Sadaka katika Ramadhaan” .Imepokelewa na At-Tirmidhiy.

Amesema Mjumbe wa Allaah (Swalla Allaahu alayhi wa aalihi wa sallam): “Atakayemfuturisha aliyefunga, atapata ujira kama ujira wake -aliyefunga- bila ya kupungua chochote katika ujira wa yule aliyefunga.” Imepokelewa na Ahmad

Masahaba na wema waliopita walijitahidi sana katika kutoa sadaka pamoja na kuftarisha wenziwao kwa kujua fadhila na utukufu wa jambo hili.

Imepokewa Abu As-Siwar Al adwi amesema “ Kundi la wanaume katika kabila la la Bani Adi walikuwa wakisali msikitini. Na hakukuwa na hata mmoja aliyekuwa akifungua peke yake. Akimuona mtu wa kula pamoja nae alikuwa anakula pamoja nae na ikiwa atakosa basi anakwenda na chakula chake msikitini ili ale chakula chake pamoja na wenzake.

Huu ni kwa uchache vipi watu wema walikuwa wakijibidiisha katika kupata matunda ya mwezi wa Ramadhan.

Nasaha kwako ewe msomaji jitahidi kuiga mifano hii ya watu wema ili nawe uwe ni mwenye kupata matunda ya mwezi wa Ramadhan kwa uwezo wake Allah (subhanahu wataala).

TAQWA NA VIPI TUTAIPATA TAQWA NDANI YA RAMADHANI

Makala Imeandaliwa na Raudhwah Islamic Group

Allah (subhanahu wataala) ametufaradhishia juu yetu kufunga. Na pale alipotufaradhishia akatuambia kuwa lengo kuu la kutufaradhishia funga ni kupata uchamungu(Taqwa). Pale aliposema “Enyi mlio amini! Mmeandikiwa Saumu, kama waliyo andikiwa walio kuwa kabla yenu ili mpate kuchamngu.”(2:183). Suali linaweza kuja nini maana ya uchamungu. Na vipi mtu anaweza kuupata uchamungu ndani ya Ramadhan? Kwa uwezo wa Allah kwa uchache majibu ya masuala hayo yatapatikana ndani ya makala hii.

TAQWA

Taqwa ni vazi ambalo anatakiwa avae kila muislamu. Vazi ambalo limekusanya yale yote aliyoamrisha Allah (subhanahu wataala) ambayo yanatakiwa yatekelezwe na yale yote yaliyoharamishwa ambayo yanatakiwa kuachwa. Msingi mkuu wa taqwa ni kufuata Quraan na Sunna za Mtume (swalla Allahu alayhi wasallam). Na vazi hili la uchamungu ndio vazi bora kuliko vazi jengine lolote. Anasema Allah (subhanahu wataala) “Enyi wanaadamu! Tumekuteremshieni nguo za kuficha tupu zenu, na nguo za pambo. Na nguo za uchamungu ndio bora…”(7:26).

Taqwa ni amri kutoka kwa Allah. Allah ametuamrisha tumche yeye pekee hapa ulimwenguni. Na akatuambia tuchukue zawadi ya uchamungu kwani ndio zawadi iliyokuwa bora kabisa na ndio itakayomfaa mwanadamu siku ya kukutana na mola wake. Anasema Allah (subhanahu wataala) “Na jitengezeeni zawadi. Na hakika bora ya zawadi ni uchamngu. Na nicheni Mimi, enyi wenye akili! (2:197).

Pia Mtume (swalla Allahu alayhi wasallam) amelisisitiza hilo kwa kututaka tuwe wenye kumcha Allah (subhanahu watala)popote tulipo iwe peke yake mtu au mbele za watu. Kutoka kwa Abu Dharr Jundub Ibn Junaada na Abu Abdur Rahmaan Muadh Ibn Jabal (radhi za Allah ziwe juu yao) kutoka kwa   Mtume (swalla Allahu alayhi wasallam) amesema: "Mche Allah popote pale ulipo, na fuatisha kitendo kibaya kwa kitendo kizuri kitafuta kitendo kibaya, na kaa na watu kwa uzuri"  At-Tirmidhiy.

Sayyidina Ali Ibn Abi Taalib (radhiya Allahu anhu) aliulizwa nini maana ya uchamungu? Akajibu “ Kumuogopa Allah, Kufanyia kazi yaliyoteremshwa (Quraan na Sunna), na kuridhia kwa kidogo (alichoruzukiwa mtu na Allah), na kujiandaa na siku ya kuondoka(kifo).

Pia Sayyidina Umar Ibn Khattwaab (radhiya Allahu anhu) aliulizwa kuhusu uchamungu. Akamuuliza yule muulizaji nini utafanya ikiwa unatembea katika njia yenye miba? Yule mtu akajibu nitatembea kwa tahadhari ili isinichome miba. Sayyidina Umar akamwambia basi huo ndio uchamungu wakati unapoishi katika ulimwengu huu. Kwa maana yale yote ya haramu mtu anatakiwa achukue tahadhari nayo ili yasije kumuingiza katika moto. Na yale ya halali ndio sehemu ya mtu kuweka mguu wake.

Kwa ujumla kabisa Taqwa ni mtu kumuogopa Allah (subhanahu wataala) na kufanya yale yote aliyoamrishwa na kuwa mbali  na yale aliyokatazwa na Allah (subhanahu wataala).

NI YAPI MALIPO YA MWENYE KUMCHA ALLAH (SUBHANAHU WATAALA)

1- Kupata wepesi wa mambo yake kutoka kwa Allah (subhanahu wataal). Anasema Allah (subhanahu wataala)“Na anaye mcha Mwenyezi Mungu, Mwenyezi Mungu humfanyia mambo yake kuwa mepesi.” (65:4).
2- Kusamehewa dhambi zake na Allah (subhanahu wataala). Anasema Allah (subhanahu wataala) “Na anaye mcha Mwenyezi Mungu atamfutia maovu yake, na atampa ujira mkubwa.”(65:5).
3- Kupata njia ya kutokea katika mambo yake na kuruzukiwa bila ya kutarajiwa. Anasema Allah (subhanahu wataala) katika Suratu Twalaaq “na anaye mcha Mwenyezi Mungu humtengezea njia ya kutokea.(2) Na humruzuku kwa jiha asiyo tazamia…(3).
4- Kupata pepo ya Allah subhanahu wataala. Tujue kuwa ndani ya pepo ya Allah hatoingia ila yule ambae ni mchamungu. Anasema Allah (subhanahu wataala) :
“Na yakimbilieni maghfira ya Mola wenu Mlezi, na Pepo ambayo upana wake ni mbingu na ardhi, iliyo wekwa tayari kwa wachamngu,”(3:133).

“Hiyo ndiyo Pepo tutayo warithisha katika waja wetu walio kuwa wachamngu.”(19:63).

Na kwa upande wa hadithi kutoka kwa Abu Hurayrah (Radhiya Allaahu anhu) Amesema: Na aliulizwa Mtume (swalla Allahu ayahi wasallam ni kitu gani kitakachowaingiza watu kwa wingi peponi? Akasema: "Kumcha Mwenyeezi Mungu na tabia njema" Na akaulizwa tena ni kitu gani kitakachowaingiza watu wengi kwa wingi motoni? Akasema "kinywa (mdomo) na utupu." Imepokelewa na At-Tirmidhiy.

VIPI TUTAIPATA TAQWA NDANI YA RAMADHANI

Muislamu anaweza kuupata uchamungu kutoka kwenye Ramadhan kwanza kwa kufunga saumu yake kwa imani na kutarajai malipo kutoka kwa Allah. Unapofunga kwa imani unaamini kuwa hiyo ni amri ya Allah ambayo inatakiwa kutekelezwa kwa vile ambavyo Allah (subhanahu wataala) ameamrisha itekelezwe.

Mwenye kufunga kwa imani daima atakuwa ni mwenye kukaa mbali na kufanya na maasi. Pia kwa kutaraji malipo. Mwanadamu akiahidiwa pesa nzuri au mshahara mzuri kutokana na kazi yake atakayoifanya basi bila ya shaka atakuwa na jitihada kufanya kazi ile kwa uzuri wa hali ya juu kabisa. Je vipi ikiwa malipo yenyewe yanatoka kwa Allah? Bila ya shaka utakuwa ni mwenye jitihada za hali ya juu kabisa kwa sababu unajua unaemfanyia jambo hilo yeye hafaidiki na kitu ila wewe ndio unafaidika na pia wewe ndio unafaidika na malipo anakupa yeye. Tuangalieni uzito wa jambo hili.

Pili kuwa na Ikhlaas katika ibada zetu zote. Ikhlaas ni kufanya jambo kwa ajili ya Allah (subhanahu wataala) pekee. Na lazima mtu awe mbali kabisa na ajiepushe na masuala ya kujionesha. Sio mtu afunge ili watu wamuone. Au afanye jambo lolote la kheri kwa sababu tu watu wapate kumuona au kumsifia. Hayo ni makosa na muislamu hatakiwi kufanya hayo.

Tatu kujibidiisha katika kuswali sala za faradhi kwa uzuri na kwa khushui. Na pia kusali sala za Sunna. Mwenye kusali sala kwa khushui na kwa ajili ya Allah (subhanahu wataala) basi kwa hakika atakuwa mbali na maasi na ndipo atakapoweza kuupata uchamungu. Allah (subhanahu wataala) anasema “Hakika Sala inazuilia mambo machafu na maovu.”(29:45).

Kujibidiisha kufanya ya kheri ikiwemo kusoma quraan kutoa sadaka,kufanya umra na mengineyo.

Muislamu ajitahidi kufanya mambo kama haya ya kheri. Na mwisho abakie kumuomba Allah (subhanahu wataala) amjaalie awe miongoni mwa wacha mungu. Kwani bila ya tawfiq ya Allah hatuwezi kufika katika darja kama hizo.

Pia muislamu anatakiwa awe mbali kabisa na kujitukuza na kujiona kuwa yeye ni mchamungu kwa sababu tu anajitahidi kufanya ibada na anakuwa mbali na mambo ya haramu. Hakuna anaeweza kujijua kuwa yeye ni mchamungu isipokuwa Allah (subhanahu wataala) ndie anaetujua sisi. Anasema Allah (subhanahu wataala) “Basi msijisifu usafi. Yeye anamjua sana mwenye kujikinga na maovu “(53:32). Tuwe na tahadhari nalo sana. Muhimu ni kuwa na bidii na mwisho ni kumuomba dua Allah atuwafikishe katika hayo.

Allah atujaalie tuwe miongoni mwa wachamungu. Aaamin.

ISTIGHFAAR

Makala Imeandaliwa na Raudhwah Islamic Group


Kila sifa njema zinamstahikia Allah (subhanahu wa ta‘ala) Muumba wa kila kilichomo katika ulimwengu huu. Swala na salamu zimuendee Mtume wetu Muhammad (swalla Allahu alaihi wa sallam).

Nini maana ya Istighfaar.?

Sayyidina Ally (radhi za Allah ziwe juu yake) alimsikia mtu mmoja akisema: Astaghfirullah. Akamuuliza unajua maana ya Istighfaar? Naye akamuuliza nini maana yake ewe Amirul muuminiin? Akajibu Sayyidina Ally: “Istighfaar ni daraja la juu la uchamungu (ililyiin) nalo ni jina lenye maana ya vitu sita: Kwanza kujuta kwa yale makosa uliyoyafanya, Kuazimia kutorejea makosa uliyoyafanya, Kuwapa watu haki zao mpaka ukutane na Allah bila ya kubaki na deni hata moja, Kutekeleza fardhi zote kwa ukamilfu, usile haramu,Uonje  na utamu wa kutenda  mema kama ulivyoonja utamu wa maasi, ukishakuyatekeleza hayo ndipo useme: ASTAGHFIRULLAH hali ya kuwa unajua maana yake”.

