Monday 30 June 2014

WASIA KWA WENYE KUFUNGA RAMADHAN

Imeandaliwa na RAUDHWAH ISLAMIC GROUP

Ilipokaribia kuingia Ramadhan Mtume swalla Allahu alayhi wassalam aliwausia masahaba zake kuhusu Ramadhan, wasia tutakaouona katika mada zijazo Inshaa Allah. Na sisi tukiwa tumeuanza mwezi huu mtukufu ni muhimu kukumbushana yafuatayo ili uwe wasia wetu kwa ajili ya kufaidika na Ramadhan.
1-Kumshukuru Allah subhanahu wataala kwa kutuwafikisha kuidiriki Ramdhan. Hakika kushukuru ni miongoni mwa ibada azipendazo  Allah, na akaahidi kwa waja wake wakimshukuru basi atawaongeza neema alizowapa. Amesema Allah subhanahu wataala“Na alipotangaza Mola wenu : Kama mtanishukuru nitakuzidishieni, na mkikufuru hakika adhabu yangu ni kali sana” (Suratu Ibrahim: 7) na akasema tena katika Suratul Baqarah aya ya 152 “….na nishukuruni wala msinikufuru”.

Uhakika hatuwezi kufikia upeo wa kushukuru neema za Allah, kwani neema zake hazihesabiki wala hazipimiki. Amesema  Ibnul Qayyim rahimahullah: “Kuwafikishwa kushkuru neema za Allah, nayo ni neema inayohitaji shukrani, na kuwafikishwa kushkuru neema ya shukrani, ni neema nyengine inayohitaji shukrani, na hivyo hivyo inaendelea kua muislamu aendelee kumshkuru Allah mpaka mwisho wa pumzi zake”. Miongoni mwa neema hizo ni kuwafikishwa kuidiriki ramadhan, alau siku moja na usiku wake, kwani wangapi walitamani alau waweze kufunga lakini maradhi yamewaweka vitandani, hawawezi kufunga, na kula yao mpaka watumie mirija? Wangapi walitamani waidiriki ramadhan na family zao, lakini sasa wako kaburini ima katika viwanaja vya pepo au mashimo ya moto? Hatutojua neema mpaka ikiondoka. Tumepewa nafasi ya kujirekebisha matendo yetu ,kwa kuitumia vizuri Ramadhan,ili siku ya Qiyama tupate ujira mkubwa apatao mfungaji, ujira ambao mimi na weye wakati huu tumewafikishwa na Allah kuupata,na tuukimbilieni huku tukiomuomba Allah atuwafikishe tuimalize Ramadhan kwa salama, asitunyime ujira wake wote, na atuwafikishe tuidiriki Ramadhan inayokuja. Tumshukuruni Allah si kwa maneno tu, bali na kwa matendo kwa kuonesha kuithamini Ramadhan.

2-Kufunga kwa Imani na kutarajia malipo

Amesema Mtume (swalla Allahu alayhi wasallam)katika hadith sahihi, iliyopokelewa na Bukhari,Muslim na Nasai rahimahumullah na kusimuliwa na Abu-Hurayra radhiallahu anhu :“Yoyote atakaefunga Ramadhan, kwa imani na kwa kutarajia malipo atasamehewa dhambi zake zilotangulia”.

Kufunga kwa Imani ni kukiri kua funga ni amri ya Allah, na ni miongoni mwa nguzo za kiislamu, atakaesimamisha basi atakua ameusimamisha uislamu wake, na atakaevunja basi atakua kaubomoa uislamu wake. Allah hataki kula yetu na wala hana haja ya kukaa na njaa kwetu lakini anachotaka ni ibada na kama anavyosema katika lengo la funga ni kuwa anataka watu wawe wacha-Mungu yani wamuogope yeye Subhanah.
Kutarajia malipo ni kutaraji kuwa kutokana na funga tunayofunga basi kuna malipo mazuri yaliyoandaliwa kwa wafungaji,na malipo ya mwanzo ni kusamehewa dhambi na mengine yanafuatia Akhera. Ni madhambi mangapi tumeyafanya ya dhahiri na siri,makubwa na madogo yote hayo yatasamehewa kwa atakaefunga kwa imani na kutaraji malipo. Amesema Mtume wa Allah (swalla Allahu alayhi wasallam) katika Hadith inayosimuliwa na Anas(radhia Allahu anhu) :“Hakuna amali kwa asiekua na nia na hakuna na malipo kwa asiyeyatarajia” . Na tumkumbukeni Allah na ukubwa wake na kwamba akatayarisha malipo mazuri kwa wafungaji na papo hapo tuyatarajie malipo hayo.

3-Kuchunga ulimi na mambo ya kipuuzi.

Anasimulia kwamba amesema Mtume swalla Allahu alayhi wassalam katika hadithi iliyopokewa na Bukhari na Abu-Daud na kusimuliwa na Abu-Hurayra:“Yoyote asiewacha maneno ya upuuzi, na kuyafanyia kazi,basi Allah hana haja ya kuacha chakula chake na kinywaji chake”.  Je tumeizingatia hadithi hii tukafumba midomo yetu?

Amesema Mtume wa Allah  (swalla Allahu alayhi wasallam) kuwa “Yoyote anaemuamini Allah, na siku ya mwisho basi na aseme la kheri au anyamaze” .(Muttafaqun alayhi). La kusikitisha Ramadhan ndio imekua mwezi wa porojo,Ramadhan imekua ndio mwezi wa kusengenyana, Ramadhan ndio mwezi wa watu kukaa barazani na kuanza kutaja sifa za wapita njia,na wengine kukaa maskani na kuhadithiana uongo. Tumejiweka wapi na hadithi hii?

Tokea hapo mwanzo Allah hahitaji chakula chetu wala kukaa  kwetu na njaa lakini analolitaka ni ucha-mungu,na haupatikani kwa kuzungumza ovyo,na kwa mwenye kusema uongo na kufanya upuuzi mwengine basi ni bora kwake kula kwani Allah hahitaji kulifungia tumbo akauwachia ulimi,kama kufunga basi na viungo vyote vifungwe. Hatopata hasara anaenyamaza kimya lakini hasara kwa asiweza kuumiliku ulimi wake.

Kumiliki ulimi ni jambo alousiwa Muadh bin Jabal na kaambiwa kuumiliki ulimi ndio itakua sababu ya kutengenea matendo yote iwe sala,swaumu,hajj na hata Jihad. Aliulizwa Mtume (swalla Allahu alayhi wasallam):” Ni kipi kitachowaingiza wengi motoni ? Akajibu kua ulimi na utupu ndivyo vitakaowaingiza wengi motoni. Na akasema atakaenidhamini viungo hivyo basi na yeye amemdhamini Jannah,(Hadith imepokewa na Bukhari). Basi na tuanze kumdhamini Mtume wa Allah viungo hivi ndani ya Ramadhan hii kwa kutosema uongo,kutosengenya,kutukana na porojo nyenginezo.

4-Kutia nia ya kuzidisha kheri, na kushindana katika mazuri.

Muumini wa kweli hatasheki na kufunga tu ndio ikawa basi,wala hatosheki na kusali sala zake tano, kisha ikawa ndio kishamuabudu Allah. Kumuabudu Allah hakutoshi kwa dakika 25 kwa sala zote tano, ndani ya masaa 24. Allah hahitaji kupangiwa au kutengewa muda kwani muda wote ni wake na anastahiki muda wote kuabudiwa. Alipotaja pepo na starehe zake akamalizia kwa kusema na washindane wenye kushindana(Muttafifin :26) na kwengine akasema Kwa mfano wa haya nawatende watendao. (swaaffaat :61). 

Pepo inahitaji kushindaniwa kwani kama anavyosema Rasuul (swalla Allahu alayhi wasallam) kuwa “….Hakika bidhaa ya Allah ni ghali na bidhaaa ya Allah ni pepo.(Tirmidhy).  Ikiwa kushindana kwenyewe sisi ndio tutaenda na sala tano tu ambazo hazina khushui ndani yake, na haikutimizwa rukuu wala sijdah, mbele ya wale ambao wanaswali mpaka kuvimba miguu yao, na kuroa ndevu zao kwa kulia na kukesha usiku mzima, kwa kumuabudu Allah hivi tutakua sawasawa? Au ndo sisi tunashindana kwa aina za vyakula na nani kapika vingi na vizurii?

Wengi wetu kabla ya Ramadhan tulitia nia ya kuzidisha kufanya kheri, na wengine baada ya kufanya vibaya Ramadhan zilopita, tukajiapiza Ramadhan ijayo nitafanya vizuri, na nitamuabudu Allah kikamilifu, lakini tunayakumbuka haya au pia tunasubiri ya mwakani, ili tufanye vizuri kwa kua Ramadhan hii tuko na mishughuliko ya world cup, hatuna muda wa kumuabudu Allah.

Na tuipambeni Ramadhan yetu kwa Qur-an na qiyamul-layl. Adhkaar na madarsa na vikao vya kheri,Tutieni nia ya kuzidisha kheri na miongoni mwa mambo tunaotakiwa kuyaazimia kuyafanya  ni kutekeleza sunna ya itikafu, sunna ambayo hakuiachapo Mtume baada ya kuhamia Madina na mwaka aloiwacha ikabidi ailipe lakini ndio sunna iliyokimbiwa na wengi.

5-Kuwahurumia wanyonge na kuacha israfu.

Anasema Allah (subhanahu wataala) “…. Na amewanyanyua daraja baadhi yenu juu ya wengine ili akufanyieni mtihani kwa hayo alokupeni…” (An-aam 165).Na akasema tena katika Suratu-Nahli aya ya 71 “Na Allah amewafadhilisha baadhi yenu kuliko wengine katika rizki, Je wale walofadhilishwa,hawarejeshi rizki zao,kwa wale wanaowamiliki kwa mikono yao ya kulia?”.

Kutofautiana kwa kipato ni dalili za uwepo wa Allah kuonesha anampa amtakae na humnyima amtakae na kwamba kupata si kwa utashi wa mtu, bali ni mipango ya Allah. Na akawataka waja wake wasaidiane. Bila shaka miongoni mwa jamii za kiislamu tunazoishi nazo wako wanaofunga lakini wasijue wataftari nini, na wanafunga hawana daku ya kula ili waweze kufunga vizuri.

Wanafunga kwa kua ni amri ya Allah (subhanahu wataala) lakini kipato chao na uwezo wao hauwaruhusu kufanya hivyo.  Watu aina hiyo wanahitaji kuangaliwa kwa jicho la huruma na wale wenye uwezo. Si vibaya kila siku kumlisha maskini mmoja kwani sadaka ya kulisha chakula ina thamani kubwa mbele ya Allah (subhanahu wataala). Na Amesema Mtume wa Allah katika hadithi inayosimuliwa na Saad bin Khalid:”Atakaemfutarisha aliefunga, basi atapata ujira sawa na wake, pasi na kupungua ujira wa mfungaji chochote”(Tirmidhy,Nasai na Ibnu-Majah). 

