Sunday 29 June 2014

FAIDA ZA MWENYE KUFUNGA HAPA DUNIANI


Makala imeandaliwa na Raudhwah Islamic Group

Kila sifa njema zinamstahikia Allah Mola wa viumbe vyote. Sala na salamu zimuendee Mtume wetu Muhammad (swalla Allahu alaihi wa sallam) na ahli zake na maswahaba wake.

Allah Subhaanahuu Wataala ametufaradhishiya funga sisi tulioamini, ili tupate uchamungu pamoja na faida mbali mbali zinazopatikana katika funga. Na tujue funga hii ni ile iliyofungwa kwa kujua na kutambua sharti, sunna na yale yanayobatilisha funga kwa mfungaji, ndipo tutakapopata uchamungu na   faida nyingi.
Hivo basi Kwa mwenye kufunga anapata faida za kiroho, za kijamii na katika siha yake. Kama zifuatazo:
Miongoni mwa faida za kiroho ni kule kuwa na subra na kuijenga khasa katika nafsi yake, na anajifunza kuifunga nafsi na kuisaidia kuwa katika hali hiyo.

Na atailea nafsi katika Taqwa na uchamungu, kwani uchamungu ndio lengo kubwa la funga. Allah anasema: “Hakika mumuefaradhishiwa funga kama walivofaradhishiwa walio kabla yenu ili muwe wachamungu” 2:183
Faida nyengine kwa mwenye kufunga ni kukubaliwa dua yake.

Hadithi aliyoipokea Imam Al Tirmidhy Radhi za Allah ziwe juu yake amesema : “Watu watatu hukubaliwa dua zao; aliyefunga mpaka aftari, kiongozi muadilifu na aliyedhulumiwa”
Pia akasema tena Mtume Swalla Allahu alayhi wassalam “Dua ya aliyefunga hupokelewa pale anapoftari” (Imepokelewa na Ibnu Maajah).

Angalia kwa namna gani faida na fadhila tunazopata pale tunafunga hapa hapa duniani.
Ama faida za kijamii kwa mwenye kufunga ni:
Kuurejesha umma au jamii katika nidhamu na umoja, na kupenda uadilifu na usawa.
Na kuengeza na kuzidisha kwa waumini upole na huruma, na tabia ya kuwa na ihsani, pale jamii inapojifunga na kuzuiya kufanya mambo ya shari na ufisadi wakati wote wa funga.

Na katika faida nyengine ya funga ni:
Faida ya kisiha na kupata afya kwa mwenye kufunga, kwani anasafisha mfumo wake wa chakula na kupumzisha tumbo, kuusafisha mwili kutokana na vidudu na minyoo inayoleta maradhi. Maana vidudu hivi hupata nguvu na pale mwanadamu anapokuwa anakula (parasites).

Na kupunguza kiwango kikubwa cha mafuta na uzito katika tumbo, kwa maana kisayansi mwili wa mwanaadamu unatakiwa usipungue kiwango cha glucose au sukari katika damu, kiwango hichi huwa sawa pale mwanadamu anapokula chakula, hivo mda anaofunga chakula na kiwango cha sukari hupungua mwilini ila mwili unajaribu kuangalia sehemu ama chakula kilichohifadhiwa na kukivunja na kukitumia ili mwili uwe sawa na kuwa na nguvu. Ndipo mwili huvunja mafuta yaliyohifadhiwa katika mwili na kuweka ustawi mzuri bila kuhisi uchovu.
Na katika hadithi mtume Sallahu alayhi wassallam  anasema: “Fungeni mtapata siha na afya” (imepokelewan na imam zubayd) katika kitabu cha “ITHAAFU SAADAT EL-MUTTAQYBA” 401:7
Na ameitaja Mundhiry katika kitabu chake cha “ATTARGHYBU WATTARHYB” 83:2

EWE ALLAH ULIETUKUKA TUPE KHERI NA FAIDA ZINAZOPATIKANA NDANI YA RAMADHANI.
WAFFAKANALLAHU FIYMA YUHIBUHUU WARDHWAA.

No comments:

Post a Comment