Sayyidina Ally (radhi za Allah ziwe juu yake) ameelezea kwa undani ni nini maana ya mtu kusema Astaghfirullah. Wengi wetu tumekuwa tukitamka tu katika midomo yetu bila ya kujua maana yake.
Ni wajibu wetu waislamu kudumu na kufanya istighfaar daima na iwe kila siku. Kwani Mtume (swalla Allahu alayhi wasallam) ambae alisamehewa na Allah (subhanahu wataala) madhambi yake yaliyopita na yatakayokuja ila bado alikuwa akileta istighfaar kila siku. Je vipi sisi ambao daima ni wenye kumuasi Allah (subhanu wataala) usiku na mchana?  Imetoka kwa Abu Hurayrah (radhi za Allah ziwe juu yake) alimsikia Mtume (swalla Allahu alayhi wasallam) akisema: "Wallaahi mimi naomba maghfirah kwa Allaah na kutubu Kwake zaidi ya mara sabiini kwa siku" Bukhaariy

Sisi tunamuasi Allah (subhanahu wataala) na tunajisahau kuwa tutaondoka hapa duniani na ndio maana hatuandai mazingira ya kukutana na mola wetu. Daima tuwe ni wenye kudumu na istighfaar. Na iwe ni istighfaar kutoka ndani ya nyoyo zetu itakayothibitishwa na vitendo vyetu vyema. Istighfaar ndio jahazi la kumuokoa muumini katika dunia hii kutokana na maasi anayomuasi Allah (subhanahu wataala) asubuhi na usiku. Na ndio maana Mtume wetu (swalla Allahu alayhi wasallam) ambae ndio kigezo chetu akawa ni mwenye kudumu na istighfaar.

Anasema Sufyan “ Ajabu kwa mwenye kuzama na pamoja yake jahazi la kumuokoa.” Wakauliza walio pamoja nae “Na ni lipi hilo jahazi la uokovu? Akajibu ISTIGHFAAR”

MANENO YA KUMPA FARAJA MWENYE KUASI

Anasema Allah (subhanahu wataala) “ Sijapata kumghadhabia mtu kama ninavyomghadhabia mtu ambae anaona dhambi yake ni kubwa kuliko msamaha wa Allah”

Maneno haya yanatupa picha halisi kuwa Allah (subhanahu wataala) anataka aombwe msamaha na wala mtu asione kafanya kubwa ambalo hawezi kusamehewa na Allah. Juu ya lolote ambalo mtu amelifanya basi alete istighfaar kwa Allah (subhanahu wataala) nae atamsamehe kwani hakika ya Allah ni mwingi wa kusamehe. "Na hakika Mimi ni Mwingi wa Kusamehe kwa anayetubia, na akaamini, na akatenda mema, tena akaongoka" (Twaaha:82)

Imetoka kwa Anas (Radhiya Allahu anhu) ambaye amesema: Nimemsikia Mtume (Swalla Allahu alayhi waaalihi wasallam) akisema: "Amesema Allahِ: Ewe Mwanadam! Hakika ukiniomba na ukanitaraji (kwa malipo) Nitakusamehe yale yote uliyonayo na wala Sijali, Ewe Mwanadam! Lau zingefikia dhambi zako ukubwa wa mbingu, kisha ukaniomba msamaha, Ningekughufuria bila ya kujali (kiasi cha madhambi uliyoyafanya). Ewe Mwanadam, Hakika ungenijia na madhambi yakaribiayo ukubwa wa ardhi, kisha ukakutana nami na hali hukunishirikisha chochote, basi Nami Nitakujia na msamaha unaolingana nao"Imepokelewa na At-Tirmidh

Hivyo ndugu zangu wakiislamu daima tuwe ni wenye kuomba msamaha kikweli kwa Allah (subhanahu wataala) ili turudi kwa Allah akiwa yupo radhi na sisi na tusiwe wenye kukata tamaa na rehma za Allah (subhanahu wataala).

BAADHI YA ISTIGHFAAR MUHIMU
Bwana wa Istighfaar
Imetoka kwa Shaddaad Bin Aws (radhi za Allah ziwe juu yake) kwamba Mtume (swalla Allahu alayhi wasallam) kasema: Bwana wa Istighfaar  ni kusema: "Allaahumma Anta Rabbiy laa ilaaha illa Anta, Khalaqtaniy wa-ana ‘Abduka, wa-ana ‘alaa ‘Ahdika wa-Wa’dika mas-tatwa’tu. A’uudhu Bika min sharri maa swana’tu, abuu Laka Bini’matika ‘alayya wa abuu bidhambi, Faghfir-liy fainnahu laa yaghfirudh-dhunuuba illa Anta" 
Maana yake ni :
"Ee Allaah,  Wewe ni Mola wangu, hapana mola apasae kuabudiwa kwa haki ila Wewe, Umeniumba mimi na mimi ni mja Wako, nami niko juu ya  ahadi Yako, na agano lako, kiasi cha uwezo wangu, najilinda Kwako kutokana  na shari ya nilichokifanya, nakiri  Kwako kwa kunineemesha, na nakiri kwa madhambi yangu, basi nakuomba unisamehe kwani hasamehi madhambi ila Wewe"Bukhaariy.

Mtume (swalla Allahu alayhi wasallam) amesema " Yeyote atakaesema "ASTAGHFRIULLAHA LLADHY LAA ILAHA ILLA HUWAL HAYYUL QAYYUM WA-ATUBU ILAYHI"
“Namuomba msamaha Allah ambaye hapana mola apasae kuabudiwa kwa haki ila yeye, aliye hai aliyesimama kwa dhati yake, na ninatubia kwake”………Allah atamsamehe hata kama ana makosa ya kukimbia vitani’

DUA YA NABII YUNUS
Dua ya Nabii Yuunus (alayhis-salaam) alipokuwa tumboni mwa  samaki alisema maneno yafuatayo "Laa ilaaha illa Anta Subhaanaka inniy kuntu minadh-dhwaalimiyn"
“Hapana mungu isipo kuwa Wewe Subhaanaka Uliyetakasika. Hakika mimi nilikuwa miongoni mwa wenye kudhulumu"  (Suratul Anbiyaa: 87).

NI ZIPI FAIDA ZA ISTIGHFAAR?

Kutoka kwa Abdillah bin Abbas radhi za Allah ziwe juu yao amesema, amesema Mtume (swallalahu alayhi wasallam): “ Mwenye kuleta Istighfaar/akaomba msamaha, Allah humjaalia mtu huyo katika kila zito na tatizo apate ufunguzi, na kila tatizo atapata faraja, na atamruzuku bila ya yeye kutegemea.”
Hadithi hii inatuonesha kwa namna gani mtu anapoleta istighfaar na kuomba msamaha Allah humpa kheri tofauti tofauti.

Faida nyengine ya istighfaar tutaipata kutoka ndani ya Quraan kupitia kisa cha Hassan Al Basri.
Mtu wa kwanza alimuendea Hassan Al Basri akamuambia kuwa nina tatizo la mtoto Hassan Al basri akamjibu lete istighfaar.Mtu wa pili akamuendea Hassan Al Basri  akamwambia nina ugumu wa maisha na hali yangu ni maskini.Nini nifanye nipate wepesi? Akamwambia lete istighfaar.Mtu wa tatu akamuendea Hassan Al Basri akamwambia mazao yangu yanakauka na mvua hakuna.Nini nifanye?akamwambia lete istighfaar.Watu waliokuwa wakisikia yale majibu wakamwambia vipi leo mbona kila anaekuja na jambo lake unamwambia lete istighfaar.au hujui nini wafanye? Hassan Al Basri akawajibu hivi mumesahau katika Suratu Nuuh aya 9-12 ya ALLAH aliwaambia waja wake walete istighfaar ili wapate watoto,wapate mali na wapate mvua kwa ajili ya mazao yao.” Nikasema: Ombeni msamaha kwa Mola wenu Mlezi; hakika Yeye ni Mwingi wa kusamehe(10) Atakuleteeni mvua inyeshe mfululizo.(11) Na atakupeni mali na wana, na atakupeni mabustani na atakufanyieni mito.(12).

Hii yote inaonyesha jinsi gani madhambi ndio yanayoleta balaa na mitihani duniani, kama ni bakora na adhabu kwa watu kama Allah alivoeleza kisa cha watu wa bustani na visa vya kaumu zilizopita, baada ya kukufuru na kutenda dhambi Allah aliwapa njaa na kiu pamoja ukame. Ila njia pekee ni kurudi kwa Allah (subhanahu wataala) na kuleta istighfaar.

Usiende kwa mganga kumshirikisha Allah ewe mwanadamu una matatizo, mambo yako hayakai vizuri basi kimbilia kuleta istighfaar ya kweli kutoka ndani ya moyo basi Allah (subhanahu wataala) atakusamehe dhambi zako na atakuneemesha neema mbali mbali kama alivyosema katika Quraan.

Hizi fadhila na faida kubwa katika istighfaar pale mja anapoomba msamaha kwa mola wake subhaanahuu wataala. Je ni wangapi ambao huleta istighfaar na wakapata kheri na neema hizi alizoahidi Allah (subhaanahuu wataala). Daima tudumu na kuleta ISTIGHFAAR.

Allah ni mjuzi zaidi.

VIPI UTAIPA NGUVU IMANI YAKO

Makala imeandaliwa na Raudhwah Islamic Group

Kila sifa njema zinamstahikia Allah Mola wa viumbe vyote. Sala na salamu zimuendee Mtume wetu Muhammad (swalla Allahu alaihi wa sallam) na ahli zake na maswahaba wake.

Imani ya mja huwa inapanda na kushuka. Na hii ni miongoni mwa tabia za muislamu. Kuna wakati muislamu imani yake humjaa na huwa anajitahidi katika Ibada. Sala tano hazimpiti tena kwa jamaa. Funga za sunna huwa ndio vazi lake. Adhkaar na sala za usiku ndio mapambo yake. Lakini baada ya muda haya mambo yote huwa hayafanyi tena. Na huanza uvivu wa kutekeleza mambo hayo.

Wengine wao huwa na imani kubwa sana na hamu ya kutenda matendo mema na nia hasa pale wanapokumbushwa. Ila baada ya muda hamu ile ya kufanya ibada inapotea. Lakini hawa wote tujiulize ni kipi kinachowafanya wawe hivyo? Tatizo lao ni udhaifu wa imani au kushuka kwa imani. Imani inapokuwa juu basi ndipo kheri zote huzikimbilia au ndipo hamu ya kufanya ibada humjaa mtu. Lakini imani inaposhuka basi huyu mtu huwa hana tena hamu ya mambo hayo na huwa na uvivu. Sasa nini afanye ili aipe nguvu imani yake? Leo katika makala hii tutajaribu kuelezea baadhi ya njia ambazo muislamu anaweza kuzifanya ili aweze kuipa nguvu imani yake. Njia zenyewe ni kama zifuatazo :

1-Kusoma Quraan kwa mazingatio
Endapo muislamu anapohisi imani yake imeshuka au inatetereka basi akimbilie kusoma sana Quraan. Ila aisome Quraan kwa mazingatio kwa kujua ni kipi ambacho Allah (subhanahu wataala) anakielezea ndani ya Quraan. Na ikiwa mtu hajui tafsiri ya Quraan basi asome kwa kutumia msahafu wa tafsiri.

Hakuna yeyote ambae amesoma Quraan kwa mazingatio isipokuwa umelainika moyo wake. Na hapo ndipo sifa ya muum,ni inapopatika. Na endapo ukaona kuwa unasoma Quraan na moyo wako hauathiriki na chochote basi jua wewe ni  maiti inayotembea duniani. Allah (subhanahu wataala) anasema “Hakika Waumini ni wale ambao anapo tajwa Mwenyezi Mungu nyoyo zao hujaa khofu, na wanapo somewa Aya zake huwazidisha Imani, na wakamtegemea Mola wao Mlezi.” (8:2). Aya hii inaonesha wazi kuwa yeyote yule anaesoma Quraan kwa ufahamu na mazingatio basi kwa hakika imani yake itapanda.

Pia Allah (subhanahu wataala) anasema ndani ya Suratu Muhammad aya ya 24 “Je! Hawaizingatii hii Qur'ani? Au kwenye nyoyo (zao) zipo kufuli?” Je sisi waumini hatuna mazingatio na aya za Allah? Au nyoyo zetu zimefungwa? Ndipo Allah akauliza au zina kufuli? Kwa maana zimefungika hakuna ndani yake kinachoingia. Tujitahidini tulainishe nyoyo zetu ili Quraan iwe ni ukumbusho kwetu.