Ikiwa ni hivyo basi na kuftarsha kwetu tusiwasahau maskini na sio shughuli zetu za kuftarisha kujazwa matajiri na wenye uwezo wao ambao hata hicho chakula hawakihitaji. Kwa kutumia kiyasa ya hadith ya Rasuul inayosimuliwa na Abu-Hurayrah kua chakula kibaya ni chakula cha harusini, kwani wanaalikwa wasiokihitaji; basi na ftari zetu kesi ndio hiyohiyo, tunawasahau maskini na wote wanaoalikwa hawakihitaji. Tusitosheke na thawabu za kuftarisha mtu bali tutake na thawabu za kulisha maskini kwani tukialika matajiri tutapata thawabu za kuftarisha tu lakini kualika maskini itakua ni thawabu za kuftarisha na za kulisha maskini.
           Ama kuhusu israfu tumeona maudhui yake katika mada zilopita

6-Kukumbuka njaa na kiu siku ya Qiyamah.

Moja kati ya mambo walohusishwa Mitume na ndo ikawa kama zawadi yao hapa duniani amesema Allah subhanah “Hakika tuliwachagua kwa lile jambo zuri kabisa la kuikumbuka Akhera” (Swaad :46). Ni zawadi ambayo imewafanya kutojali maisha ya dunia ni kutoshughulishwa na starehe za duniani.

Amesema Allah (subhanahu wataala) hii kuonesha kua kila kitu chao walikua wakifiri akhera.Na hivyo ndio anavyotakiwa muislamu wa kweli awe. Awe anafikiri akhera,kwani nguzo zote za kiislamu kuanzia sala,swaumu na hata hajji vinamkumbusha mtu mambo yatakayotokezea siku ya kiyama. Funga inatakiwa imkumbushe mtu njaa na kiu, kitakachowakuta watu wa motoni na kutokana na kiu hiyo wataomba kwa watu wa peponi kama anavyotusimulia Allah (subhanahu wataala) katka suratu A’raf  aya ya 50 “Na watanadi watu wa motoni kuwaita wa peponi: Tumiminieni maji au chochote katika alivyokuruzukuni Allah. Watasema watu wa peponi: Hakika Allah ameviharamisha vyote viwili (yani chakula na maji) kwa makafiri”. Hivyo basi mtu anapokaa na njaa na kiu akumbuke kua akhera watu waovu watakaa na njaa na kiu.(Allah atuhifadhi)

Allah atuwafikishe kuyatekeleza haya na mengineyo ya kheri.

Sunday 29 June 2014

Fadhila za kusali Dhuhaa

Makala imeandaliwa na Raudhwah Islamic Group

Imesimuliwa na Abu-Hurayra -radhi za Allah ziwe juu yake- amesema:"Ameniusia Kipenzi changu(swalla Allahu alayhi wasallam) mambo matatu: Kufunga siku tatu kila mwezi,Rakaa mbili za Dhuha na kusali witri kabla ya kulala" Imepokelewa na Bukhari na Muslim na pia Mtume swalla Allahu alayhi wassalam alimuusia hayo hayo swahaba wake mwengine Abuu-Dardai radhia Allahu anhu katika hadityhi ilopokelewa na Imam Muslim na Abu-Daud

Ndugu zangu wa kiisalamu, sala ya dhuha ni sala yenye ujira mkubwa lakini ni katika swala ambazo zimesahaulika katika jamii ya kiislamu, na hata wengine hawajui kama kuna sunna hiyo, hii ni kutokana na kuwa na mishughuliko mingi ya kidunia kwani swala hii huswaliwa robo saa mara baada ya kuchomoza  jua mpaka kabla ya adhuhuri, hivyo watu huwa katika mishughuliko yao, na kusahau kusali sala hii, Anasimulia swahaba Abdullah bin Amr bin Aas -radhiallahu anhu kua mara moja maswahaba walirud katika vita hali ya kua wamepata ngawira nyngi na wamerudi katika muda mfupi sana, wakawa watu wanazungumzia kuhusu habari yao, Mtume akawauliza"Jee nikutajien kitu chenye thamani kuliko hata hizo ngawira na chenye kutosheleza muda? Maswahaba wakasema ndio. Akawaambia:Mwenye kutawadha akaelekea msikitini na kusali dhuhaa basi huyo kapata zaidi kuliko hata hizo ngawira" Imepokelewa na Imam Ahmad

Atakaeswali Dhuhaa kachukuliwa dhamana na Allah ya kusimamiwa mambo yake kwa siku ile kama anavyosema Mtume swallahu alayhi wassalam katika hadithi ilopokelewa na Uqba bin Amir radhia Allahu anhu kua "Amesema Allah kumwambia mwanadamu:Ewe mwanadamu nitosheleze mwanzo wa mchana kwa rakaa nne nami nitakutosheleza mwisho wa mchana" Imepokelewa na Imam Ahmad

swala ya dhuhaa ina rakaa mbili mpaka nane na muda wake ni robo saa baada ya kuchomoza jua na kabla ya adhuhuri , ina fadhila nyingi Allah atuwafikishe kuisali na atulipe ujira kamili
Wallahu a'alam.

Usisahau kusali DHUHA

VIPI TUTAIPOKEA RAMADHANI


Makala imeandaliwa na Raudhwah Islamic Group

Kila sifa njema zinamstahikia Allah Mola wa viumbe vyote. Sala na salamu zimuendee Mtume wetu Muhammad (swalla Allahu alaihi wa sallam) na ahli zake na maswahaba wake.

Kwa hakika mwezi wa Ramadhani tayari umeshafika. Na baada ya muda mchache tutaingia katika mwezi huo mtukufu. Mwezi uliokuwa bora. Mwezi ambao ni shamba la watenda wema ili kuchuma mazuri yatakayowafaa kesho akhera. Ni mwezi wa kuomba tawba tukasemehewa dhambi zetu. Ila suala la muhimu kabisa ni vipi fursa hii ya Ramadhani tunaweza kuitumia? Ni lazima uweke maandalizi ambayo yatakuja kukufaa na kuyafanya ndani ya mwezi wa ramadhani.

Kwa nini tuuthamini mwezi huu wa Ramadhani? Na kwa nini inamlazimu muislamu kuwa na makusudio na jitihada maalum ndani ya Ramadhani. Kwanza tuangalie hadithi ya Mtume (swalla Allahu alayhi wasallam) inayosema “ Kutoka kwa Abdul rahmaan Bin Sakhar Al dausy (Abuu Huraira) (radhi za Allah ziwe juu yao)  amesema RASOUL  (swalla Allahu alayhi wasallam) “UMEPEWA UMMAH WANGU MAMBO MATANO KATIKA RAMADHANI HAUKUWAHI KUPEWA UMMAH WOWOTE KABLA YAKE.
1-HARUFU INAYOTOKA KWENYE KINYWA CHA ALIYEFUNGA INAPENDEZA ZAIDI MBELE YA ALLAH KULIKO HARUFU YA MISKI.
2- MALAIKA HUWAOMBEA MSAMAHA WAJA HAO MPAKA WAFTARI.
3- ALLAH HUIANDAA NA KUIPAMBA PEPO YAKE KILA SIKU NA HUIAMBIA JANNAH KWA WAKARIBIA WAKATI AMBAPO WAUMINI WATATUPULIA MBALI MITIHANI MIKUBWA YA DUNIA NA KUKUINGIA.
4-SHETANI HUFUNGWA MINYORORO ILI WASIWATIE UOVU KAMA AMBAVYO HUFANYA MIEZI MENGINE.
5-USIKU WA MWISHO WA RAMDHANI WAFUNGAJI HUSAMEHEWA MADHAMBI YAO”  (Imepokelewa na Ahmad na Baihaqi)

Ndani ya mwezi wa ramadhani kuna makumi matatu. Rasoul swalla Allahu alayhi wasallam anasema ya kwamba mwanzo wake ni rehma katika yake ni magh-firah na mwisho wake mja kuepushwa na moto.
Mwezi wenyewe ndio unakaribia kutufikia bila shaka mambo mazuri kama hayo kila mtu anahamu ayapate lakini unahitaji maandalizi sasa mimi na wewe je! vipi tutaweza kuupokea mwezi mtukufu wa ramadhani.

1-Kwanza kabisa muislamu ahakikishe anajua elimu kamili juu ya funga. Kuanzia  sharti za kusihi kwa wafunga, yanayobatilisha funga, nani anaruhusika kufungua au kutofunga, yaliyo sunna kwa mwenye kufunga na mengineyo.

Ikiwa muislamu atayajua hayo atakuwa na tahadhari ya kuichunga funga yake ili asije akawa anakaa na njaa ila hana chochote katika funga yake.

2- Kuchukua tahadhari zaidi na dhambi zinazotokana na ulimi. Katika viungo ambavyo Mtume (swalla Allahu alayhi wasallam) amesema yeyote atakaemdhamini viungo hivyo kwa maana kuvitumia katika kheri na akajiepusha na haramu basi anamdhamini pepo. Kutoka kwa Sahli bin Saad (Radhiya Allaahu anhu) amesema: Mtume (Swalla Allaahu alayhi wa aalihi wa sallam) amesema: "Atakayenidhaminia kilichomo baina ya taya zake [yaani ulimi] na kilichomo baina ya miguu yake (yaani tupu au sehemu za siri) nami nitamdhamini Pepo" (Al-Bukhaariy na Muslim)

Suali litakuja je ulimi unaweza kumfanya mtu asiwe na funga? Tuangalie hadithi ya Mtume (swalla Allahu alayhi wasallam) inayosema " Yule ambae haachi kusema uongo na haachi vitendo viovu. Allah (subhanahu wataala) hana haja na funga yake." Bukhari na Muslim.

Hadithi ya hapo juu inaonesha wazi ikiwa mtu hatofunga pamoja na kuuzuia ulimi wake na maasi basi hatokuwa na funga. Hivyo muislamu aupokee mwezi huu kwa kukusudia hasa kuwa mbali na dhambi kama za kusengenya,kusema uongo,matusi basi ajue Allah hana haja na funga yake na anakaa na njaa tu. Allah atujaalie wale ambao watazizuia ndimi zao na dhambi hizo na mfano wa hayo.

3- Muislamu aweke nia na azma ya kufunga ramadhani kwa uzuri na kwa kutaraji malipo kutoka kwa Allah (subhanahu wataala). Amesema Mtume (swalla Allahu alayhi wasallam) : "Atakayefunga Ramadhaan kwa imani na kutaraji malipo atasamehewa madhambi yake yaliyotangulia " Bukhaariy na Muslim.

4- Kuhakikisha muislamu kuwa anasali sala za faradhi kwa wakati na kujihimiza sana na kusali sala za sunna. Miongoni mwa sala za sunna ni rakaa 12 za sunna (Qabliya na Baadiyah), sala ya dhuha,sala ya witri na sala ya tarawehe.

5-Kushikamana na kusoma quran kwani mwezi wa ramadhani ndio ulioteremshwa Quraan. Allah (subhanahu wataala) anasema "Mwezi wa Ramadhani ambao imeteremshwa humo Qur'ani kuwa ni uwongofu kwa watu, na hoja zilizo wazi za uwongofu na upambanuzi. "(Baqara :185).

Hata Jibril alikua akishuka kila mwaka katika mwezi wa ramadhani kwa kumdurusisha Quraan Mtume (swalla Allahu alayhi wasallam)  sio kua hajui kusoma ila ni kuonesha ubora na umuhimu wa ibada hiyo ndani ya mwezi wa Ramadhani.