Vipi watu wema walikuwa wakiathirika kwa kusoma Quraan kwa mazingatio ? Tuangalie mifano ifuatayo halafu tujiulize na sisi nafsi zetu zipo sehemu gani?

Siku moja Sayyidina Omar (radhiya Allahu anhu) alikuwa akiisoma aya katika aya za Quraan. Alipozisoma akaanza kulia na kulia. Mpaka akawa anashindwa kutoka nje ya nyumba yake kwa sababu ya kilio alichokuwa nacho. Je alilia tu bure bure? Hapana alilia kwa sababu aliyafahamu maneno ya Allah kwa upeo wa juu na akawa anajiuliza vipi yeye hali yake itakuwa. Aya yenyewe aliyoisoma ni  “Hakika adhabu ya Mola wako Mlezi hapana shaka itatokea.(7) Hapana wa kuizuia.(8). Machozi yake yalishindwa kujizuia akikaa akijiuliza vipi adhabu za Allah (subhanahu wataala) zitakuwa. Vipi mimi na wewe tunapozisoma aya kama hizi? Je nyoyo zetu hazipaswi kunyenyekea na kuwa na mazingatio?

Tumuangalie nae Omar Ibn Abdul Aziz. Siku moja Omar Ibn Abdul Aziz alisikilikana analia kwa sauti na kushindwa kujizuia.Jirani yake akaenda kumuuliza “Je ni kipi kimekusibu hadi unalia?”Omar Ibn Abdul Aziz akamwambia ”Hakuna kinachoniliza isipokuwa aya hii ndani ya Quraan,Allah(subhanahu wataala)anasema “…Na uhadharishe na Siku ya Mkutano, haina shaka hiyo. Kundi moja litakuwa Peponi, na kundi jengine Motoni”(42:7).Najiuliza ndani ya nafsi yangu je nitakuwa katika kundi lipi kati ya haya mawili?.

Hebu tuangalie vipi wenzetu wamekuwa wakiathirika na kusoma Quraan. Vipi mimi na wewe? Je hatuzipiti aya hizi? Je tunaisoma Quraan kwa mazingatio? Hawa ni wachache tu ambao wanaathirika kwa kusoma Quraan. Mifano ipo mingi ndugu zangu wakiislamu. Tujitahidini sana kuisoma Quraan kwa mazingatio ili tuweze kuzikuza imani zetu.

2- KUKITHIRISHA KUKUMBUKA MAUTI

Mauti ni safari ya lazima kwa kila mwanadamu. Nayo ni safari ya kutoka katika dunia katika maisha ya mpito na kuelekea katika maisha ya akhera. Mwanadamu yanapomkuta mauti basi muda wa mtihani wake ndio unakuwa umekwisha na kinachobaki ni kwenda kukutana na hesabu. Je ulishwahi kujiuliza ni vipi roho yako itatolewa? Itatolewa kwa ajili ya kwenda jannah au itatolewa kwa ajili ya kwenda motoni? Je ulishawahi kujiuliza vipi itakuwa hali yake pale utakapokuwa umebebwa kwenye jeneza? Je ulishawahi kukaa na kujiuliza vipi utaikuta hesabu yako? Je umeshawahi kujiuliza nini utamjibu Allah pale utakaposimamishwa mbele yake? Mauti ni mazingatio tosha kwa muislamu na kumkumbusha ili aweze kukaa katika njia ya Allah (subhanahu wataala).

Mtihani mkubwa zaidi ni watu kuyachukia mauti. Na wapokuwa wakikumbushwa kuhusu mauti huwa wanachukia na kuona Sheikh hakuwa na mawaidha ila ya kuwatisha. Kumbe wanasahau kukumbushwa mauti ni kumfanya mtu aizidishe imani yake na kujiandaa na siku ya kutoka roho. 

Mtume (swalla Allahu alayhi wasallam) anasema katika hadithi “ Kithirisheni katika kukumbuka chenye kukata ladha “ Mtume (swalla Allahu alayhi wasallam) ameyaita mauti kama ni kikata ladha. Ndiyo mauti ni yenye kukata ladha ya starehe za uongo za dunia. Mwnadamu anapokumbuka mauti basi awe anajiuliza masuala ya msingi ambayo atakutana nayo. Na endapo muislamu ataona kuwa hata akikukumbuka mauti moyo wake hauthiriki basi pi ana yeye ataingia katika kundi la wale maiti wanaotembea katika dunia hii.
Anasema Allah (subhanahu wataala) ““Kila nafsi itaonja mauti. Na bila shaka mtapewa ujira wenu kamili Siku ya Qiyaama.”(3:185).

Tujiandaeni mauti na tujitahidini katika kukithirisha kukumbuka mauti kila wakati hili litamsaidia muumini na kumuasi Allah (subhanahu wataala).

3-KUTEMBELEA MAKABURI

Makaburi nayo yana siri nzito ndani yake. Tayari tumeshamuhifadhi ndugu yetu katika kuelekea katika maisha yake ya milele. Nini kinachojiri ndani ya mauti. Mwanadamu atakapokaa na kuliwaza kaburi, giza lake na juu yake kufukiwa na michanga. Vipi atakaa ndani ya shimo hilo?  Je ulishawahi kujiuliza vipi itakuwa usiku wa kwanza ndani ya kaburi lako?Je wakati watu watakapokuwa washamzika ataweza kujibu maswali ya Munkar na Nakir? Je kaburi lake litakuwa ni bustani katika bustani ya peponi au mashimo katika mashimo ya motoni?

Mtume (swalla Allahu alayhi wasallam) ametuusia kutembelea makaburi pale aliposema “Mtume (Swalla Allaahu alayhi wa aalihi wasallam) amesema, “Nilikuwa nimewakataza kwanza kuzuru makaburi lakini kuanzia sasa yatembeleeni.” (Muslim) katika riwaya nyingine , “Kwani huko kuzuru makaburu hukukumbusheni na akhera.” (Ahmad) .Kutembelea huku sio ule wakati wa kwenda kuzika. Mtu awe anapanga siku maalum kwenda kuyatembelea makaburi kwa lengo iwe ni mazingatio kwake yeye. Kwa lengo na yeye ajiulize vipi itakuwa hali yake pale atakapowekwa ndani ya kaburi.

Sayyidina Othman Ibn Affan (radhiya Allahu anhu) alikuwa akitajiwa kuhusu moto na adhabu za Allah analia. Lakini anapotembelea makaburi huwa analia zaidi mpaka ndevu zake zikarowa machozi. Maswahaba wakamuuliza ni kipi kinachomfanya hivyo ? Sayyidina Othman akajibu kaburi ndio nyumba ya kwanza ya maisha ya akhera. Ikitengenea hali ndani ya kaburi ndio yametengenea mengine na hali ikiwa mbaya basi ndio mwanadamu amekhasirika. Sasa najiuliza vipi kaburi langu litakuwa?

Mmoja ya watu wema alikuwa akiingia sehemu ya makaburi basi huuziba uso wake kwa kilemba chake. Kwa nini huuzibaa? Ili asionekane akilia kwani alikuwa anashindwa kujizuia asilie akikaa akiliwaza kaburi lake. Litakuwa na hali gani.

Hawa ndio ambao wakikumbuka vitu kama hivi huvikumbuka kwa mazingatio makubwa ndani yake. Je vipi mimi na wewe? Sio wale ambao tunaenda kwenye makaburi na simu zetu za kuchat mkononi? Sio sisi tunaenda kwenye makaburi na mazungumzo ya kusema watu yapo kwenye midomo yetu?
Tembelea makaburi ili uizidshe imani na uwe ni mwenye kujiandaa daima na kukaa katika kaburi lako.

4- KUKAA NA MARAFIKI WEMA NA KUSHIRIKI VIKAO VYA KHERI

Rafiki huchangia kwa kiwango kikubwa maisha ya binaadamu. Na hili linathibitishwa na Mtume Muhammad(swalla Allahu alayhi wasallam) kwa kauli yake pale aliposema “ Mtu hufuata mwenendo wa rafiki yake,basi aangalie mmoja wenu ni nani anaemfanya kuwa ni rafiki” Attirmidhy.

Jitahidi sana na kuwaepuka marafiki waovu kwani hawawezi kukusaidia katika kuikuza imani yako. Kaa na rafiki mwema rafiki ambae daima atakuwa ni mwenye kukuhimiza katika kufanya yalo mema na yaliyo mazuri. Tumeona mifano ya wengi ambao wamepotoka kwa sababu tu ya marafiki.

Na Allah (subhanahu wataala) anatuambia ndani ya Quraan “Wala usimt'ii tuliye mghafilisha moyo wake asitukumbuke, na akafuata matamanio yake yakawa yamepita mpaka.”(18:28). Aya hii ni ukumbusho kwa muumini awe mbali na wale ambao hawako katika kumtii Allah (subhanahu wataala) nao hufuata matamanio ya nafsi zao.

Mtume (swalla Allahu alayhi wasallam) anasema "Mfano wa rafiki mwema na rafiki mbaya ni kama ule wa muuzaji wa misk na mhunzi. Basi kwa muuzaji wa misk, imma atakunusisha, au utanunua kwake ama angalau utafurahia harufu nzuri kwake. Na kwa yule mhunzi, imma atakuchomea nguo au utapata harufu mbaya kutoka kwake.” [Al-Bukhaariy na Muslim].

Katika tafsiri ya Hadiyth hii, Imam An-Nawawiy alisema: Mtume ((Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam)) alilinganisha rafiki mzuri na muuzaji misk kwasababu, kwa rafiki mzuri mwenye tabia ya upole, na elimu, utapata faida kwake. Na Mtume (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) alitukataza kukaa na wale wenye kufanya maovu.

Hivyo ndugu yangu muislamu tafuta rafiki mwema ambae daima mazungumzo yenu yatakuwa ni ya kheri na ni yenye kuhimizana kufanya mema na kukumbushana pale mtu anapokosea.

Pia kushiriki katika vikao vya kheri katika misikiti,kwenda katika mihadhara kwani katika vikao hivyo hukumbushwa yaliyo mema na kukatazwa yaliyo mabaya ambayo mtu yatamfaa katika maisha yake ya dunia na kesho akhera. Na tusichoke kuhudhuria kwa wingi na kwa wakati mwingi kama vile tunavyotumia wakati mwingi katika kuangalia michezo,mipira au kupoteza wakati kwa kuchat na ndani ya facebook.
Mwisho kabisa ndugu yangu wa kiislamu nakuusia mambo mawili. Jambo la kwanza kithirisha sana katika kumuomba dua Allah (subhanahu wataala) katika kuifanya imani yako isiwe yenye kutetereka na aijaalie imani yako iwe ni yenye kuzidi pale unapokutana na misukosuko. Pia kuwa ni mwenye kuihesabu nafsi yako daima kabla ya kulala hii itasaidia katika kukuzindua ni kwa kiasi gani uko mbali na Allah. Na hesabu hiyo uwe unaifanya ni sababu ya wewe kujiepusha na maasi yale ambayo umeyatenda.

Namuomba Allah atujaalie imani zetu ziwe thabiti na aturidhie pale tutapoondoka hapa duniani. Aaamin.

KWA NINI HATUATHIRIKI NA FUNGA ZETU?

Makala Imeandaliwa na Raudhwah Islamic Group

Kila sifa njema zinamstahikia Allah Mola wa viumbe vyote. Sala na salamu zimuendee Mtume wetu Muhammad (swalla Allahu alaihi wa sallam) na ahli zake na maswahaba wake.

Allah (subhanahu wataala) ametufaradhishia juu yetu kufunga. Na pale alipotufaradhishia akatuambia kuwa lengo kuu la kutufaradhishia funga ni kupata uchamungu(Taqwa). Pale aliposema “Enyi mlio amini! Mmeandikiwa Saumu, kama waliyo andikiwa walio kuwa kabla yenu ili mpate kuchamngu.”(2:183).
Analolisema Allah (subhanahu wataala) lazima tuliamini na mwenye kuwa na shaka na kauli za Allah (subhanahu wataala) basi huyo anatoka kwenye uislamu. Funga kwa uhakika lengo lake ni kutufanya sisi tuwe wachamungu. Lakini masuali ya kujiuliza Je kweli tunakuwa wachamungu? Je tunaathirika na funga zetu? Malengo mengine ya saum Je tunayafikia?

Majibu ni wachache wenye kufikia hayo na kutambua hayo. Ila ni yapi hasa matatizo yanayotufanya tusifikie malengo ya funga?. Leo katika makala hii tutaelezea miongoni mwa sababu ambazo zinapelekea waislamu kutopata matunda ya funga zetu na kutoathirika nazo.
Ama sababu zwenyewe ni :

1-KUTOWEZA KUTAMBUA THAMANI YA MUISLAMU KUIDIRIKI RAMADHAN
Mwanadamu anapojua thamani ya kitu huwa ni mwenye kukithamini kitu kile pia na kuwa na tahadhari ya juu ili kitu kile kisiweze kupata madhara. Chukulia mfano mtu amepata Almasi vipi atakuwa mwenye kuithamini? Kwa vile anajua thamani ya almasi ni kubwa hivyo atakuwa na tahadhari ya hali ya juu asije kuitupa hali kadhalika atakuwa ni mwenye furaha kwani anajua kuwa almasi ile inaweza kuwa sababu ya kuondoka umasikini wake.

Tuje kwenye Ramadhan wengi wetu hatujui thamani ya Ramadhan na ndio maana hatuuthamini au wenye kujua thamani ya mwezi huo basi hawaupi ile thamani inayostahiki. Nizungumzie mawili tu katika mengi ambayo tunayapata ndani ya Ramadhan. La kwanza ni usiku wenye cheo. Anasema Allah (subhanahu wataala) “Hakika Sisi Tumeiteremsha (Qur-aan) katika Laylatil-Qadr (usiku wa cheo). Na nini kitakachokujulisha ni nini huo (usiku wa) Laylatul-Qadr? (Usiku wa) Laylatul-Qadr ni (usiku) mbora kuliko miezi elfu Wanateremka humo Malaika na Ruwh (Jibriyl) kwa idhini ya Mola wao kwa kila amri (jambo). (Usiku huo ni) Amani mpaka kuchomoza Alfajiri. (Al-Qadr: 97). Ni nani asiyeutaka usiku huu umkute ikiwa yumo ndani ya Ibada? Tunatambua uzito wake ila hatuoneshi thamani yake kivitendo. Bali vitanda vyetu ndivyo tunavyovithamini.

Ama jambo la pili ni kutoka katika hadithi sahihi ya Mtume (swalla Allahu alayhi wasallam) iliyopokelewa na Bukhari,Muslim na Nasai Rahimahumullah na kusimuliwa na Abu-Hurayra radhiallahu anhu :“Yoyote atakaefunga Ramadhan, kwa imani na kwa kutarajia malipo atasamehewa dhambi zake zilotangulia”.

Wako wasiyoyajua haya ndio maana hawauthamini na wako wenye kujua ila hawafanyi bidii za kuonesha thamani ya mwezi wa Ramadhan.
Hivyo basi Yule mwenye kutaka kupata uchamungu basi kwanza authamini. Na kuuthamini kwenye kuwe kwa vitendo vyema na ibada hapo ndipo mja ataweza kufikia lengo la funga.

2-KUTOJIANDAA NA KUIPOKEA MWEZI WA RAMADHAN

Ramadhan inahitaji maandalizi. Maandalizi yanayoihitaji kwanza ya kielimu. Ni lazima mwenye kutaka kufunga ajue nguzo za funga,yanayobatilisha funga,yaliyo sunna kwa mwenye kufunga. Mambo haya mtu akiyajua basi alau atakuwa anajua nini anachokifanya ndani ya funga.

La muhimu zaidi katika yaliyosahaulika na ni ambalo lenye kufunguza ajue maneno machafu na kusema uongo pia nayo yanafunguza.. Mtume (swalla Allahu alayhi wasallam) inayosema " Yule ambae haachi kusema uongo na haachi vitendo viovu. Allah (subhanahu wataala) hana haja na funga yake." Bukhari na Muslim. Ikiwa mwenye kufunga hayajui haya vipi ataweza kuyachunga ikiwa kusema uongo ni haramu halafu yeye ndio imekuwa ada yake? Vipi unadhani mtu kama huyu anaweza kufikia malengo ya funga?

Maandalizi mengine ni ya kimwili. Wako baadhi ya watu miili yao imeshalemaa haiwezi kabisa kuamka usiku. Haiwezi kabisa kuacha vitanda na kumuabudu Allah (subhanahu wataala) katika thuluthi ya mwisho ya usiku. Lazima mwanadamu auzoeshe mwili wake kutopenda kitanda na awe ananyanyuka kusali usiku kabla ya Ramadhan kuingia ili ramadhan ikifika awe ni mwenye kuendelea tu na ibada.

Jambo hili la maandalizi wengi wetu yamekuwa ni madogo bali tumekuwa ni wazuri wa kujiandaa na vyakula na nguo za sikukuu na tunaisahau kabisa Ramadhan. Tusikubali kutekwa na nafsi zetu lazima turejeshe mioyo yetu kwa ajili ya kupata kheri za Ramadhan.

3-KUTOKUWA NA MAAMUZI YA KIUKWELI YA KUBADILIKA NAFSI ZETU

Maamuzi ya kikweli yanakosekana ndani ya Ramadhan. Mtu husema ndani ya nafsi yake Ramadhan hii ikifika nataka nijibadilishe kabisa. Lakini maneno haya huwa ni kutoka katika ulimi tu ila ndani ya moyo huwa hayapo.

Mwenye kutaka kubadilika kwa haki basi lazima atakuwa na bidii ya hali ya juu. Na mwenye kujitahidi katika njia ya Allah basi lazima atafanikiwa. Allah (subhanahu wataala) anasema “Na wanao fanya juhudi kwa ajili yetu, Sisi tutawaongoa kwenye njia zetu. Na hakika Mwenyezi Mungu yu pamoja na watu wema” (Ankabut : 69).

Maneno ya Allah ni ya kweli na daima yataendelea kubakia kuwa ni ya kweli. Suali la kujiuliza ikiwa Allah (subhanahu wataala) ametuambia hayo je kweli sisi tunayo dhamira ya kweli katika kubadilika? Au kutaka kubadilika kwetu huwa ni maneno tu kutoka katika vinywa vyetu na sio kutoka ndani ya nyoyo zetu?

Vipi mwenye kutaka kubadilika bado anaendelea kuyafanya yale ya haramu anayotaka kuyawacha. Vipi mwenye kutaka kubadilika bado anaendelea kukaa na marafiki waovu? Vipi mwenye kutaka kubadilika hajihimizi na vikao vya kheri,kusoma Quraan?

Mwezi wa Rehma wenye fadhila nyingi ni miongoni mwa sababu kubwa ya kumfanya mja aweze kubadilika. Tusikose kuitumia fursa hii kwani hatujui kuweza kufika ramadhan ijayo.

4-KUJISHUGHULISHA ZAIDI NA DUNIA NA KUSAHAU IBADA

Unapoingia mwezi wa Ramadhan muislamu lazima ajipange vizuri ili adumishe ibada. Ila sisi dunia imetuteka na ndio maana hatufikii malengo ya funga. Mfanyabiashara anajua ndio mwezi wa kuchuma pesa akili yote ipo katika kuutafuta mzigo wa kuuza, wengine ndio wanaona mwezi wa kuwakomoa watu na bei. Wanunuzi nao wanawaza kwenda kununua na ndio maana kwenye maduka watu wanajaa katika mwezi  wa Ramadhan.

Sisemi watu wasinunue na wasiuze bali wajipangie vizuri ili wapate na alau muda wa mtu kufanya ibada. Mfanyabiashara daima ajiweke vizuri mapema kabla ya kuingia Ramadhan ili ikifika ramadhan asiwe mwenye kushughulishwa. Na mnunuzi nae ajipangie vizuri. Unapohangaika kutwa nzima bila ya kupumzika basi usidhanie kama utapata alau muda wa kumuabudu Allah kwani machofu yatatawala katika mwili wako.
Pia mambo yote ya haramu tunayaweka usiku baada ya kumaliza kuftari. Sasa vipi mtu anafunga lakini baada ya funga tu magharibi anayakimbilia maasi. Huku ni kuipenda dunia na kusahau akhera.
Tusipe thamani kubwa dunia itatupeleka pabaya enyi ndugu zangu wa kiislamu. Daima tuwe wenye kujishughulisha na ibada kwani ndizo zitakazotufaa siku ya Qiyama.

5-KUPOTEZA WAKATI KATIKA MAMBO YASIYOKUWA NA MSINGI

Wakati ni jambo muhimu sana katika maisha ya mwanadamu ndio maana Allah (subhanahu wataala) ameapa na wakati ndani ya sura mbali mbali. Mwanadamu unapokwisha wakati wake wa kuishi duniani ndio mauti yake yamefika na anaondoka katika dunia.

Ni wachache kati yetu wenye kujua thamani ya wakati na kuutumia vizuri wakati wetu. Wengi kati yetu tumekuwa ni wenye kuupoteza wakati wetu katika mambo yasiyokuwa na maana. Funga na malengo yake ili tuweze kupata fadhila zake na kufikia malengo yake ni lazima tuutumie wakati wetu katika kheri kwa kufanya ibada na kusoma Quraan,na ibada nyengine za kheri.

Sasa ikiwa tunafunga ili tufikie lengo la kumcha Allah (subhanahu watala), kwa nini waislamu wanatumia wakati wao katika michezo ya kipuuzi ikiwemo kuangalia mipira, kuangalia sinema zisizokuwa na maana, kucheza makeram, karata, zumna nk. Sasa vitu hivi vinatupelekea kusahau lengo  la funga kwa sababu ya kupoteza wakati mwingi katika mambo hayo. Kwani wakati huo ungetafuta la kheri ungekuwa umejichumia thawabu ngapi? Na wengine husema kabisa anafanya hayo ili wakati upotee funga yake isiwe tabu kwake.

Kwa hiyo ndugu zangu wakiislamu hatutaathirika na funga kwa sababu tuanaendekeza anasa za kidunia na tunaacha  mambo yanayotupelekea tupate huo uchamungu tuliouelezea.

Lau tungejua yale ambayo yamo ndani ya mwezi wa Ramadhan tusingeiwacha hata sekunde moja ndani ya mwezi huu itupite bila ya mtu kufanya kheri.

Nasaha kwenu enyi ndugu zangu wakiislamu lengo la funga ni kumcha Allah kama alivyosema Allah katika Quraan Uchamungu hauji tu kwa kutamani bali kuna sababu nyingi zitakazo kufanya uupate uchamungu. Sababu zenyewe pale unapofunga basi uwe ni mwenye kudumisha ibada za faradhi na unajishughulisha na kufanya ibada mbali mbali za sunna, kama kusoma Qur-an, kuswali sala za sunna,kutoa sadaka, kuleta dhikri nk. Na hizi ndizo ibada zitakazokupelekea upate lile lengo la funga.

Tujitahidini kuzifanya kwa hima na tumuombe Allah (subhanahu wataala) atuwafikishe katika hayo.

Monday 7 July 2014

MILANGO YA KHERI NDANI YA RAMADHAN


   Makala imeandaliwa na Raudhwah Islamic Group

MILANGO YA KHERI NDANI YA RAMADHANI

Kila sifa njema zinamstahikia Allah Mola wa viumbe vyote. Sala na salamu zimuendee Mtume wetu Muhammad (swalla Allahu alaihi wa sallam) na ahli zake na maswahaba wake.

Milango ya kheri ndani ya Ramadhani hii ni milango ambayo muislamu ajitahidi aifungue na aingie ndani yake kwa ajili ya kupata radhi za Allah (subhanahu wataala) pia kwa ajili ya kupata matunda ya mwezi mtukufu wa Ramadhani. Milango ya kheri ndani ya Ramadhani ni mingi mno. Ila tutaielezea baadhi ambayo muislamu ajitahidi aifanyie kazi.