Kusoma Quraan kuna faida nyingi sana. Miongoni mwa faida hizo ni mtu kupata thawabu kwa kila herufi atakayoisoma. Imetoka kwa Abdullahi bin Masuud (Radhiya Allahu anhu) kwamba Mtume (Swalla Allahu alayhi wasallam) amesema: "Atakayesoma herufi moja katika kitabu cha Allaah atapata hasanah (jema) moja, na kila hasanah moja ni sawa na thawabu kumi, wala sisemi "Alif-Laam-Miym" ni herufi moja, bali Alif ni herufi moja na Laam ni herufi moja na Miym ni herufi moja))  At-Tirimidhiy.

Pia Quraan itakuwa kiombezi kwa watu wa Quraan. Watu waliokuwa wamedumu kusoma Quraan kwa mazingatio na kuifanyia kazi. Imetoka kwa Abu Umaamah (Radhiya Allahu anhu)  kwamba Mtume (Swalla Allahu alayhi wasallam)  amesema "Someni Qur-aan kwani itakuja siku ya Qiyaamah ikimuombea   mwenye kuisoma" Muslim.

Hivyo basi muislamu azidishe kusoma Quraan na ajitahidi aisome kwa mazingatio.

6- Kuhudhuria katika sehemu mbali mbali za kujifunza kama katika mihadhara na madarsa mbali mbali.  Jambo hili leo hii wengi wetu tumeliwacha na tumekuwa tukitumia muda wetu mwingi ndani ya whatsapp,facebook na mitandao mengineyo pamoja na vibaraza vyenye mazugumzo yasiyokuwa na manufaa. Na mtu anapoambiwa ahudhurie sehemu za kheri basi hutoa sababu zisizo na msingi ila yote hayo tumeghafilika na mauti na imetuhadaa dunia.
Sehemu za kujifunza na kukumbushana yaliyo mema ni nzuri sana katika kuufanya moyo wa mja uwe unaathirika na maneno ya Allah. Na hii itamfanya daima awe anakumbuka wajibu wake kama kiumbe wa Allah(subhanahu wataala) katika ulimwengu huu.

Mwisho kwa kumalizia tujitahidini kuyafanyia kazi haya tuayokumbushana kabla ya ramadhani ,ndani ya ramadhani na baada a ramadhani ili tuweze kuzitafuta radhi za Allah hapa duniani na kesho akhera.
Tunamuomba Allah (subhanahu wataala) atujaalie wale ambao watafika ramadhan na watafunga na kupata ujira mkubwa kutoka kwa Allah (subhanahu wataala) pamoja na kusamehewa dhambi zetu. Aaamin.

MALIPO YA MWENYE KUFUNGA SIKU YA QIYAMAH


Makala imeandaliwa na Raudhwah Islamic Group

Kila sifa njema zinamstahikia Allah (subuhanahu wata‘ala) Muumba wa wanaadamu na viliyomo duniani na akhera na baina yake na akavikadiria maisha yao. Swala na salamu zimuendee Mtume wetu Muhammad (swalla Allahu alaihi wa sallam).
Ndugu wa Kiislamu, Allah (subuhanahu wata‘ala) ametuwekea namna mbali mbali za ibada ili kutujenga kiroho na kimwili kuwa ndani ya twa‘a yake wakati wote. Swaum (funga) ni moja ya ibada hizo na ni nguzo ya nne katika Uislamu kama anavyosema Mtume (swalla Allahu alaihi wa sallam): “Uislamu umejengwa kwa nguzo tano: Kushuhudia kuwa hapana Mola apasae kuabudiwa isipokuwa Allah na Muhammad ni mja wake na mjumbe wake, Kusimamisha Swala, Kutoa zaka, Kufunga Ramadhaan, na Kwenda Makka kuhiji kwa mwenye uwezo.” Bukhary na Muslim.
Na imethibiti kufaradhishwa kwake ndani ya mwezi wa Ramadhaan pale Allah Aliposema: “Enyi mlio amini! Mmefaradhishiwa Saumu, kama waliyo faradhishiwa walio kuwa kabla yenu ili mpate kuwa wachaMungu.” [Al-Baqara 2 : 183].
Swaum ni ‘amali yenye kumpatia mja malipo mengi makubwa makubwa wakati ambao amefunga kwa matendo mbali mbali ya ibada anayoyafanya akiwa ndani ya mwezi mtukufu wa Ramadhaan. Kwa leo in sha Allah, tutazungumzia malipo ambayo Allah (subuhanahu wata‘ala) amemuandalia mfungaji siku ya Qiyamah.
Swaum ni kiombezi. Swaum itakuja kumuombea shifaa mwenye kufunga siku ya Qiyama kama ilivyothibiti hadithi kutoka kwa Abdullah ibh Amr (radhi za Allah ziwe juu yake), Amesema Mtume (swalla Allahu alaihi wa sallam): “Funga na Quran ni  viombezi viwili vya mja wa Allah siku ya Qiyamah, Funga itasema: Ewe Mola, nilimzuia na chakula na matamanio wakati wa mchana, niruhusu nimuombee. Na uombezi wao utakubaliwa.” Ahmad.
Swaum ni sababu ya kumuingiza mtu Peponi. Mwenye kufunga na akaitimiza funga yake na akajiepusha na maovu na machafu yanayopunguza fadhila za swaum, Allah amemuandalia pepo kwa ajili yake. Abuu Umamah amesema: “Nilienda kwa Mtume (swalla Allahu alaihi wa sallam) nikamwambia: Niamrishe ‘amali ambayo itaniwezesha kuingia peponi. Akasema: “Jilazimishe na kufunga kwani hakuna iliyo sawa na hiyo.” Baadae nikaja tena kwake na Akasema: “Jilazimishe na kufunga.” Ahmad, An-Nasai na Al-Hakim.
Allah atawafadhilisha wenye kufunga kwa kuwaingiza Peponi kupitia mlango maalum uitwao Rayyaan. Amesimulia Sahl ibn Sa‘ad (radhi za Allah ziwe juu yake) kuwa Mtume (swalla Allahu alaihi wa sallam) amesema: “Kuna mlango wa kuingilia Peponi uitwao Rayyaan, siku ya Qiyama utasema: wako wapi walokuwa wakifunga? Akishapita wa mwisho kuingia (mlango) utafungwa.” Bukhary na Muslim.

Swaum humsaidia mfungaji kuwekwa mbali na mashimo ya moto wa Jahannam. Imesimuliwa na Abu Said al-Kudry (radhi za Allah ziwe juu yake) kuwa Mtume (swalla Allahu alaihi wa sallam) amesema: “Hakuna mja atakaefunga siku moja katika njia ya Allah isipokuwa Allah atamuondoshea moto umbali wa miaka sabiin na uso wake.” Imepokewa na kundi la watu wa hadithi isipokuwa Abu Daud.
Swaum ni ‘amal yenye malipo makubwa kiasi kwamba Allah (subuhanahu wata‘ala) amesema kuwa ‘amali hii ni kwa ajili yake na yeye ndiye atakayeilipa pasi na kubainisha ukubwa wa malipo yake. Kutoka kwa Abu Hurayrah (radhi za Allah ziwe juu yake), Mtume (swalla Allahu alaihi wa sallam) amesema: Allah amesema: Kila ‘amali anayoifanya mwanaadam ni kwa ajili yake isipokuwa funga, kwani hiyo ni kwa ajili yangu, na Nitatoa malipo kwa ajili yake (funga). Funga ni ngao, ikiwa mtu amefunga asitumie lugha chafu, asinyanyue sauti yake, au kufanya vitendo viovu. Ikiwa mtu atamtolea maneno au kupigana naye aseme “mimi nimefunga” ... ” Muslim, Ahmad na An-Nasai.
Ndugu wa Kiislamu, hayo  ni katika baadhi ya Aliyotuandalia Allah (subuhanahu wata‘ala) endapo tutaitekeleza ibada hii kwa usahihi wake na kujiepusha na yale yote yenye kupunguza fadhila za swaum kama kucheza game wakati mtu amefunga au karata au kutizama filamu na tamthilia zinazokwenda kinyume na maadili ya Uislamu.
Tunamuomba Allah (subuhanahu wata‘ala) atuwezeshe kuifunga Ramadhani hii na zijazo kwa namna anayoiridhia na kuifurahia na atuwezeshe kupata malipo yote aliyowaandalia wafungaji. Amin.

FAIDA ZA MWENYE KUFUNGA HAPA DUNIANI


Makala imeandaliwa na Raudhwah Islamic Group

Kila sifa njema zinamstahikia Allah Mola wa viumbe vyote. Sala na salamu zimuendee Mtume wetu Muhammad (swalla Allahu alaihi wa sallam) na ahli zake na maswahaba wake.

Allah Subhaanahuu Wataala ametufaradhishiya funga sisi tulioamini, ili tupate uchamungu pamoja na faida mbali mbali zinazopatikana katika funga. Na tujue funga hii ni ile iliyofungwa kwa kujua na kutambua sharti, sunna na yale yanayobatilisha funga kwa mfungaji, ndipo tutakapopata uchamungu na   faida nyingi.
Hivo basi Kwa mwenye kufunga anapata faida za kiroho, za kijamii na katika siha yake. Kama zifuatazo:
Miongoni mwa faida za kiroho ni kule kuwa na subra na kuijenga khasa katika nafsi yake, na anajifunza kuifunga nafsi na kuisaidia kuwa katika hali hiyo.

Na atailea nafsi katika Taqwa na uchamungu, kwani uchamungu ndio lengo kubwa la funga. Allah anasema: “Hakika mumuefaradhishiwa funga kama walivofaradhishiwa walio kabla yenu ili muwe wachamungu” 2:183
Faida nyengine kwa mwenye kufunga ni kukubaliwa dua yake.

Hadithi aliyoipokea Imam Al Tirmidhy Radhi za Allah ziwe juu yake amesema : “Watu watatu hukubaliwa dua zao; aliyefunga mpaka aftari, kiongozi muadilifu na aliyedhulumiwa”
Pia akasema tena Mtume Swalla Allahu alayhi wassalam “Dua ya aliyefunga hupokelewa pale anapoftari” (Imepokelewa na Ibnu Maajah).

Angalia kwa namna gani faida na fadhila tunazopata pale tunafunga hapa hapa duniani.
Ama faida za kijamii kwa mwenye kufunga ni:
Kuurejesha umma au jamii katika nidhamu na umoja, na kupenda uadilifu na usawa.
Na kuengeza na kuzidisha kwa waumini upole na huruma, na tabia ya kuwa na ihsani, pale jamii inapojifunga na kuzuiya kufanya mambo ya shari na ufisadi wakati wote wa funga.

Na katika faida nyengine ya funga ni:
Faida ya kisiha na kupata afya kwa mwenye kufunga, kwani anasafisha mfumo wake wa chakula na kupumzisha tumbo, kuusafisha mwili kutokana na vidudu na minyoo inayoleta maradhi. Maana vidudu hivi hupata nguvu na pale mwanadamu anapokuwa anakula (parasites).

Na kupunguza kiwango kikubwa cha mafuta na uzito katika tumbo, kwa maana kisayansi mwili wa mwanaadamu unatakiwa usipungue kiwango cha glucose au sukari katika damu, kiwango hichi huwa sawa pale mwanadamu anapokula chakula, hivo mda anaofunga chakula na kiwango cha sukari hupungua mwilini ila mwili unajaribu kuangalia sehemu ama chakula kilichohifadhiwa na kukivunja na kukitumia ili mwili uwe sawa na kuwa na nguvu. Ndipo mwili huvunja mafuta yaliyohifadhiwa katika mwili na kuweka ustawi mzuri bila kuhisi uchovu.
Na katika hadithi mtume Sallahu alayhi wassallam  anasema: “Fungeni mtapata siha na afya” (imepokelewan na imam zubayd) katika kitabu cha “ITHAAFU SAADAT EL-MUTTAQYBA” 401:7
Na ameitaja Mundhiry katika kitabu chake cha “ATTARGHYBU WATTARHYB” 83:2

EWE ALLAH ULIETUKUKA TUPE KHERI NA FAIDA ZINAZOPATIKANA NDANI YA RAMADHANI.
WAFFAKANALLAHU FIYMA YUHIBUHUU WARDHWAA.

YALIYO SUNNAH KWA MWENYE KUFUNGA


Makala imeandaliwa na Raudhwah Islamic Group

Kila sifa njema zinamstahikia Allah (subhanahu wata‘ala) Mola wa viumbe vyote vyenye kuonekanwa na visivyoonekanwa. Swala na salamu zimuendee Mtume wetu Muhammad (swalla Allahu alaihi wa sallam) na ahli zake na maswahaba zake.
Ndugu wa Kiislamu, kama ilivyo katika ibada ya swala kuwa kuna baadhi ya matendo ya sunnah hufanywa ndani yake ili kuengeza fadhila na daraja ya swala hiyo, kadhalika katika ibada ya swaum (funga) kuna matendo ya sunnah amabayo mfungaji akiyafanya hupata fadhila zaidi katika funga yake na kupata ujira maradufu.

Katika makala hii in sha Allah, tutazungumzia baadhi ya mambo yaliyo sunnah kwa mwenye kufunga kuyafanya. Miongoni mwa mambo hayo ni haya yafuatayo.

Kula daku

Daku ni chakula kinacholiwa mwishoni mwa usiku kwa ajili ya kutekeleza sunnah ya Mtume (swalla Allahu alaihi wa sallam) na pia kumfanya mfungaji awe mchangamfu na mwenye nguvu hali itakayompelekea kutokushindwa kufanya harakati zake za maisha kama ilivyo kawaida yake katika siku za kula mchana. Imethibiti hadithi kutoka kwa Anas bin Malik (radhi za Allah ziwe juu yake) amesema: Amesema Mtume (swalla Allahu alaihi wa sallam): “Kuleni daku kwani katika daku kuna baraka.” Bukhary na Muslim.

Kuchelewesha kula daku
Pia imesuniwa kuchelewesha kula daku hadi karibu na swala ya asubuhi kama ilivyopokewa hadithi na Anas kutoka kwa Zayd bin Harith (radhi za Allah ziwe juu yake) ambae amesema: “Tulikula daku na Mtume (swalla Allahu alaihi wa sallam) kisha tukainuka tukaswali.” Nikasema: “Kulikuwa na muda gani baina ya adhana na daku?” Akasema: “Ni muda wa kusoma aya hamsini (50).” Bukhary

Kuharakisha kufutari (kufunguwa)
Vile vile ni sunnah kuharakisha kufunguwa mara tu baada ya jua kuzama kama alivyokuwa Akifanya Mtume (swalla Allahu alaihi wa sallam), tofauti kabisa na wafanyavyo baadhi ya ndugu zetu ambao husubiri mpaka wamalize kuwali magharibi pamoja  na sunnah yake ya baadiyah. Kufanya hivi sio sahihi kwa mujibu wa mafundisho ya Mtume wetu. Imepokewa hadithi kutoka kwa Mtume (swalla Allahu alaihi wa sallam) amesema: “Watu wataendelea kuwa katika hali nzuri maadam wanaharakisha kufunguwa (funga zao).” Bukhary na Muslim.


Kufunguwa kwa kula tende
Ni sunnah kwa mwenye kufunga kufutari kwa kula tende mbichi, ikiwa atakosa basi kwa tende kavu na ikiwa atakosa basi na afungue kwa kunywa mafunda ya maji. Kama ilivyopokewa kutoka kwa Anas (radhi za Allah ziwe juu yake) ambae amesema: “Mtume (swalla Allahu alaihi wa sallam) alikuwa akifunguwa kwa tende mbichi kabla ya kuswali, ikiwa hamna tende mbichi basi kwa kavu na ikiwa hamna basi hunywa mafunda machache ya maji.” Abu Daud na Tirmidhy.

Kuomba dua kwa wingi
Vile vile inahimizwa kuomba dua kwa wingi wakati mtu akiwa amefunga na kabla ya kufutari kwani mtu aliyefunga ni katika watu ambao hukubaliwa dua zao, kama ilivyokuja hadithi ya Mtume (swalla Allahu alaihi wa sallam) isemayo: “Dua za watu watatu hazirejeshwi (hazikataliwi), dua ya baba (kwa mwanawe), dua ya mtu aliyefunga, na dua ya msafiri.” Imepokewa na Al-Bayhaky kutoka kwa Anas (radhi za Allah ziwe juu yake).

Kujitenga na mabishano na majibizano
Mtu aliyefunga hatakiwi kuanzisha mabishano na malumbano, na kama mtu atakuja kwa ajili ya kugombana naye au kutaka kupigana naye basi ni wajibu wake kujizuia na kusema kuwa “mimi nimefunga” ili kuepukana na kuiharibu funga yake na kupunguza fadhila za funga yake.
Amesema Mtume (swalla Allahu alaihi wa sallam): “Funga ni Pepo hivyo kusiwe na mazungumzo machafu na tabia chafu. Ikiwa mtu atampiga au kumtukana (aliyefunga) na aseme, “Mimi nimefunga” mara mbili. Naapa kwa yule ambaye roho yangu iko Mikononi Mwake, harufu itokayo kinywani mwa mtu aliyefunga ni bora mbele ya Allah kuliko harufu ya miski. (Allah anasema:) “Ameacha chakula chake, kinywaji na matamanio yake kwa ajili Yangu. Funga ni kwa ajili Yangu Nami nitailipa, na matendo mema hupata malipo mara kumi yake.” Bukhary na Muslim.

Ndugu wa Kiislamu, ni muhimu pia juu yetu kuzidisha kufanya ‘amali nyingi tukiwa tumefunga kama vile kutoa sadaka, kuwasaidia wahitaji na kutumia muda wetu mwingi kuisoma Quran na kuhudhuria madarsa ili kujifunza maana yake, kwani bila ya kujifunza maana yake hatutoweza kuishi kwa mujibu wa Quran na kupelekea kuishi maisha ambayo Allah haridhiki nayo na hatimae kuingia katika adhabu za Allah.

Ni muhimu pia kuendeleza yale yote ya kheri tunayoyafanya katika mwezi mtukufu wa Ramadhaan katika miezi myengine khassa kuhudhuria madarsa na kujifunza dini yetu. Kwani bila ya elimu hakuna litakalofanywa kwa usahihi wake.

Tunamuomba Allah atuwezeshe kuyafanya haya na mengine ya kheri hadi mwisho wa maisha yetu na Atuweze kupata Rehma zake na Kutuingiza katika Pepo yake. Amin.

SHARTI ZA KUSIHI KWA FUNGA- SEHEMU YA PILI


Makala imeandaliwa na Raudhwah Islamic Group

3 – KUJIZUIA KUFANYA TENDO LA NDOA KWA MAKUSUDI NA KUJITOA MANII

Ikiwa mtu atafanya jimai bila ya kukusudia basi mtu huyo atakuwa amesameheka. Kwa kauli ya Allah: “Lakini ipo lawama katika yale ziliyo fanya nyoyo zenu kwa makusudi.” (Suratul Ahzaab : 5).

Ama yule ambae atafanya jimai kwa makusudi basi huyo funga yake itabatilika na itamlazimu kwake yeye kuilipa funga hiyo pamoja na kutoa kafara. Kafara kwa yule ambae atafanya tendo la ndoa katika mchana wa Ramadhani ni :

i. Kuacha huru mtumwa.
ii. Kufunga miezi miwili mfululizo.
iii. Alishe maskini 60 kila mmoja kibaba kimoja.

Ikiwa mke au mume mmoja wao amemlazimisha kwa nguvu mwenzake kufanya tendo la ndoa ndani ya mchana wa Ramadhan na wamo katika funga basi yule aliemlazimisha mwenzake ndio itamuwajibikia kutoa kafara.

Na mwanamke hatakiwi akubali kufanya tendo la ndoa wakati amefunga ndani ya Ramadhani. Na  maulamaa wengine wakaengeza kwa kusema hata ikiwa anaweza kupigana na mume wake basi ampige. Kuonesha uzito wa funga. Na wala mtu asitumie kivuli kuwa amelazimishwa kujitetea ajue kuwa Allah (subhanahu wata‘ala) anajua kila kilichomo ndani ya nafsi ya mja wake.

Ikiwa mtu atafanya tendo la ndoa hali ya kuwa amefunga ndani ya Ramadhani kwa siku mbili tofauti basi ni juu yake kafara mbili. Kila funga moja basi na kafara yake moja.

Pia ikiwa mtu anafanya tendo la ndoa na baadae ikambainikia kuingia kwa alfajiri basi kinachotakiwa ni kuacha tendo la ndoa hapo hapo akakoge janaba na aendelee na funga yake.

Je ni wakati gani jimai ya mchana wa Ramadhani inaruhusika?

Ikiwa mke na mume wote wana dharura za kisheria za kutofunga kwa mfano wote wamesafiri basi hakuna ubaya na hawatotoa kafara. Kwani awali ruhusa ya kutofunga ishakuwepo kwao wao.

Ikiwa mume amerudi safari na mke wake hakufunga siku hiyo kwa sababu ya hedhi na ametwaharika baada ya funga kuanza, basi tendo la ndoa kwao wao linaruhusika kwani mume hajafunga na mke hakufunga.

Ama kinyume na hali hizo wakifanya tendo la ndoa ndani ya mchana wa Ramadhani wakiridhia wenyewe basi kwa kila mmoja juu yake kafara ama mmoja amemlazimisha mwenzake basi yule aliyemlazimisha mwenzake ni juu yake kutoa kafara.

Kujitoa maniii kwa makusudi kunabatilisha funga. Hivyo basi yeyote ambae amefunga anatakiwa ajizuie na kujitoa manii kwa makusudi. Na mfano wa kujitoa manii kwa makusudi ni puunyeto, au kwa kumkumbatia au kumchezea mkewe au mwanamke mpaka akatokwa na manii.

1-SUALI
Walifanya jimai kabla ya kuanza kwa funga na baadae hawakuwahi kukoga janaba wakalala mpaka ikaingia alfajiri. Je nini hukmu ya funga yao?
JIBU
Ikiwa walitia nia ya kufunga basi funga yao itasihi. Kinachowalazimu ni kukoga janaba ili waweze kuswali na waendelee na funga yao. Na hili ni kwa ushahidi wa hadithi ya Bibi Aysha na Ummu Salamah (radhiya Allahu anhuma) “kwamba Mtume (Swalla Allahu alayhi wasallam) alikuwa akiamka na janaba kutokana na kukutana kimwili na wake zake, kisha anakoga na kufunga.” (Al Bukhariy na Muslim).