1-KUFUNGA KWA IMANI NA KUTARAJI MALIPO

Jambo la kwanza kabisa ambao muislamu anatakiwa alifanye ni kufunga Ramadhani kwa imani na kwa kutaraji malipo. Mwenye kufunga kwa imani na kutaraji malipo basi husamehewa dhambi zake zote zilizopita. Kwa ushahidi amesema Mtume (swalla Allahu alayhi wasallam)katika hadith sahihi, iliyopokelewa na Bukhari,Muslim na Nasai Rahimahumullah na kusimuliwa na Abu-Hurayra radhiallahu anhu :“Yoyote atakaefunga Ramadhan, kwa imani na kwa kutarajia malipo atasamehewa dhambi zake zilotangulia”.
Hili ni jambo la kwanza muhimu kabisa mtu alifanye ili aweze kusamehewa dhambi zake.

2-KUSALI SALA ZA USIKU
Muislamu ajitahidi sana kusali tarawehe,sala za usiku (tahajjud). Mtume (Swalla Allaahu alayhi waaalihi wasallaam) amesema:  "Atakayesimama (kwa Swalah ya usiku) kwa imani na kutaraji malipo, atasamehewa madhambi yake yaliyotangulia" Bukhaariy na Muslim

Sala ya tahajjud hii ni sala inayosaliwa wakati wa usiku katika thuluthi ya tatu ya usiku, kuanzia saa saba mpaka saa kumi na sunna zaidi mtu alale aamke.

Na sala hii husaliwa rakaa nane na kumalizia rakaa za witri 1,3,5 kwa rakaa mbili mbili na kumaliza na rakka moja ya witri, au tatu au tano.

Kwa ushahidi wa hadithi aliyopokea Ibnu Abbas radhi za Allah ziwe juu yake anasema, “Nilienda kumtembelea Mtume Swallalahu alayhi wasallam tukalala usiku wake akaamka akatia udhu wa kuswali, akasimama kisimamo cha rakaa mbili, akaatoa salamu, akasali tena rakaa mbili refu zaidi kuliko za mwanzo, akafanya hivo mpaka rakaa nane, ndipo akasimama kuswali rakaa moja, riwaya nyengine akasali rakaa tatu mfululizo  bila ya kutoa  salamu.

Sala hizi zote mtu akisali humuweka karibu mja na Allah subhaanahuu wataala na kupanda darja katika imani na uchamungu.

3-KUMFTARISHA YULE ALIYEFUNGA

Amesema mtume swallalahu alyhi wasallam “Atakayemfutarisha aliyefunga , atapata ujira sawa na Yule aliyefunga bila ya kupungua chochote katika ujira wa Yule aliyefunga” ıimepokelewa na Imam Ahmad na Annasaiy).

Wengi wa watu wanajisahau hapa. Watu huwaftarisha wale wenye uwezo na kusahau maskini. Ili mtu apate ujira zaidi basi awe ni mwenye kuwaftarisha wale wahitaji zaidi. Kwani ndani ya jamii zetu kuna watu wanafunga lakini ftari zao hawajui n inini kwa sababu ya umaskini.

4-KUKAA ITIKAFU KATIKA MSIKITI

Kutoka kwa bibi A’aisha radhi za Allah ziwe juu yake amesema: “Alikuwa Mtume swallalahu alyhi wassalam  akikaa itikaafu katika kumi la mwisho wa mwezi wa Ramadhani, na mwaka ambao aliondoka duniani alikaa siku ishiriini” (Imepokelewa na Imam Bukhary)

Hadithi inaonesha fadhila za iitikafu nayo ni kukaa kikao katika msikiti kwa kuleta adhkaar, kusoma qur-an, kusikiliza mawaidha, kusoma darsa za dini nk.

Kufanya hivi mtu huandikiwa thawabu kwa muda wote aliokaa katika masjid mpaka atakapoondoka.
5- USIKU WENYE CHEO (LAYLATUL QADRI)

Laylatul Qadri ni usiku mmoja ndani ya mwezi wa Ramadhan. Usiku huu ni usiku bora kwa zaidi ya miezi elfu moja (miaka 83) kwa usiku wa kawaida. Anasema Allah (subhanahu wataala) “Hakika Sisi Tumeiteremsha (Qur-aan) katika Laylatil-Qadr (usiku wa cheo). Na nini kitakachokujulisha ni nini huo (usiku wa) Laylatul-Qadr? (Usiku wa) Laylatul-Qadr ni (usiku) mbora kuliko miezi elfu Wanateremka humo Malaika na Ruwh (Jibriyl) kwa idhini ya Mola wao kwa kila amri (jambo). (Usiku huo ni) Amani mpaka kuchomoza Alfajiri. (Al-Qadr: 97).

Yeyote utakaomdiriki usiku huu anafanya ibada basi Allah (subhanahu wataala) anamuandikia ibada zake sawa na ibada ya miaka 83. Imehisabiwa mtu atakapofanya ibada katika usiku huo mmoja ni kama amefanya ibada sawa na miaka 83 na hii ni katika fadhila kubwa kabisa. Na katika kitabu Muwatwaa, Imamu Maalik  amesema. Mtume (Swalla Allaahu 'alayhi wa sallam) ameona umri wa umma za mwanzo ni mrefu, na umri wa ummah wake ni mfupi akapewa usiku wa Laylatul-Qadr uwe ni bora kuliko miezi elfu.

Usiku huu haujulikani lini ila kauli yenye nguvu zaidi ni kumi la mwisho ndani ya ramadhani. Ili muislamu aweze kuupata usiku huu basi awe ni mwenye kufanya ibada kwa wingi nyakati za usiku. Na azidishe zaidi katika kumi la mwisho wa Ramadhani.

6- KUKITHIRISHA KUSOMA QURAAN

Muislamu ajitahidi sana kusoma Quraan tena aisome kwa mazingatio. Mwezi wa Ramadhan ndio mwezi ambao imeteremshwa Quraan. Anasema Allah (subhanahu wataala)” Mwezi wa Ramadhaan ambao imeteremshwa humo Qur-aan ili iwe Hidaaya kwa watu na hoja bayana za Hidaaya na Al-Furqaan (Upambanuzi). (Al-Baqarah: 185).

7- AKITHIRISHE KUTOA SADAKA
Mtume (Swalla Allaahu alayhi waaalihi wasallaam) amesema: "Sadaka iliyo bora  ni ile inayotolewa katika mwezi wa Ramadhaan" At-Tirmidhiy.

8- KUKITHIRISHA KULETA ISTIGHFAAR

Muislamu aitumie vizuri fursa ya Ramadhan kumuomba msamaha Allah (subhanahu wataala) kutoka na makosa yake. Hivyo basi akithirishe kuleta istighfaar. Ili asije akaingia katika wale wanaokula khasara. Mtume (swalla Allahu alayhi wasallam) aliitikia Aamin kutokana na dua iliyoombwa na Jibril kuwa amekula khasara yeyote yule ambae ameidiriki ramadhani na hakusamehewa dhambi zake.

Na nyakati nzuri zam tu kuleta istighfaar ni katika thuluthi ya mwisho ya usiku. Anasema Allah (subhanahu wataala) “Na kabla ya Alfajiri wakiomba maghfira (Adh-Dhaariyaat: 18).

Tujitahidini katika kuyafanyia kazi haya tunayoambizana. Na tuitumie fursa ya ramadhani kwa ajili ya kupata rehma za Allah (subhanahu wataala) na kusamehewa dhambi zetu. Allah atuwafikishe katika hayo. Aaamin.

RAMADHANI NA QUR-AN


                  Imeandaliwa na Raudhwah Islamic Group

             Sifa zote njema zinamstahikia Allah Subhaanahu Wataala Muumba mbingu na ardhi na vyote vilivyomo ndani yake, Sala na salamu zimuendee kipenzi cha umma bora Mtume Muhammad Swalla Allahu Alayhi Wa Sallam pamoja na Ahli zake na Swahaba zake na walio wema hadi siku ya malipo.

            Ndugu yangu katika Imani hatuna budi kumshukuru Allah Subhaanahu Wa Taala kwa kutujaalia kuwemo miongoni mwa waja wake aliowachagua kuudiriki mwezi huu mtukufu wa Ramadhani.

Tunamuomba Allah Subhaanahu wa Taala atuwezeshe kuzitekeleza Ibada zote kwa wingi na atujaalie kuwa miongoni mwa waja wake watakaofikia lengo la kufunga mwezi huu Mtukufu wa Ramadhani na siku ya malipo ikifika atujaalie kwa Rehma zake kuingia katika Pepo yake kwa daraja za juu bila ya hisabu.

            Ndugu yangu katika Imani, katika makala yetu tutajaribu kuzungumzia kuhusu kufungamana kwa Ramadhani na Qur-an.

             Ibada baada ya Sala na Zakka iliyofaradhishwa kwetu na Allah Subhaanahu wa Taala ni Funga ya Ramadhani. Ibada hii ya kufunga imefaradhishwa katika sheria za Mitume wote tangu mwanzo. Umma zote zilizopita zilikuwa zikifunga kama Umma huu wa Mtume Muhammad Swalla Allahu Alayhi wasallam unavyofanya.  Lakini kuhusu masharti ya kufunga na idadi ya siku za kufunga vilikuwa vikitafautiana kwa kila sheria ya kila umma. Historia hii fupi ya Funga imethibitishwa ndani ya Qur-an katika Suratul BAQARA  aya ya 183, pale Allah Subhaanahu wa Taala aliposema :- “Enyi mlioamini! Mumefaradhishiwa kufunga kama walivyofaradhishiwa waliopita kabla yenu ili mupate kuwa Wacha-Mungu.”

               Kutokana na aya hii inaonesha wazi kwamba katika kila sheria aliyoleta Allah Subhaanahu Wa Taala kwa kila Umma basi haikukosekana Ibada ya Funga.

             Ndani ya mwezi wa Ramadhan muislamu anatakiwa ajibidiishe katika kufanya yaliyo ya kheri kuanzia ya faradhi na yale ya sunna. Pia muislamu anatakiwa ajitahidi  aisome sana Quraan ndani ya mwezi wa Ramadhan. Na usomaji wenyewe uwe tofauti na usomaji mwengine. Uwe ni usomaji wenye mazingatio. Ili muislamu atumie chuo cha Ramdhani katika kuiweka sawa imani yake na kuzingatia ujumbe kutoka kwa mola wake. Ndani ya mwezi wa Ramadhani ndipo ilipoteremshwa Qur-an Tukufu kwa namna tofauti.

Amesema Allah Subhaanahu wa Taala katika Sura ya pili (2) (AL-BAQARA), Aya ya 185 :- “Mwezi wa Ramadhani ambao imeteremshwa Qur-an ili iwe uongofu kwa watu, na hoja zilizowazi za uongofu na upambanuzi (wa baina ya haki na batili)………”

                   Aya hii inatuthibitishia wazi kuwa Qur-an iliteremshwa katika mwezi wa Ramadhani, kwa hiyo inaonekana wazi kwamba mwezi huu wa Ramadhani haukuchaguliwa kuwa mwezi wa kufunga bure bure tuu bila ya sababu, isipokuwa mwezi huu umechaguliwa kwa sababu ndio mwezi ambao ndani yake iliteremshwa Qur-an kwa namna tofauti na nyakati tofauti. Na Quraan ndio nuru kwa umma.

QUR-AN
                    Qur-an Tukufu ni kitabu cha Allah Subhaanahu wa Taala kilichoteremshwa kwa Mtume Swalla Allahu Alayhi wa Sallam ili iwe uongofu kwa watu wote (viumbe vyote).

                  Qur-an ni kitabu kilichokusanya mambo yote ya maisha ya kidunia  na Akhera  ya mwanzo na ya mwisho, Pia ni kipambanuzi cha haki na batili. Pia ni yenye kuwaonya waumini na  kwa maana hizo tunaona wazi kwamba Allah Subhaanahu wa Taala ameiteremsha Qur-an ili tupate kujua namna ya kuishi maisha bora ya utii hapa duniani ili kupata Rehma za Allah Subhaanahu wa Taala katika maisha ya duniani na akhera.

Anasema Allah (subhanahu wataala) :
“Mwezi wa Ramadhani ambao imeteremshwa humo Qur'ani kuwa ni uwongofu kwa watu, na hoja zilizo wazi za uwongofu na upambanuzi.”(Baqara :185).
“……Hizi ni Aya za Kitabu na Qur'ani inayo bainisha.”(Hijri :1).