2-SUALI
Alifanya jimai bila ya kujua kwamba alfajiri imeingia. Na baadae akajua kuwa alifanya jimai wakati tayari alfajiri ishaingia. Nini hukmu yake?

Ikiwa wakati anafanya hajui kama wakati umeingia basi atakoga na ataendelea na funga yake. Kwani hakuna kosa kwa mtu kutojua.Ama akifanya kwa kusudi basi funga itabatilika funga yake na itamlazimu kutoa kafara na kuilipa funga hiyo.

4-KUEPUKANA NA HEDHI NA NIFASI

Ni lazima kwa mwanamke anaetaka kufunga awe ametoharika kutokana na hedhi na nifasi. Na pindi mwanamke anapokuwa na hedhi au nifasi basi huwa ni wajibu kwake kuacha kufunga. Na hii ni amri kutoka kwa Allah (subhanahu wata‘ala) na mwanamke akitoharika ataendelea na kufunga. Pia siku ambazo ameziacha kwa kutofunga atakuja kuzilipa baada ya Ramadhani.

SUALI
Bado muda mdogo sana kumalizika kwa funga. Mwanamke akapatwa na hedhi. Je itahesabika funga yake ile?

JIBU
Hapana, haitohesabika funga ile kwa sababu wakati haujatimia. Na itamlazimu mwanamke huyo aje kuilipa funga hiyo baada ya kumalizika kwa Ramadhani.

SUALI
Mwanamke amepatwa na maumivu au dalili nyengine za kuonyesha atapatwa na hedhi ila hakupata wala hakutokwa na damu. Nini hukmu yake?
JIBU
Hatowajibika kuilipa na funga yake itakuwa sahihi.

SUALI
Ikiwa mwanamke siku zake za hedhi zimekaribia. Akaona matone ya damu ila damu haikutoka. Nini hukmu ya funga yake?
JIBU
Lazima ailipe funga hiyo kwani matone hayo ya damu yatahesabika kama ni damu ya hedhi.

SUALI
Miaka yote Ramadhan napata kufunga siku 10 tu au 11. Na zinazobaki nakuwa katika siku za hedhi. Sipati kufanya ibada ambazo zina fadhila kubwa kuliko miezi mingine. Nakuwa mnyonge kutokana na hali hiyo.
Je naweza kutumia vidonge vya kuzuia hedhi ?

JIBU
Kuhusu hedhi muda wake wajuu kabisa ni siku kumi na tano, zikizidi hapo huwa ni ugonjwa, kwa maelezo yako unakuwa ukitokwa na damu kwa takriban siku 20, hii inaonesha una tatizo jitahidi kutafuta tiba ya ugonjwa huo.
Ama ikiwa zitabaki siku 15 au chini ya hapo tutaizingatia kuwa ni hedhi, na kipindi unachokua ndani ya hedhi kuacha yale sheria iliokutaka kuyaacha ni ibada, hivyo ibada iliyokuzuilia kufanya ibada nyengine fadhila zake ni kubwa zaidi kwa wakati huo.
Pili.
Kuhusu kutumia vidonge vya hedhi wako maulamaa wanasema kuwa haifai kutumia vidonge hivyo kwani vimethibitika vina madhara.

Ama tukisema havina madhara basi ushauri wetu ni bora kuiacha hedhi katika utaratibu wake ndio bora zaidi kiibada na kiafya pia. Kwani ndio maumbile yake mwanamke alivyoumbwa na Allah (subhanahu wata‘ala). Na Allah ndie mjuzi zaidi.

SUALI
Ikiwa mwanamke amemaliza nifasi kwa siku chache mfano siku saba je anaweza kufunga?
JIBU
Ikiwa kweli imesita damu ya nifasi mwanamke huyo anaweza kufunga. Na Allah ni mjuzi zaidi.

SUALI
Ni ipi hukmu ya funga kwa mwanamke aliyeharibu mimba?
JIBU
Ikiwa mimba imeharibika kabla ya mtoto kuumbika basi damu hiyo si damu ya nifasi na mwanamke atakoga kujisafisha na kuendelea na funga yake.
Ikiwa mimba imeharibika baada ya mtoto kuumbika basi damu hiyo itakuwa ni ya nifasi na itambidi ajizuie kufunga mpaka pale itakaposita damu ya nifasi. Na Allah ni mjuzi zaidi.

SUALI
Mwanamke ametoharika kabla ya kuanza kwa alfajiri ya kweli. Akatia nia ya kufunga ila akachelewa kukoga josho. Je anaweza kufunga?
JIBU
Ndio anaweza kufunga. Kitakachomlazimu ni kukoga josho kabla ya kutoka kwa swala ya alfajiri ili asiache swala na ataendelea na funga yake. Na Allah ni mjuzi zaidi.

Hayo ndio masharti ambayo yanalazimika kutimizwa ili funga ya Muislamu isihi. Na kinyume cha masharti hayo ni kubatilika kwa funga hiyo. Na kama tulivyoeleza itamuwajibikia mtu huyo kulipa. Ama yule ambae kwa sababu ya kufanya tendo la ndoa yeye itamuwajibikia kulipa pamoja na kafara. Na Allah ni mjuzi zaidi.

SHARTI ZA KUSIHI KWA FUNGA - SEHEMU YA KWANZA


Makala imeandaliwa na Raudhwah islamic Group

Ili swaum isihi kuna sharti zake zitimizwe ndipo funga hiyo itasihi. Na sharti hizi zisipokamilika basi funga haitosihi au funga itabatilika na itamlazimu mwenye kufunga aje kuilipa funga hiyo. Hivyo hatutokuja kueleza yanayofunguza. Bali makala hii in shaa Allah itamtosheleza msomaji kujua sharti za kusihi kwa funga na kubatilika kwa funga. Pia katika baadhi ya vitabu wametumia neno NGUZO ZA FUNGA zote hizo ni sawa na wanakusudia kukieleza kitu hicho hicho.

1-KUTIA NIA KILA SIKU
Ni lazima kwa mwenye kufunga atie nia kwa kila siku anayofunga. Iwe funga hiyo ya sunna au faradhi kama Ramadhan. Na hatokuwa na funga yule atakaekuwa hajatia nia. Kwani katika hadithi kutoka kwa Sayyidina Omar (radhi za Allah ziwe juu yake) amesema: “ Nimemsikia Mjumbe wa Allah akisema: “ Hakika kila jambo huambatana na nia na kila mtu atalipwa kutokana na kile alichokinuwia … .” Bukhari na Muslim.

Na inamuwajibikia mwenye kufunga Ramadhan atie nia kabla ya kuanza kwa alfajiri ya kweli. Na endapo mwenye kutaka kufunga hatotia nia kabla ya wakati huo basi hatokuwa na funga. Na itamuwajibikia kwake yeye kuja kuilipa funga hiyo. Kwa ushahidi wa Hadithi ya Mtume (swalla Allahu alayhi wasallam): “Yeyote ambae hatoweka nia ya kufunga kabla ya alfajiri hatokuwa na funga.” Imepokewa na Imam Ahmad na An-Nasai. Hivyo inamlazimu atie nia kwa kuzingatia kabla ya kuanza kwa funga na nia hiyo iwe kwa kila siku atakayoifunga. Ama mwenye kufunga sunna anaweza kutia nia kabla ya kupambazukwa kwa jua kama ilivyoelezwa katika mada zilizopita.

Kwa nini mtu atie nia kila siku ndani ya Ramadhani? Swala humalizika kwa mtu kutoa salam. Na anapotaka kuingia katika swala nyengine basi analazimika kutia nia ya swala nyengine. Hivyo hivyo kwa mwenye kufunga, swaumu humalizika kwa kuzama kwa jua hivyo basi anaetaka kufunga siku ya pili lazima atie nia nyengine. Kwani anakuwa ameanza swaumu nyengine. Na hii ndio kauli yenye nguvu.

Je kutia nia ni kwa kutamka au moyoni tu inatosha?
Kwanza ni jambo lisilokuwa na shaka kuwa nia mahali pake ni moyoni. Ama suala la kutamka kwa kauli za maulamaa wengi ni jambo ambalo halikuthibiti katika dini. Hivyo basi mwenye kufunga atatia nia moyoni mwake kwani Allah anajua yale yote yaliyomo ndani ya nafsi zetu na hakifichiki kwake kitu chochote.
Ama ziko kauli katika madhehebu ya Imam Shafi kuwa kutamka nia ni sunna. Rejea katika kitabu cha MUQADDIMATUL HADHARAMIYYAH katika Mlango wa funga.

Ama mimi muandishi wa makala hii naunga mkono zaidi rai ya kuwa kutamka nia sio lazima. Muhimu mtu atie nia ndani ya moyo wake.

2- KUJIZUIA KULA NA KUNYWA

Ni lazima kwa mtu mwenye kufunga ajizuie kula na kunywa kuanzia kuingia kwa alfajiri ya kweli hadi kuzama kwa jua. Kwa kauli ya Allah (subhanahu wata‘ala): “Na kuleni na kunyweni mpaka kubainike kwenu weupe wa alfajiri katika weusi wa usiku, Kisha timizeni saumu mpaka usiku.”  (Suratul Baqara : 187).

Nini hukmu ya kula kwa kusahau

Yule ambae atakula kwa kusahau iwe kidogo au sana basi haitobatilika funga yake kwa ushahidi wa hadithi ya Abu Hurayrah (radhi za Allah ziwe juu yake) amesema : Amesema Mtume (Swalla Allahu alayhi wa sallam): “Mwenye kusahau nae amefunga, basi akala au akanywa na aikamilishe funga yake.” Al Bukhariy na Muslim. Na katika riwaya nyengine “Kwani hakika Allah amemlisha na amemnywisha.” Ila Muislamu azingatie asije kujiigiza kuwa amesahau kwani ataweza kuwadanganya watu lakini Allah hawezi kumdanganya hata kidogo.

Je kupiga mswaki ndani ya Ramadhan kwa kutumia dawa inasihi?

Kupiga mswaki ndani ya funga hilo linasihi kwani Mtume (swalla Allahu alayhi wasallam) alikuwa akipigwa mswaki nae amefunga. Ama suala linakuja kwenye kupiga mswaki kutumia dawa.  Dawa ya mswaki haibatilishi swaum ikiwa wakati anasafisha meno atatema na wala hamezi. Ama ikiwa atakusudia kumeza, swaumu yake itabatilika.  Na yule ambae anakhofia anaweza kumeza basi bora asitumie dawa. Na kilichopendekezwa zaidi na maulamaa mtu apige mswaki kwa kutumia dawa kabla ya kuanza kwa saumu na itakapoingia saumu apige mswaki bila ya kutumia dawa ili asije kutumia dawa na kuimeza.

Je kuonja chakula wakati mtu amefunga inasihi?

Kuonja chakula wakati mtu amefunga inasihi kwa sharti ahakikishe kuwa hamezi kile alichokiweka kwenye ulimi kwa ajili ya kuonja.

Je kukoga katika mchana wa Ramadhan inasihi?

Kukoga au kukosha uso ikiwa mtu yumo kwenye funga inasihi. Ila ahakikishe maji hayaingii katika matundu ya mwili. Ama yakiingia bila ya kukusudia hilo halina tatizo. Na yakiingia kwa kusudia basi atakuwa amefungua.

Ni ipi hukmu ya mwenye kufunga kutia dawa kwenye macho?
Anaruhusika kutumia na haitobatilika funga yake.

Nini hukmu ya kuchoma sindano  wakati mtu amefunga?

Ikiwa sindano  ni ya dawa tu basi haifunguzi. Ila sindano ikiwa imewekewa kitu chochote ambacho ndani yake kitampa mwenye kufunga nguvu kama glucose basi hapo itakuwa amefungua. Allah ni mjuzi zaidi.

3-KUJIZUIA NA KUJITAPISHA KWA MAKUSUDI

Pia ni wajibu kwa mwenye kufunga kujizuia na kujitapisha kwa makusudi. Ama akitapika bila ya kukusudia basi ataendelea na funga yake kama kawaida. Na akijitapisha kwa makusudi ni lazima ailipe funga hiyo. Kutoka kwa Abu Hurayrah (radhiya Allahu anhu) amesema: Amesema Mtume (Swalla Allahu alayhi wa sallam): "... na mwenye kujitapisha basi inamuwajibikia kulipa." Bukhari na Muslim.

4-KUWA MUISLAMU
Ikiwa mtu sio Muislamu basi kwake yeye haimuwajibikii kufunga. Na akija kusilimu basi hatolipa kwa zile siku ambazo hakufunga kwani alipokuwa sio Muislamu haikumuwajibikia kufunga.
Ama Muislamu ambae ataritadi wakati amefunga basi moja kwa moja funga yake itabatilika na akija kutubu na kuamua kurudi kwenye Uislamu basi inamuwajibikia kuzilipa siku zote ambazo aliziwacha wakati ametoka kwenye Uislamu.

5-KUWA NA AKILI KATIKA MCHANA MZIMA WA RAMADHAN
Pia ili swaumu isihi lazima mwenye kufunga awe na akili na ikiwa atarukwa na akili basi funga yake itabatilika. Na hakuna tatizo kwa mtu kuzimia kwa muda mchache katika mchana wa mwezi wa Ramadhan.

Usikose kusoma sehemu ya pili ya makala hii.

Thursday 26 June 2014

Duaa Anazozihitaji Muislamu Ramadhaan


 Makala kutoka alhidaaya.com

Du’aa Ya Kuona Mwezi Unaponaama [Unapoandama, miezi yote si Ramadhaan pekee]

اللهُ أَكْـبَر، اللّهُمَّ أَهِلَّـهُ عَلَيْـنا بِالأمْـنِ وَالإيمـان، والسَّلامَـةِ والإسْلامِ، وَالتَّـوْفيـقِ لِما تُحِـبُّ وَتَـرْضَـى، رَبُّنـا وَرَبُّكَ اللهُ.

Allaahu Akbar, Allaahumma Ahillahu ‘alaynaa bil-amni wal-iymaani, wassalamaati wal-Islaami, wattawfiyqi limaa Tuhibbu Rabbunaa wayardhwaa Rabbuna wa-Rabbuka-Allaah
Allaah ni Mkubwa, Ee Allaah, Uuanzishe kwetu kwa amani na imani, na usalama na Uislamu, na taufiqi ya kile Unachokipenda Mola wetu na kukiridhia, Mola  wetu na Mola wako ni Allaah

Du'aa ya kwenda Msikitini

اللّهُـمَّ اجْعَـلْ فِي قَلْبـي نُوراً ، وَفي لِسَـانِي نُوراً،   وَفِي سَمْعِي نُوراً, وَفِي بَصَرِيِ نُوراً, وَمِنْ فََوْقِي نُوراً , وَ مِنْ تَحْتِي نُوراً, وَ عَنْ يَمِينيِ نُوراَ, وعَنْ شِمَالِي نُوراً, وَمْن أَماَمِي نُوراً, وَمِنْ خَلْفيِ نُوراَ, واجْعَلْ فِي نَفْسِي نُوراً, وأَعْظِمْ لِي نُوراً, وَعظِّمْ لِي نُوراً, وَاجْعَلْ لِي نُوراً, واجْعَلنِي نُوراً, أللَّهُمَّ أَعْطِنِي نُوراً, واجْعَلْ فِي عَصَبِي نُوراً, وَفِي لَحْمِي نُوراً, وَفِي دَمِي نُوراً وَفِي شَعْرِي نُوراً, وفِي بَشَرِي نُوراً (أَللَّهُمَّ اجِعَلْ لِي نُوراً فِي قّبْرِي  وَ نُوراَ فِي عِظاَمِي) (وَزِدْنِي نُوراً, وَزِدْنِي نُوراَ , وَزِدْنِي نُوراً) (وَهَبْ لِي نُوراً عَلَى نُوراً (

Allaahumma-j-'al Fiy Qalbiy Nuuraa,  Wa fiy Lisaaniy Nuuraa  Wa fiy Sam'iy Nuuraa, Wa Fiy Baswariy Nuuraa, Wa Min Fawqiy Nuuraa, Wa Min Tahtiy Nuuraa, Wa 'An Yamiiniy Nuuraa, Wa 'An Shimaliy Nuuraa, Wa Min Amaamiy Nuuraa, Wa Min Khalfiy Nuuraa, Waj-'al Fiy Nafsiy Nuuraa, Wa A'adhwim Liy Nuuraa, Wa 'Adhwim Liy Nuuraa, Waj-'al-Liy Nuuraa, Waj-alniy Nuuraa, Allaahuumma A'atwiniy Nuuraa, Waj'al fiy 'Aswabiy Nuuraa, Wa fiy Lahmiy Nuuraa, Wa fiy Damiy Nuuraa Wa fiy Sha'ariy Nuuraa, Wa fiy Bashariy Nuuraa. Allaahumma-j'al liy Nuuran  fiy Qabriy, Wa Nuuran Fiy 'Idhaamiy,   Wazidniy Nuuraa, Wazidniy Nuuraa, Wazidniy Nuuraa, Wahab liy Nuuran 'Alaa Nuuraa.

“Ewe Mwenyezi Mungu, Weka katika moyo wangu nuru, na katika ulimi wangu nuru, na katika masikio yangu nuru, na katika macho yangu nuru, na juu yangu nuru, na chini yangu nuru, na kuliani kwangu nuru, na kushotoni kwangu nuru, na mbele yangu nuru, na nyuma yangu nuru, na Weka katika nafsi yangu nuru, na Nifanyie kubwa nuru, na Nifanyie nyingi nuru, na Uniwekee mimi nuru, na Nifanyie mimi nuru, Ewe Mwenyezi Mungu  Nipe nuru, na Uweke  katika  mishipa yangu nuru, na katika  nyama  yangu nuru, na katika damu yangu nuru, na katika nywele zangu nuru, na katika ngozi yangu nuru, (Ewe Mwenyezi Mungu  Niwekee nuru katika kaburi langu, na nuru katika mifupa yangu) (Na Unizidishie nuru, na Unizidishie nuru, na Unizidishie nuru) (na Unipe nuru juu ya nuru ) .

Du'aa ya kuingia Msikitini

أَعُوذ باللهِ العَظيـم وَبِوَجْهِـهِ الكَََرِِيـمِ وَسُلْطـانِهِ القََدِيـمِ مِنَ الشّيْـطانِ الرَّجِـيمِ،[ بِسْـمِ الله، وَالصَّلاةُ] [وَالسَّلامُ عَلى رَسولِ الله]، اللّهُـمَّ افْتَـحْ لي أَبْوابَ رَحْمَتـِكَ

A'udhu BiLLahil-'Adhwiym Wabiwaj-hihi-l-Kariym Wasul-twaanihi-l-Qadiym Mina-shaytwaanir-rajiym.  BismiLLahi Was-Swalaatu Wassalaamu 'Alaa RasuliLLah.  Allaahummaf-tah liy Abwaaba Rahmatika.
“Najilinda na Mwenyezi Mungu  Aliye Mtukufu, na kwa uso Wake, Mtakatifu, na kwa utawala Wake wa kale, kutokana na shetani aliyeepushwa na rehma za Mwenyezi Mungu, (Kwa Jina la Mwenyezi Mungu na rehma) (Na amani zimfikie Mtume wa Mwenyezi Mungu ) Ewe Mwenyezi Mungu  Nifungulie milango ya rehma Zako"

Du'aa ya kutoka Msikitini

بِسمِ الله وَالصّلاةُ وَالسّلامُ عَلَى رَسولِ الله، اللّهُـمَّ إِنّـي أَسْأَلُكَ مِـنْ فَضْـلِك، اللّهُـمَّ اَعْصِمْنـي مِنَ الشَّيْـطانِ الرَّجـيم

Bismillahi Was-Swalaatu Was-Salaamu 'Alaa RasuliLLah, Allaahumma Inniy As-aluka Min Fadhlika
Allaahumma A'aswimniy Minash-shaytaani-rajiym. 

“Kwa Jina la Mwenyezi Mungu na rehma na amani zimfikie Mtume wa  Mwenyezi Mungu, Ewe Mwenyezi Mungu  hakika mimi nakuomba katika fadhila Zako, Ewe Mwenyezi Mungu najilinda kutokana na shetani aliyeepushwa na rehma Zako (aliyelaaniwa )

Du'aa ya Qunuut ya Witr

اللّهُـمَّ اهْـدِنـي فـيمَنْ هَـدَيْـت، وَعـافِنـي فـيمَنْ عافَـيْت، وَتَوَلَّـني فـيمَنْ تَوَلَّـيْت ، وَبارِكْ لـي فـيما أَعْطَـيْت، وَقِـني شَرَّ ما قَضَـيْت، فَإِنَّـكَ تَقْـضي وَلا يُقْـضى عَلَـيْك ، إِنَّـهُ لا يَـذِلُّ مَنْ والَـيْت، [ وَلا يَعِـزُّ مَن عـادَيْت ]، تَبـارَكْـتَ رَبَّـنا وَتَعـالَـيْت.

Allaahummah-diniy fiyman Hadayta , Wa 'Aafiniy fiyman 'Aafayta, Watawallaniy fiyman Tawallayta, Wabaarik liy fiymaa A'atwayta, Waqiniy Sharra Maa Qadhwayta, Fainnaka Taqdhwiy Walaa Yuq-dhwa 'Alayka, Innahu Laa yadhillu  mawwaalayta, Walaa Ya'izzu man 'Aadayta, Tabaarakta Rabbana Wa Ta'aalayta.