“Ametukuka aliye teremsha Furqani kwa mja wake, ili awe mwonyaji kwa walimwengu wote” (Furqaan :1).
                  Qur-an Tukufu ilikuwa imehifadhiwa katika Ubao unaoitwa “LAUHI-MAHFOODH”. Anasema Allah (subhanahu wataala) katika Suratul Buruj “Bali hii ni Qur'ani tukufu(21)Katika Ubao Ulio Hifadhiwa. (22)
Na baada ya hapo iliteremshwa hadi katika wingu wa kwanza wa dunia kwa ujumla wake, wakati huo ilikuwa katika mwezi wa Ramadhani. Na baadae ilianza kuteremshwa kwa Mtume Muhammad Swalla Allahu Alayhi wa Sallam kidogo kidogo, Mara ya kwanza kuanza kuteremshwa kwa Mtume Swalla Allahu Alayhi wa Sallam ilikuwa katika mwezi wa Ramadhani katika kumi la mwanzo, na aya za mwanzo kuteremshwa ni aya tano za mwanzo za Suratul-Alaq. Na ilikuwa ikiteremshwa na Malaika mtukufu JIBRIL Alayhi Salaam ambaye alikuwa akiwashukia Mitume wote kwa ajili ya kuwapelekea Wahyi kutoka kwa Mola wao.

                  Kutokana na Historia hiyo fupi tunaona wazi kwamba Qur-an imefungamana na mwezi wa Ramadhani kwa sababu ndio mwezi ulioteremshwa Qur-an kwa namna tofauti na nyakati Tofauti.

                       Ndugu yangu katika Imani, hakika ya Funga pamoja na kusoma Qur-an ni Ibada zilizokuwa kubwa zaidi na zenye malipo makubwa. Lakini kuisoma Qur-an kusiwe juu juu tuu na sauti zilizokuwa nzuri zenye kuvutia. Isipokuwa kuisoma Qur-an kunatakiwa umakini mkubwa pamoja na kuizingatia vizuri tafsiri yake na kuifanyia kazi katika maisha. Allah (subhanahu wataala) anasema “Je! Hawaizingatii hii Qur'ani? Au kwenye nyoyo (zao) zipo kufuli?”( Suratu Muhammad :24). Hivyo basi na sisi tuisome Quraan kwa mazingatio makubwa kwa sababu kwenye Qur-an ndipo tunapopata kila kitu juu ya maisha tunayotakiwa tuishi. Kwa hivyo tunapofunga katika mwezi huu wa Ramadhani tujitahidi kwa kadiri ya uwezo wetu wote kuisoma Qur-an kwa wingi na kwa mazingatio pamoja kuifanyia kazi mafundisho yake ili tupate kuongoka. Tunapofanya hivyo ndipo tunapofikia yale malengo ya kufunga mwezi wa Ramadhani nayo ni kufikia daraja za Ucha-Mungu.

Fadhila za kusoma Quraan hatutozielezea kwani tayari tumezieleza katika darsa zetu nyengine.

                     Tumuombe Allah Subhaanahu wa Taala atuwafikishe kuifunga Funga hii ya Ramadhani na atuwezeshe kuisoma Qur-an kwa mazingatio na atujaalie kuwa miongoni mwa waja wake watakaofikia daraja ya Ucha-Mungu, na Siku ya malipo ikifika atuingize Peponi kwa Rehma zake. Aaamin.

Friday 4 July 2014

REHMA ZA ALLAH (SUBHANAHU WATA‘ALA) KWA WAJA WAKE


Makala imeandaliwa na Raudhwah Islamic Group

Kila sifa njema zinamstahikia Allah Mola wa viumbe vyote. Sala na salamu zimuendee Mtume wetu Muhammad (swalla Allahu alaihi wa sallam) na ahli zake na maswahaba wake.

Ndugu zangu wa kiislamu Mtume (swalla Allahu alayhi wasalam) anatuambia kuwa Ramadhan imegawika katika makumi matatu. Kumi la kwanza ni REHMA, la pili ni MAGHFIRA na la tatu ni KUACHWA HURU NA MOTO. Kwa hakika sasa hivi tuko katika kumi la Rehma. Rehma za Allah kwa waja wake ni nyingi na hatuwezi kuzielezea au kuzizungumza na tukaweza kuzimaliza. Hivyo basi tutazungumza kwa uchache kuhusu Rehma za Allah kwa waje. Muislamu atakapoyafahamu vizuri haya ndipo atakapojua umuhimu wa yeye daima kuomba Rehma za Allah (subhanahu wata‘ala).

Awali kabisa katika mada hii napenda nielezee maneno haya mawili nayo ni ARRAHMAAN NA ARRAHYM. Maana ya maneno haya ni kuwa Allah ni mwingi wa Rehma na mwenye kurehemu. Maneno haya ni majina miongoni mwa majina ya ALLAH kwani ALLAH (subhanahu wata‘ala) ana majina mengi. Na kwa kuangalia maana ya majina haya kwa haraka kabisa utaona kuwa yana maana moja kwa sababu yanatokana na neno Rehma (huruma). Ila maana zake kiundani ni kuwa, ARRAHMAAN maana yake ni rehma za ALLAH kwa waja wake wote hapa ulimwenguni. Kila kiumbe chake Allah basi anapata rehma kutoka kwa muumba wake. Anasema Allah (subhanahu wata‘ala): “Na rehema yangu imeenea kila kitu.” (7:156). Na neno ARRAHYM hizi ni rehma maalum kwa waja wake walioamini pekee katika siku ya malipo pale Allah aliposema katika suratul Ahzaab mwisho wa aya ya 43: “Naye ni Mwenye kuwarehemu Waumini.”

Rehma za Allah (subhanahu wata‘ala) kwa waje wake ni nyingi mno. Na huruma za Allah kwa viumbe vyake ni kubwa sana. Hebu tuangalie kwa uchache baadhi ya mifano ya rehma za Allah (subhanahu wata‘ala) kwetu.

Hebu angalia rehma za Allah (subhanahu wata‘ala) kwa mtoto mchanga ndani ya tumbo la mama yake. Mbali ya kuwa mtoto yumo ndani ya tumbo na hana anaemuona wala kumshughulikia, Allah (subhanahu wata‘ala) anajaalia mtoto yule anakuwa vizuri na anapata rizki zake akiwa yumo mule mule ndani ya tumbo la mama yake.

Mtoto amezaliwa tayari wako baadhi yao wamezaliwa wakiwa na upungufu wa viungo na wengine wakiwa na viungo kamili. Wote hawa kuzaliwa na hali yoyote ile basi huwa ni rehma kwao. Leo binaadamu hajakaa kumuomba Allah (subhanahu wata‘ala) ampe macho, masikio, miguu wala akili ila Allah (subhanahu wata‘ala) amemjaalia kiumbe yule amezaliwa akiwa na viungo vyote hivyo na hajaviomba. Jee hatuoni kuwa hii ni rehma katika rehma zake Allah (subhanahu wata‘ala) kwetu?

Wengine wamezaliwa hawaoni, hawasikii au hawatembei vipi tutasema kwao wao ni rehma? Ndio ni rehma kwani tayari wameshapewa takhfif ya mtihani huko akhera. Mtihani ambao kila aliyepewa neema hizo lazima akazielezee vipi amezitumia. Mwenye macho ataulizwa vipi ameyatumia macho yake, jee ameyatumia katika halali au haramu? Ila yule aliyekosa macho basi hatokuwa na mtihani huo kwani jicho lake halikuwahi kudiriki kuona. Hivyo tuwe waangalifu na ambayo tunayafanya.

Rehma nyengine ya Allah kwetu sisi ni kuwa tumezaliwa katika neema kubwa ya Uislamu. Si kwa ubabe wetu wala uhodari wetu bali ni kwa rehma zake Allah (subhanahu wata‘ala) kwetu sisi. Kwani wako wengine wanazaliwa hali ya kuwa si Waislamu. Suala litakuja je hawa wamekosa rehma za Allah? Hapana hawakukosa rehma za Allah. Zipo rehma za Allah kwake na ndio maana akampa akili na baadae kumpelekea mjumbe wa kumlingania katika haki. Allah (subhanahu wata‘ala) hataki hata mja wake mmoja afe hali ya kuwa anamuasi. Ila sisi wenyewe ndio tunaojiingiza katika maangamizo.

Pia ni katika Rehma za Allah kwetu sisi kutujaalia tumezaliwa tukiwa tumo katika Umma bora, umma wenye kitabu bora pamoja na kuletewa Mtume bora. Je hatujui sisi kuwa katika wakati huu pekee ni rehma za Allah (subhanahu wata‘ala) kwetu sisi. Nabii Mussa alayhi salaam alitamani awe mfuasi tu ndani ya Ummat Muhammad. Jee mimi na wewe tunathamini hilo? Jee tunajua kuwa ni rehma zake Allah (subhanahu wata‘ala) kutujaalia sisi kuwa katika Umma huu?

Ndugu zangu wa kiislamu rehma za Allah kwetu sisi ni kubwa mno. Hatuwezi kumaliza mifano kwa kuiandika wala kuzungumza.

Tutosheke na mifano hiyo michache ambayo iwe ni mazingatio kwetu sisi.

KIMBILIA KATIKA KUZIPATA REHMA ZA ALLAH NA USIKATE TAMAA KUTOKANA NA REHMA ZAKE

Mifano tuloitaja juu ni mifano ya rehma za Allah (subhanahu wata‘ala) kwetu sisi. Mifano ambayo hatukukaa kuiomba bali mwenyewe Allah ametujaalia. Muislamu hatakiwi kukaa tu akasema rehma za Allah zipo tu kwangu na zitakuja. Lazima Muislamu wa kweli ajibidiishe katika kuzitafuta rehma za Allah. Hakika kila mmoja wetu ni muhitaji wa rehma za Allah (subhanahu wata‘ala) kwa kila jambo. Hakuna mtu anaeweza kusema kuwa ametosheka na rehma za Allah.

Jee Muislamu ili azipate rehma za Allah afanye nini? Jambo la kwanza Muislamu anatakiwa awe ni mwingi wa kufanya mazuri na kujiepusha na haramu. Kufanya hivyo kutamfanya aweze kupata rehma za Allah kwa ushahidi wa Quraan: “Hakika rehma za Allah zipo karibu kwa wenye kufanya mazuri(muhsinin).” (7:57).
Aya hapo juu inaonyesha wazi kabisa rehma za Allah ziko na wenye kufanya mazuri. Hivyo Muislamu azitafute rehma za Allah kwa kukimbilia kufanya mazuri na kujiepusha na kufanya madhambi.
Jambo la pili ni kwa Muislamu kuzidisha dua kumuomba Allah (subhanahu wata‘ala) aweze kumpa rehma zake. Msingi wa ibada ni dua. Wakati watu wanakimbilia kuomba majumba, fedha na utajiri ndugu yangu Muislamu wewe kimbilia katika kuomba rehma za Allah (subhanahu wata‘ala).

Latatu Muislamu akithirishe katika kumtaka msamaha Allah (subhanahu wata‘ala) kwa wingi itamfanya aweze kupata rehma za Allah. Ukiangalia katika Quraan sehemu nyingi ambazo Allah anataja kuhusu msamaha au yeye Allah ni mwingi wa kusamehe basi hutaja mbele yake neno RAHIIM. Hii ni kuonyesha wazi kwetu sisi tunapotaka rehma za Allah basi tukimbilie katika kuomba msamaha wa kweli kwa Allah ili tuzipate rehma zake.

Mfano wa aya hizo ni:
1. “Waambie waja wangu ya kwamba Mimi ndiye Mwenye kusamehe, Mwenye kurehemu.” (15:49).
2. “Na ALLAH ni Mwenye kusamehe na Mwenye kurehemu.” (2:218).
3. “ Ni vyeo hivyo vinavyo toka kwake, na maghfira na rehema. Na Mwenyezi Mungu ni Mwingi wa maghfira na Mwenye kurehemu.” (4:96).