“Ewe Mwenyezi Mungu  Niongoze pamoja na Uliowaongoza, na Unipe afya njema pamoja na Uliowapa afaya njema, na Nifanye kuwa ni mpenzi Wako pamoja na Uliowafanya  wapenzi na Nibariki katika Ulichonipa na Nikinge na shari ya Ulilolihukumu kwani Wewe Unahukumu wala Huhukumiwi.  Hakika hadhaliliki Uliyemfanya mpenzi (wala hatukuki Uliyemfanya adui) Umetakasika Ewe Mola wetu na Umetukuka

اللّهُـمَّ إِنِّـي أَعـوذُ بِرِضـاكَ مِنْ  سَخَطِـك، وَبِمُعـافاتِـكَ مِنْ عُقوبَـتِك، وَأَعـوذُ بِكَ مِنْـك، لا أُحْصـي ثَنـاءً عَلَـيْك، أَنْـتَ كَمـا أَثْنَـيْتَ عَلـى نَفْسـِك

Allaahumma Inniy A'udhu Biridhwaaka Min Sakhatwika, Wabimu'aafaatika min 'Uquubatika, Wa A'udhu
 Bika Minka, Laa Uhswiy Thanaan 'Alayka, Anta Kamaa Ath-nayta 'Alaa Nafsika.
“Ewe Mwenyezi Mungu  hakika mimi najilinda kwa radhi Zako kutokana na hasira Zako na kwa msamaha Wako kutokana na adhabu Yako, na najilinda  Kwako kutokana na Wewe, mimi siwezi kuzidhibiti sifa Zako, Wewe ni kama Ulivyojisifu Mwenyewe”

اللّهُـمَّ إِيّـاكَ نعْـبُدْ، وَلَـكَ نُصَلّـي وَنَسْـجُد، وَإِلَـيْكَ نَسْـعى وَنَحْـفِد، نَـرْجو رَحْمَـتَك، وَنَخْشـى عَـذابَك، إِنَّ عَـذابَكَ بالكـافرين ملْحَـق. اللّهُـمَّ إِنّا نَسْتَعـينُكَ وَنَسْتَـغْفِرُك، وَنُثْـنـي عَلَـيْك الخَـيْرَ، وَلا نَكْـفُرُك، وَنُـؤْمِنُ بِك، وَنَخْـضَعُ لَكَ وَنَخْـلَعُ مَنْ يَكْـفرُك

Allaahumma Iyyaaka Na'abud Walaka Nuswalliy Wanasjudu, Wa-Ilayka Nas'aa Wanahfidu, Narju Rahmataka, Wanakhsha 'Adhaabaka, Inna 'Adhaabaka Bil-Kaafiriyna Mulhaqq.  Allaahumma  Innaa Nasta'iynuka Wanastaghfiruka, Wanuthniy 'Alaykal-khayra, Walaa Nakfuruka, Wanu-uminu Bika, Wanakhdhwa'u Laka, Wanakhla'u Man Yakfuruka.

“Ewe Mwenyezi Mungu, Wewe tu Ndiye tunaekuabudu, na Kwako tunaswali na tunasujudu, na Kwako tunakimbilia na tunakutumikia, tunataraji rehema Yako na tunaogopa adhabu Yako, kwani adhabu Yako hakuna shaka kuwa makafiri itawifikia.  Ewe Mwenyezi Mungu  hakika sisi tunakutaka msaada na tunakutaka msamaha na tunakusifu kwa kheri na wala hatukukufurishi na tunakuamini Wewe, na tunakunyenyekea na tunamuepuka anaekukufuru”

Dua baada ya salamu katika swala ya Witri (Mwisho kabisa baada ya kumaliza Swalah yote na sio kila baada ya Rakaa mbili au nne)

سُـبْحانَ المَلِكِ القُدّوس

Subhaanal-Malikul-Qudduus

“Ametakasika Mwenyezi Mungu  Mfalme, Mtakatifu"
(mara tatu)

(Kisha unavuta kwa sauti )

 ربِّ الملائكةِ والرّوح

Rabbul-Malaaikati War-Ruuh

“Ewe Mola wa malaika na wa Jibriil”

Du'aa ya wakati wa kufungua  Swawm

ذَهَـبَ الظَّمَـأُ، وَابْتَلَّـتِ العُـروق، وَثَبَـتَ الأجْـرُ إِنْ شـاءَ اللهُ

Dhahabadh-Dhwama-u Wabtallatil-'Uruuq,, Wathabbatal-Ajru Insha-Allaah.

“Kiu kimeondoka na mishipa imelainika, na yamethibiti malipo Mwenyezi Mungu  Akipenda”

Imepokelewa kutoka kwa ‘Abdillaahi bin ‘Amr bin ‘Al -‘Aas (Radhiya Allaahu ‘anhu) amesema:

‘Amesema Mtume wa Mwenyezi Mungu  “Aliyefunga wakati wa kufuturu kwake ana Du'aa isiyorudishwa”

اللّهُـمَّ  إِنَّـي أَسْـأَلُـكَ بِرَحْمَـتِكَ الّتي وَسِـعَت كُلَّ شيء، أَنْ تَغْـفِرَ لِي

Allaahumma Inniy As-aluka Birahmatikal-latiy Wasi'at Kulla Shay'in An Taghfiraliy.

“Ewe Mwenyezi Mungu  hakika mimi nakuomba kwa rehma Zako ambazo zimeenea kila kitu, Unisamehe”

Du'aa kabla ya kula

 Atakapokula mmoja wenu chakula basi aseme:

بِسْمِ الله

Bismillahi

“Kwa jina la Mwenyezi Mungu"

Na akisahau mwanzo wake basi aseme:

بِسْمِ اللهِ في أَوَّلِهِ وَآخِـرِهِ

Bismillahi Fiy Awwalihi Wa Aakihirihi

“Kwa jina la Mwenyezi Mungu  mwanzo Wake na mwisho Wake”

Yeyote ambae Mwenyezi Mungu Amemruzuku chakula aseme:

اللّهُـمَّ بارِكْ لَنا فيهِ وَأَطْـعِمْنا خَـيْراً مِنْـهُ

Allaahumma Baarik Lana Fiyhi Wa Atw'imna Khayran minhu.

“Ewe Mwenyezi Mungu Tubariki katika chakula hichi na Tulishe bora kuliko hichi "

Na yeyote ambae Amemruzuku maziwa basi aseme:

اللّهُـمَّ بارِكْ لَنا فيهِ وَزِدْنا مِنْهُ

Allaahumma Baarik Lana Fiyhi Wazidna  Minhu

“Ewe Mwenyezi Mungu Tubarikie kinywaji hichi na Utuzidishie”

Du'aa ya baada ya kula

الْحَمْـدُ للهِ الَّذي أَطْعَمَنـي هـذا وَرَزَقَنـيهِ مِنْ غَـيْرِ حَوْلٍ مِنِّي وَلا قُوَّةٍ

Alhamduli-Llahi-lladhiy Atw'amaniy Haadhaa Warazaqaniyhi Min Ghayri Hawlim-Minniy Walaa Quwwatin.
“Sifa njema ni za Mwenyezi Mungu  Ambaye Amenilisha mimi chakula hichi na Akaniruzuku pasina uwezo wangu wala nguvu zangu”

الْحَمْـدُ للهِ حَمْـداً كَثـيراً طَيِّـباً مُبـارَكاً فيه، ]غَيْرَ مَكْفِيٍّ[ وَلا مُوَدَّعٍ وَلا مُسْتَغْـنىً عَنْـهُ رَبُّـنا

AlhamduliLLahi Hamdan Kathiyran Twayyiban Mubaarakan Fiyhi, Ghayra Mukfiyyi  Walaa Muwadda'iw- Walaa Mustaghna 'Anhu Rabbunaa.

“Sifa njema ni za Mwenyezi Mungu, sifa nyingi nzuri, zenye  baraka ndani yake, zisizo toshelezwa wala kuagwa, wala kutoshwa nazo mtu.  Ewe Mola wetu”

Du'aa ya mgeni kumuombea aliyemkaribisha chakula

اللّهُـمَّ بارِكْ لَهُمْ فيما رَزَقْـتَهُم، وَاغْفِـرْ لَهُـمْ وَارْحَمْهُمْ

Allahumma Baarik Lahum Fiyma Razaq-tahum Waghfir-lahum War-ham-hum.
 “Ewe Mwenyezi Mungu Wabariki katika Ulichowaruzuku na Uwasemehe na Uwarehemu" 

Du'aa ya kumuombea aliyekupa kinywaji au anayetaka kukupa

اللّهُـمَّ أَطْعِمْ مَن أَطْعَمَني، وَاسْقِ مَن سَقانِي

Allaahumma Atw'im Man Atw'amaniy Wasqi Man Saqaaniy.

“Ewe Mwenyezi Mungu Mlishe aliyenilisha na Mnyweshe aliyeninywesha"

Du'aa ya kumuombea uliyefuturu/futari kwake

أَفْطَـرَ عِنْدَكُم الصّـائِمونَ وَأَكَلَ طَعامَـكُمُ الأبْـرار، وَصَلَّـتْ عَلَـيْكُمُ الملائِكَـة

Aftwara 'Indakumu-Swaaimuna Wa Akala Twa'aamakumul-Abraar, Waswallat 'Alyakumul-Malaaikah.

 “Wafuturu kwenu waliofunga na wale chakula chenu watu wema, na wawaombee rehema malaika”

Du'aa ya aliyealikwa chakula lakini akawa amefunga

Akialikwa mmoja wenu aitike mwito, akiwa amefunga basi awaombee Du'aa na kama hakufunga basi ale

Anachosema aliyetukanwa hali ya kuwa amefunga

إنِّي صَائِمٌ ,  إنِّي صَائِمٌ”

Inniy Swaaimun Inniy Swaaimun

“Hakika mimi nimefunga, hakika mimi nimefunga" 

Wednesday 18 June 2014

WANAOWAJIBIKA KUFUNGA, WALIORUHUSIWA WASIFUNGE NA WENYE KURUHUSIWA KULA NA KUFIDIYA


Makala kutoka Raudhwah Islamic Group

Kila sifa njema zinamstahikia Allah Mola wa viumbe vyote. Swala na salamu zimuendee Mtume wetu Muhammad (swalla Allahu alaihi wa sallam) na ahli zake na maswahaba.

MAKALA HIZI ZIMEKUSANYA HUKUMU ZILIZOKUWA LAZIMA KUZIJUA KWA KILA MFUNGAJI WA MWEZI WA RAMADHANI, ILI MFUNGAJI AWE NA UJUZI KAMILI KATIKA KUTEKELEZA IBADA HII TUKUFU YA SWAUMU YA MWEZI WA RAMADHANI. KWA HIVYO NDUGU MUISLAMU, TUJIITAHIDI SANA KUZISOMA MAKALA HIZI KWA MAKINI SANA NA UYAELEWE YALIYOMO. NAOMBA MWENYEZI MUNGU ATUFANYIE WEPESI KATIKA KUZIJUA HUKUMU ZA KUFUNGA NA FADHILA ZA RAMADHAN.

Baada ya utangulizi huo,

Ndugu Waislam, Ni katika baraka zake Allaah (Subhaanahu wa Ta’ala) kwa Muislamu Kumuwezesha kufunga mwezi wa Ramadhani na kuutumia wakati wake wa usiku kwa Swalah. Ni mwezi ambao ndani yake amali njema huzidishwa malipo na watu hupandishwa daraja (vyeo). Ni wakati ambao Allaah (Subhaanahu wa Ta’ala) huwaachia huru baadhi ya watu kutokana na Moto. Kwa hivyo Muislamu ni lazima ajitahidi sana kufanya mambo mema katika mwezi huu; ni lazima afanye hima katika kuutumia wakati wa uhai wake kwenye ibada. Kuna watu wangapi ambao wamenyimika katika mwezi huu kutokana na maradhi, mauti au kukosa maelekezo mema.
Ndugu waislamu, Allah (Subhaanahu wa Ta’ala) ametufaradhishia kufunga swaum ya Ramadhan kama iliyokuja katika qur-an tukufu "Enyi mlio amini! Mmeandikiwa Saumu, kama waliyo andikiwa walio kuwa kabla yenu ili mpate kuchamngu”. (Al Baqara : 183).