Lamuhimu kuambizana ni kuwa tuombe msamaha wa kweli kwa Allah basi atatusamehe kwa rehma zake na tutazipata rehma za mambo mengine. Miongoni mwa rehma anazozipata mwenye kuomba msamaha ni kule kujaaliwa dhambi zake kuwa ni thawabu. “Isipo kuwa atakaye tubu, na akaamini, na akatenda vitendo vyema. Basi hao Mwenyezi Mungu atayabadilisha maovu yao yawe mema. Na Mwenyezi Mungu ni Mwenye kusamehe, Mwenye kurehemu.” (25:70). Lakini haya hayapatikani isipokuwa mtu kuomba msamaha wa kweli kwa Allah (subhanahu wata‘ala).

Mwisho kabisa natoa nasaha kwa Waislamu wote kuwa mtu asikate tamaa na rehma za Allah (subhanahu wata‘ala). Kadri utakavyokuwa umemuasi Allah basi utakapoamua kurudi kwake kikweli basi Allah atakupokea na atakusamehe dhambi zako. Muhimu ni mtu kuamua kurudi kikweli kwa Allah (subhanahu wata‘ala). Pia hata yule asiyekuwa Muislamu basi atasamehewa dhambi zake na kuwa kama mtoto mchanga pale anapozaliwa wakati atakapoingia katika Uislamu.

Na angalia rehma za Allah kwa waje wake. Mja juu ya kumuasi Allah bado Allah anamwita mja huyo kwa jina la Mja ( abdu). Mwanadamu akikerwa kidogo tu basi yule aliyemkera humwita kila aina ya majina kuonyesha hasira zake. Ila Allah (subhanahu wata‘ala) juu ya mja kumuasi bado humuita kwa jina la abdu. Na anamwambia arudi kwake na asikate tamaa. Vipi rehma za Allah zilivyokubwa kwetu sisi. Allah (subhanahu wata‘ala) anasema: “Sema: Enyi waja wangu walio jidhulumu nafsi zao! Msikate tamaa na rehema ya Mwenyezi Mungu. Hakika Mwenyezi Mungu husamehe dhambi zote. Hakika Yeye ni Mwenye kusamehe, Mwenye kurehemu.” (39:53).

Tusikate tamaa na rehma za Allah (subhanahu wata‘ala) na tujitahidini kuzitafuta rehma zake kwa kuyafanya yale aliyotuamrisha. Allah atuwafikishe. Aaamin.

Wednesday 2 July 2014

TUNAKUOMBA UDHURU RAMADHAN


Makala imeandaliwa na Raudhwah Islamic Group

Ni wajibu wetu kuiomba msamaha Ramadhan na ni haki yake kutusamehe au kututosamehe,kukubali udhuru wetu au kuukataa udhuru wetu.

Kwanini tuiombe msamaha Ramadhan? Ni kwasababu ilipokuja mwaka jana, tuliazimia kufanya mengi, na baada ya kutushinda kuyatekeleza, tukaazimia kuyafanya tena mwaka huu, na kujiapiza kua tutayatekeleza kwa hali yoyote ile. Lakini ndio hiyo inaendelea kwenda kumalizika bila ya kutekeleza hata nusu ya tuliyoyaazimia.

Tunarejea makosa yaleyale tuloyayafanya Ramadhan zilopita. Tunarejea kukosa sala za jamaa, na kutosheka mtu kusali ndani ya wakati tu,tunarejea kosa la kuzungumza maneno maovu, na kusahau kua tunatakiwa tusifunge matumbo yetu tu, bali hata midomo yetu na viungo vyenginevyo. Tunarejea tena kosa la kutosoma Qur-an, na anaesoma hazingatii maana yake.

Je tunajua kwanini tunashindwa kuyatekeleza hayo yote na kutoipa Ramadhan haki yake? Ni kwasababu moja tu; na si nyengineo nayo ni kua TUNATAKA KUFANYA MAMBO AMBAYO HATUKUZOEA KUYAFANYA KABLA YA RAMADHAN. Hatukuzoea kusimama usiku kusali alau rakaa moja ya witri. Hatukuzoea kusoma Qur-an alau juzuu moja kwa siku, na tukakhitimisha baada ya mwezi,hatukuzoea kukaa miskitini katika vikao vya kheri na kusikiliza darsa,na hatukuzoea kusali sala za sunnah, hivyo tunashindwa kudumu na tarawehe. Hatukuzoea kua na khushui ndani ya swala hivyo hata anaeswali tarawehe na sala za usiku haathiriki na kinachosomwa kwani akili haipo, na ipo kwenye mechi ya leo nani atakua mshindi. Hatukuyazoea yote hayo na ndio yanatushinda kuyafanya, na anaefanya hushindwa kudumu nayo.

Tunahitaji kuiomba radhi Ramadhan kwa sababu kwa wengi imekuja wakati sio, kwani tumeghafilika na kutizama kandanda, na kupanga mechi, hivyo hatuhitaji kushughulishwa na jengine. Na hivyo ndivyo itakavyokua hali mpaka kinapomjia mtu kiama chake kidogo, (kutokwa na roho) au kikubwa atakua ameghafilika. Amesema Allah subhanah katika Suratul-Anbiyaa aya ya 1-3 “IMEWAKARIBIA WATU HESABU YAO, NA WAO WAMEGHAFILIKA NA KUPUUZA.HAYAWAJII MAWAIDHA MAPYA KUTOKA KWA MOLA WAO, ILA HUYASIKILIZA HALI YAKUA WANACHEZA. ZIMEGHAFILIKA NYOYO ZAO………..”. Hivyo Ramadhan una haki kutusamehe au kutotusamehe, lakini udhuru wetu ndio huo.

Amesema Mtume rehma na amani ziwe juu yake kuwabashiria maswahaba zake ilipoingia Ramadhan:“Umekujieni mwezi wa Ramadhan,mwezi wenye Baraka. Mumefaradhishiwa ndani yake Funga.Milango ya pepo hufunguliwa, na kufungwa ya moto. Ndani yake kuna usiku bora kuliko miezi elfu,atakaeharamishiwa kheri za usiku huo basi uyo ameharamishiwa. (kikweli kweli ameharamishiwa kheri zote)” (Nasai).

Jee sisi tunabashiriana kwa lipi? Au tunabashiriana kwa ushindi wa timu zetu? Amesema Mtume wa Allah katika hadith inayosimuliwa na Jaabir “Pua lake lirambe mchanga, (amepata hasara), anaeidiriki Ramadhan, kisha asisamehewe dhambi zake” . Lakini Jee kusamehwa dhambi ni kwa kila mtu atakaefunga?. Laa hasha wa kalla. Yule atakaefunga kwa Imani na kutarajia malipo, akajiepusha na mambo ya kipuuzi na kusema maneno yasiyokua ya kheri, huyo ndio iliyokamilika funga yake, kwani ameyafunga na kuyazuia matamanio ya tumbo lake,utupu wake, ulimi wake na viungo vyenginevyo.

Hivyo ndivyo walivyokua waja wema waliotangulia kuanzia maswahaba matabiina na wengineo,kwao wao mwaka mzima ulikua Ramadhan. Walijiandaa kuipokea Ramadhan, na wakimuomba Allah miezi sita awafikishe Ramadhan, na miezi sita baadae kuomba wakubaliwe waloyoyatenda Ramadhan.Walijua thamani ya funga itoshe hadithi ya Rasuul kua “Atakaefunga siku moja katika njia ya Allah, ataepushwa na moto mwendo wa miaka sabini”(Muttafaqun alayhi).

Walidumu na funga si za Ramadhan tu, bali na za Sunnah. Ramadhan waliipa haki yake, na ndipo wakaweza kufunga na za Sunnah. Sayyidina Uthmaan radhia Allahu anhu ameuwawa hali ya kua amefunga, na alikua akisoma Qur-an, ni kweli mtu hufa kwa amali aloizoea kuifanya.

Inasimuliwa kua Ibnu Umar yeye na baba yake radhia Allahu anhuma walikua hawafungi wanapokua safarini, na walikua hawali wanapokua nyumbani ,zaidi ya siku zilizoharamishwa kufunga. Lakini jee sisi tunaweza hayo au ndio tunatamani Ramadhan iishe ili jukumu la kufunga lituishie? Wengine kufikia kusingizia maradhi ya vidonda vya tumbo, ili tusifunge. Tumesahau kua aliefaradhisha Funga, ni mwenye kusikia na mwenye kuona, na anajua kila kitu,hakifichiki kwake kitu kama anavosema “…Na anajua yaliyomo barani na baharini,na halianguki jani ila anajua,wala punje katika giza la ardhi(ila anajua)…” (An-am :59).

Wengine wakafikia kuhama miji yao, na kwenda miji ya makafiri kwa kukimbia funga.Kwa kweli tunahitaji kuiomba radhi si ramadhan pekee bali na aloileta Ramadhan.

Allah ameeleza Lengo la kutufaradhishia funga, na si jengine zaidi ya kutaka tuwe wacha-mungu, kwa maana nyengine tumuogope yeye subhaanah,lakini je tumelifikia lengo hilo? Ramadhan ngapi zishapita na bado hatujalifikia lengo hilo. Kiukweli tunahitaji kuiomba msamaha Ramadhan.

Ramadhan ni mwezi ulioteremshwa Qur-an, na fadhila za kusoma Qur-an tumeona katika makala mbali mbali na kuzungumizwa na masheikh wengi, lakini Je tumezingatia fadhila hizo au ndio tuko na mashughuli ya kidunia na kusahau Akhera?. Kiasi Mtume wa Allah atushtaki pale aliposema “Na akasema Mtume:Ewe Mola wangu,hakika watu wangu wameihama Qur-an” (Fur-qaan 30). Na sisi hatufai kutushtakiwa kwa kuihama Qur-an tu, bali tunahitaji kushtakiwa kwa kutoipa hadhi yake stahiki Ramadhan.
Ramadhan ni mwezi wa maghfira,na toba na kuwachwa huru na moto. Lakini je tumayakimbilia haya?
Ramadhan ni mwezi wa subra na sadaka, na kuhurumiana baina ya watu na kuunganisha koo Lakini jee tunayafanya haya?

Ramadhan ni mwezi kushkuru na kuomba dua, na ndio mwezi wa ushindi,kwa waislamu kama tutakavyoona katika mada ya “Matukio muhimu ndani ya Ramadhan,”basi kwa nini wasifurahi waumini kwa hili na wanafurahia mengine?

Ramadhan ni mwezi wa adhkaar,itikafu,qiyamul-layl,tarawehe na kuengezewa mema na kufutiwa madhambi. Tunayafanya haya? au ndio tumeigeuza kuwa ndio mwezi wa kula na kunywa na kuchezacheza. Amesema Allah kumwambia Mtume wake “Waachie wale, na wacheze na yawapoteze matamanio na karibuni watajua”(Hijri 3). Tumeilizangatia onyo hili? Kwani ndo hali yetu wengi,tunakula,tunakunywa na kuchezacheza.

Maswahaba waliyafahamu haya, na ndio wakaipa Ramadhan thamani stahiki. Waliufahamu wasia wa Mjumbe wa Allah, na kama alivyosema swahaba wake mtukufu Abu-Dardai radhia Allahu anhu nilikua mfanya biashara mashuhuri, niliekua na mafanikio katika biashara zangu alipotumwa Muhammad, nikaona biashara na ibada haviendani, (kutokana na mishughuliko ya kibiashara) nikaamua kuchagua ibada na kuacha biashara. Amesema kweli Allah pale alipowasifu watu kama hawa na mfano wake: “Wanaume ambao haiwashughulishi biashara wala mauzo,(kuwasahaulisha) kutokana na kumkumbuka Allah,na kusimamisha sala,na kutoa Zakka,na wanaiogopa siku zitakapobadilika nyoyo na macho (Qiyamah)”( Nuur 37) .
Hii ndo ilikua hali yao, basi ni ipi hali yetu ? Jee sisi tumechagua nini; Ramadhan au Mashughuliko ya kidunia? Tusameh Ramadhani

Tuesday 1 July 2014

KOMBE LA DUNIA (WORLD CUP) NA RAMADHAN

Makala imeandaliwa na Raudhwah Islamic Group 

“IMEWAKARIBIA WATU HESABU YAO, NA WAO WAMEGHAFILIKA NA KUPUUZA.

HAYAWAJII MAWAIDHA MAPYA KUTOKA KWA MOLA WAO, ILA HUYASIKILIZA HALI YAKUA WANACHEZA. ZIMEGHAFILIKA NYOYO ZAO………..” (AL-ANBIYAA 1-3)

Ni suali wanalojiuliza walimwengu wote, kuhusu nani atakaekua bingwa wa soka mwaka huu? Ni kike kwa kiume, wakubwa na wadogo, WAISLAMU na wasiokua waislamu,hukusanyika chini ya vioo vya televishen ifikapo usiku, na kupoteza dakika 90 au zaidi, kuangalia michuano ya soka la kombe la dunia.
Tumejisahau kama tuko ndani ya mwezi mtukufu wa Ramadhan. Tumesahau kua wakati huo wa usiku, Allah hushuka katika wingu wa dunia, na kuuliza nani anaeniomba nimjibu? Nani anaeniuliza nimpe? Na nani anaenitaka msamaha nimsamehe,?(Imesimuliwa na Abu-Hurayra na kupokewa na Muslim na Tirmidhy).

Je sisi tuko katika kundi gani, tunalomuomba ili atupe au kumtaka msamaha atusamehe? Ni kweli imekaribia hesabu ya watu, lakini wenye kuhesabiwa WAMEGHAFILIKA juu ya hilo. Hivi hatuoni kua ni kumfanyia istihzai Allah (subhanahu wataala), kua anashuka kwa ajili yetu na sisi tumeshughulika tukishangiria kandanda? Mara moja alipita Hassanulbasry rahimahullah ,akamkuta mtu anacheka kupindukia, akamuuliza: Je umeweza kuvuka katika Swiraat? Akamjibu: Laa, akamuuliza Je umevuka kutokana na Jahannam? Akamjib: Laa, akamuliza basi hicho kicheko ni cha nini?. Basi nasi tujiulize hivi vicheko vya nini? Au jibu ni kua timu yangu imeshinda?

Tunajiuliza kuhusu nani atashinda mechi ya leo, na nani atanyakua ubingwa, huku tukisahau kujiuliza nini tufanye ili tuifaidi Ramadhan? Je tukifa wakati huu, tunacho cha kumjibu Allah (subhanahu wataala? Tumejiandaa vipi kwa mauti na sakarati yake,kaburi na giza lake,ufufuo na zahma zake,hesabu na undani wake,na mwishowe Jahannam na joto lake?

Mara moja alipita Sayyidina Aliy kwenye kaburi akaliuliza: Je nikupe habari za duniani, ili na mimi unipe za uko ulipo? Akamwambia ama za duniani: Wake zenu wameshaolewa,majumba yashakaliwa na mali zenu zishagaiwa, na kama ungeliweza kunambia habari za uko ulipo, nadhani ungenambia kua :“Chukueni masurufu, kwani safari ya Akhera ni ndefu.”

Amesema Mtume swalla Allahu alayhi wasallam katika hadithi inayosimuliwa na Abi-Ya’ala: “Mwenye akili ni yule anaejipima nafsi yake, na akafanya yatakayomsaidia baada ya mauti.Na mjinga ni yule anaendekeza matamanio ya nafsi yake, na akatarajia mazuri kutoka kwa Mola wake” (Tirmidhy). Je sisi tuko katika kundi gani? La Wenye akili ama wajinga kutokana na hadithi hii.

Si kama haijulikani kama mwezi huu ni mwezi wa ibada, lakini makafiri hawatoacha kufanya kila aina ya hila, ili waislamu waghafilike, na kwa hilo wamefanikiwa. Amesema ALLAH subhanah“Na hawatoacha kukupigeni vita (makafiri),mpaka wakurejesheni kwenye dini yao ikiwa wataweza”.(Baqarah :217). Umma wa kiislamu umekua ukijua habari za ulimwengu wa mipira, kuliko habari zinazoendelea katika ulimwengu wa sasa wa kiislamu, seuze habari za wema walotangulia, ambapo habari zao wameachiwa wenyewe.

umesahau kua, waislamu wenzetu wanafunga lakini hawajui watakula nini. Na wengine wanafunga, huku wakiwa hawana uhakika kama wataimalizia funga ile palepale nyumbani au hospitalini, baada ya kujeruhiwa na risasi au wataimalizia kaburini. Hii ndio hali ya waislamu nchini Syria, Palestina, Iraq, Myenmaar (Burma), Kashmiir, Afganistan, Chechenia, Somalia,Afrika ya kati na kwengineko. Lakini tuliobaki tumejishau kua tuko katika neema, na ndio tunaitumia neema hiyo, ya uhai ,uzima na amani katika michuano ya kombe la dunia. Amesema Mtume wa Allah (swalla Allahu alayhi wasallam)“Asiejali mambo ya waislamu basi si katika sisi.”

Yamehifadhiwa majina ya wachezaji ,mwaka alozaliwa, mwaka alojiunga na klabu, pesa ilonunuliwa mkataba wake, mwaka gani atastaafu, anachezea mguu gani ,anapenda nini na hata nani atakaemuoa.Imesahauliwa historia ya Rasuul na nasaba yake,na yule alokua anadai kua anajitahid katika mambo ya dini, basi atamjua mpaka babu yake Abdul-Muttalib. Masahaba 10 walobashiriwa pepo hawajulikani. Majina ya Wake za Mtume na baba zao hayajulikani. Vita vya badri havijulikani vimepiganwa mwaka gani,na idadi ya waislamu walopigana,wala idadi ya mashahidi, Lakini ratiba za mechi na saa zilochezwa fainali zote, tokea mtu apate akili zake anazijua.

Tumeanza kuwapenda wachezaji, mpaka kusahau imani zetu kua sisi ni waislamu na wao ni makafiri, na hatuna uhusiano nao. Tumesahau kua sahaba alimuua baba yake katika vita vya Badri, kwa sababu anaipinga dini ya Allah, na Allah akateremsha aya kumsifia kwa kitendo hicho cha ki-imani na kishujaa, lakini sisi ndio kwanza tunawakumbatia na kujinasibisha nao. Amesema Allah subhanah“Hutowakuta watu wanaomuamini Allah na siku ya mwisho, wakawa wanawapenda wale wanaompinga Allah na Mtume wake, hata wakiwa baba zao, au watoto wao, au ndugu zao, au jamaa zao.” (Mujadalah: 22).

Akasema tena katika suratu-Tawbah 23: “Enyi mloamini,msiwafanye baba zenu na ndugu zenu,kua ni vipenzi vyenu,ikiwa watapenda kufru badala ya Imani” Ikiwa hali ndo hiyo ata kwa jamaa wa karibu, madamu kafiri basi hutakiwi kumpenda, seuze wachezaji mipira ambao hata hajui kama kuna watu wanalia anapouumizwa.

Tumeanza kuwapenda na baadae tukawaiga mikato yao, mienendo yao,na hatimae hadi majina yetu tukaengeza viambishi ili kufanana na yao. Mchezaji kamaliziwa na “vin” basi na mimi jina langu litakua ni “Saidivin”. Tumesahau kua jina la Said lina maana ya kua ni mtu mwema, sasa sijui kua likiengezewa na “vin” litaleta maana gani. Tumesahau kua Said ni jina la sahaba alobashiriwa pepo na mtu analikataa, na badala yake anaeka jina la kafiri. Na mfano wa majina kama hayo yapo mengi. Amesema Allah subhanah“Hawatoridhika mayahudi wala manasara mpaka uwafate mila zao” (Baqarah 120), na ndo izo tunazifuata na kuziiga.

Tumekatazwa kufanya urafiki na makafiri na kuwakumbatia ikawa ndio vipenzi vyetu. Amesema Allah(subhanahu wataala) “Enyi mloamini msiwafanye mayahudi na manasara, kua ni vipenzi vyenu.” (Maidah :51). Je tumeizingatia aya hii au ndio tunalia kwa kifo cha kafiri, na kusahau kua yeye alimkana Mola ambae wewe unadai kua ni Mola wako? Amesema Mtume wa Allah (swalla Allahu alayhi wasallam) katika hadithi iliyopokelewa na Ibnu-Hibbaan na kusimuliwa na Ibnu-Umar,“Atakaejifananiza na kaumu basi nae ni miongoni mwao” Tunawapenda watu ambao Allah amewalaani.

Wangapi kati ya wachezaji huvaa herini? Jee hayo si katika mapambo ya wanawake? Tumesahau kua wanaojifananisha na wanawake Allah amewalaani? Wangapi katika wachezaji hukata mikato ya ki fir-aun? Bado tu tunaendelea kuwapenda,? na hao ambao watasemwa kua ni waislamu, basi matendo yao hayatofautiani na makafiri kwani hutia herini kama wanavyotia wachezaji wenzake,hufanya mengineo kama wanavyofanya wenzake. Basi ni lipi la kuwatofautisha?

Tunasahau kua wanawafanya waungu watatu kua ndo wanaondesha ulimwengu huu kama familia,kuna baba, mwana na roho mtakatifu.Imekuja sura nzima kuwazungumzia mayahudi na manasara kua wamekufuru, na sisi waislamu hatutakiwi kua na mapenzi nao, badala yake tuwe na juhudi ya kuwalingania, na sio kufurahia matendo yao na kuyaiga. Amesema Allah (subhanahu wataala) katika Suratul-Maidah aya ya 73“Hakika wamekufuru wale wailosema Allah ndie Masih Issa bin Maryam, na akasema katika aya inayofata “. Hakika wamekufuru wale walosema kua Allah ni mmoja kati ya waungu watatu. Hakuna Mola wa haki zaidi ya Allah” Basi ni nani hao zaidi ya hao hao makafiri tunaowashabikia, na kufikia kujiua pindi timu zao zinapofungwa?

Kwa kua ndio ilikua desturi yetu kabla ya ramadhan kuwacha yalo muhimu, na kupoteza dakika 90 chini ya kioo, basi shetani ameendelea kututeka akili zetu mpaka ndani ya Ramadhan, tunaendeleza yale yale badala ya kurudi kwa Mola wetu, na kumlilia atusamehe madhambi yetu.

Swala zimekosa Khushui kwani kila unaposali mtu hukumbuka mechi ya jana, na ya leo sijui itakuaje. Kazi ya ukocha hufanywa ndani ya swala, na kupangwa namba za wachezaji ndani yake, na kama si takbira za imamu basi maamuma hatojua ameswali rakaa ngapi. Amesema Mtume wa Allah (swalla Allahu alayhi wasallam) katika hadith inayosimuliwa na Ibni Abbaas radhia Allahu anhuma “ Faidika na mambo matano kabla ya matano: Uhai wako kabla ya kifo, Uzima wako kabla ya maradhi yako, Ujana wako kabla ya uzee wako, Faragha yako kabla ya mashughuliko yako,na utajiri wako kabla ya ufakiri wako.” [Al-Haakim].

Je sisi kwa muda wa dakika 90, tunafaidika na kipi kabla ya kipi? Amesema Allah subhanah“Waachie wale, na wastarehe na yawadanganye matarajio,karibuni ivi watajua” ( Suratul Hijri :3). Tusisahau kua Qur-an imeteremshwa ndani ya mwezi huu, na Mtume (swalla Allahu alayhi wasallam) alimshtakia Mola wake kua umma wake umeihama Qur-an. Wakati wa mchana kila mtu yuko mbioni kutafuta dunia yake, na usiku hufungwa kazi zote na watu hujiandaaa vizuri si kwa jengine, zaidi ya kuangalia kandandanda dakika 90. Je tungesoma Qur-an ingekua tushafika juzuu ya ngapi? Tukumbuke kua pamoja na kua milango ya pepo iko wazi,na ya moto kufungwa ndani ya Ramadhani, si kwamba atakaekufa na mwisho mbaya hatoingia motoni. Laa hasha wakalla. Badala yake atakaekufa akishuhudia upuuzi basi atafufuliwa hali yakua anashuhudia upuuzi, kutokana na hadithi ya Mtume wa Allah“Atafufuliwa mtu kutokana na kile alichofia.”(Muslim).
Na akasema katika hadithi nyengine “Watafufuliwa watu na wale wanaowapenda” (Ahmad).Basi na sisi nani tunaowapenda kina Abubakar na Umar ama wachezaji mipira na waimbaji.

"ALLAH TUJAALIE WALE WENYE KUAMBIWA MAZURI NA KUYAFANYIA KAZI NA KUKATAZWA MABAYA NA KUYAWACHA"Aaamin.