Pia Allah (Subhaanahu wa Ta’ala) anaendelea kusema "..... Basi ataye kuwa mjini katika mwezi huu naafunge.....”(Al Baqara : 185).
Wakati tunapojiandaa na kuianza Ramadhani, tunapaswa kujua kwamba, amri ya kufunga ni yake Mwenyezi Mungu. Na wala amri hii haikuwa ya yeyote yule kati ya viumbe,hivyo basi ni vyema kujua masharti ambayo ukiyakamilisha itakua ni wajibu kwako kufunga
Na masharti yafuatayo ukiwa umeyakamilisha utalazimika kuanza Saumu, na wala hutokuwa na udhuru wowote ukuzuiao kufunga.

I. AL-ISLAM: Uislamu ni shuruti moja katika shuruti za kukubaliwa Saumu na ibada zote. Ijapokuwa juu ya kafiri pia ni wajibu kufunga na kufanya ibada zote, lakini kwa vile yeye si Mwislamu basi haitasihi na kukubaliwa ibada zake.

II. BALEGHE: Mtu huhesabika kuwa amebaleghe kwa kutimiza miaka kumi na mitano, au akiwa mwanamke aliyewahi kutokwa na damu ya mwezi. Pia ikiwa amewahi kuota kama anatangamana na mke (akiwa mume) au na mume (akiwa mke) na kutokwa na manii kwa ndoto hiyo, basi atalazimika kuanza kufunga.

III. AKILI: Funga ya mwezi mtukufu wa Ramadhani haiwajibiki kwa mtu asiyekuwa na akili mfano Kichaa,kama zilivyo ibada nyingine.

Pia katika vitabu vyengine wameeleza sharti nyengine ikiwemo kuepukana na hedhi, kuwa mkaazi (msafiri anaruhusiwa kutokufunga kama tutakavyoieleza hapo baadae) na pia kuweza kufunga. (Kuna watu wana maradhi sugu hawawezi kufunga au uzee hawa kwao haiwajibikii kufunga. Ila tutaeleza nini wakifanye watu hawa.

Kama tulivyosema awali,kila muislamu aliye baleghe na mwenywe akili timamu lazima afunge Ramadhani.Wanaosameheka ni watu wa namna hii
a) Wanawake wenye hedhi au nifas
b) Wagonjwa na wasafir

WANAWAKE WENYE HEDHI AU NIFAS

• Wanawake wanapokuwa katika siku zao za miezi au katika damu ya uzazi ni haramu kwao kufunga.

• Ramadhani ikianza na yeye yumo katika hedhi au nifasi hatofunga mpaka atakapomaliza na kuoga na kuwa tohara.

• Damu ikitoka katika swaumu hapo,mwanamke lazima avunje swaumu,hata kama bado muda mchache wa kuzama kwa jua.

• Damu ikimalizika usiku,anaweza kutia nia ya kufuga bila ya kupoteza wakati kwa kujitoharisha lakini iwe kabla ya kuchomoza alfajiri ya kweli.

• Mwanamke mwenye damu humbidi azifunge siku alizowacha .Bi Aisha radhi za Allah ziwe juu yake amesema” Katika kipindi cha Mtume tuliamrishwa kuzilipa siku tulizowacha kwa sababu ya kutokwa na damu wala hatukuamrishwa tuzilipe sala tano”

• Mwanamke mjamzito au mwenye kunyonyesha wameruhusiwa kutofunga kwa kuja kuzilipa. Anas bin Malik (radhi za Allah ziwe juu yake) anasimulia hadithi kutoka kwa Mtume (swalla Allahu alayhi wasallam)

"إن الله وضع عن المسافر شطر الصلاة ووضع عن المسافر والحبلي والمرضع الصوم أو الصيام"
“Mwenyezi Mungu kampunguzia msafiri sala na kampunguzia msafiri na mwenye mimba pamoja na mwanamke mnyonyeshaji saumu” (muslim)

TANBIH
Mwanamke mjamzito au anayenyonyesha ambae atakuwa anaikhofia nafsi yake huyu atalipa tuu hatatoa fidia,lau ikiwa anakhofia nafsi yake pamoja na kiumbe kilichokuwa tumboni atalipa na kutoa fidia

MGONJWA NA MSAFIRI

• Kwa huruma zake mola,mgonjwa na msafiri wameamrishwa wasifunge ila waje kuzilipa funga zilizowapita “………..Na aliyekuwa mgonjwa au msafiri basi atomize hesabu siku nyengine…..”(Baqarah:184)

• Qur-an haikutaja ugonjwa maalumu wala kuelezea namna ya ugonjwa,ila baadhi ya wanzuoni wamesema ugonjwa utakaomkalifisha asiweze kufunga.

• Safari iliyoruhusiwa kufungua ni ilie safari ambayo inaruhusa ya kufupisha sala na kusali safari.

Mtu anaweza kufuturu au kuendelea kufunga anapokua katika safari kwa kauli ya Anas bin Malik (radhi za Allah ziwe juu yake) amesema” Tulikuwa tunasfiri pamoja na Mtume (swalla Allahu alayhi wasallam) ,Hakupata kuwalaumu hata mara moja wale waliokua wakifunga au wale ambao hawakufunga”

Vile vile bwana Hamza Al-Aslami alimwambia Mtume (swalla Allahu alayhi wasallam) “Yaa Rasulla allah mimi najiona ninazo nguvu za kufunga huku nimo safarini Je! Kuna ubaya wowote” Mtume alimjibu << Hii ni ruhusa kutoka kwa Mwenyezi Mungu atakayeitumia ni bora ,Ama yule apendaye kufunga hana ubaya wowote ule>> “ (Muslim)

• Na safari, sharti iwe ya halali, isiwe kazi yake kama kondakta, dreva nahodha n.k. asiwe atakaa huko zaidi ya siku 10 akiwa atakaa zaidi ya siku 10 atafunga hata huko huko safarini.

WENYE KURUHUSIWA KULA NA KUFIDIYA

Uislamu ni Dini ipendayo kusahilisha mambo kwa wale wasioweza kuyatenda,kwa hiyo watu wafuatao wamepewa ruhusaya kula na kutoa fidia kwa kulisha kila siku chakula {kibaba (sawa na kilo kasorobo) kwa kila siku. Kibaba hiki kiwe ni cha chakula kitumiwacho sana na watu wa sehemu hiyo }cha wastani cha mtu futari,hapa inategemea hali ya huyo mlishaji ikiwa yeye mwenye hana uwezo huwa amesamehewa..Watu wenyewe ni
a) Mzee mtu mzima sana hawezi kufunga ila kwa shida sana
b) Mgonjwa asiyekuwa na tamaa ya kupona maradhi yake
c) Mwanamke mwenye kunyonyesha au mja mzito mwenye kuogopea kile kizazi

HITIMISHO

NDUGU ZANGU KATIKA IMAN,FUNGA YA RAMADHANI NI FARADHI NA NI LAZIMA KWETU KUFUNGA,INASIKITISHA KUWAONA BAADHI YA WAISLAMU KUWA HAWAFUNGI,ABU HURAIRA (RADHI ZA ALLAH ZIWE JUU YAKE) AMEPOKEA KWA MTUME (SWALLA ALLAHU ALAYHI WASALLAM) “ MWENYE KUFUNGUA SIKU MOJA KATIKA RAMADHANI BILA YA UDHURU WENYE KUKUBALIWA KISHERIA,MTU HUYO HATAWEZA KUIFIDA KWA KITU HATA KAMA ATAFUNGA MILELE”(BUKHARIY)

PIA WAMEKUBALIANA WANAZUONI KUWA MTU ASIYEFUNGIA RAMADHANI NA AKAACHA KUIFUNGA BILA YA SABABU HUWA MBAYA ZAIDI KULIKO MZINZI NA MLEVI.

HIVYO SHIME WAISLAMU TUFUNGE MWEZI WA RAMADHANI KWA AJILI YA ALLAH ILI TUWEZE KUPATA UJIRA MKUBWA. ALLAHU A’ALAM.

Tuesday 17 June 2014

FUNGA NA AINA ZAKE


Makala kutoka Raudhwah Islamic Group

                Sifa zote njema zinamstahikia Allah Subhaanahu Wa Taala muumba mbingu na ardhi bila ya vizuizi, Swala na Salaamu zimshukie kipenzi cha Umma huu ulio bora Mtume Muhammad Swalla Allahu Alayhi Wa Sallam, pamoja na ahli zake na Swahaba zake na wote waliowema hadi siku ya malipo.

                Ndugu yangu katika Imani leo napenda kukuletea makala hii muhimu kwa waislamu, kwani sote tunatambua ya kwamba tumekabiliwa na mwezi mtukufu mno na wenye fadhila nyingi kwa waislamu katika maisha ya duniani na kesho Akhera. Kwa maana hiyo tumeonelea tukumbushane yaliyo bora zaidi mbele ya Allah ili tupate kuwa waja wema na anaowapenda Allah Subhaanahu Wa Taala, Kwani Allah mwenyewe ametuhimiza tuyakimbilie mambo mazuri katika kuyatenda ili tupate kuingizwa katika fungu la WachaMungu. Anasema Allah Subhaanahu Wa Taala Katika kuyatilia Mkazo hayo : “Na yaendeeni upesi upesi maghfira ya mola wenu na Pepo yake ambayo upana wake tu ni sawa na mbingu na ardhi, Pepo iliyowekewa kwa wamchao Allah.”   (AL-IMRAN : 133).

                Ndugu yangu katika Imani, Mada tutakayoizungumzia leo ni kuhusu Funga.

MAANA YA FUNGA

               Funga Kilugha ni kile kitendo cha kujizuilia na kitu chochote. Kwa maana hiyo tunapata mafunzo kwamba unaweza ukajizuilia na kitendo chochote kile kama kusema au kuzungumza au kula kwa muda wowote uliojiwekea na ukasema nimefunga. Allah Subhaanahu wa Taala anatupa mfano wa hayo katika Qur-an Tukufu pale alipomzungumzia Bibi Maryam wakati alipomzaa Nabii Issa Alayhi Salaam, alipoulizwa na jamaa zake kuhusu mtoto yule amempata wapi ? Bibi Maryam akajibu kwa kuashiria : “Hakika mimi nimeweka nadhiri ya kufunga kwa Allah mwingi wa Rehma, basi sitozungumza na mtu yeyote kwa siku ya leo.”  (MARYAM : 26).  Kwa hiyo inawezekana ukanuia kufunga kwa kutofanya kitendo chochote kile ulichodhamiria. Kama hapa bibi Maryam amesema kufunga kwa maana ya kujizuia na kuzungumza. 
          
              Funga Kisheria ni kujizuilia kula, kunywa na mambo yote yenye kufunguza mchana kutwa, kuanzia alfajiri ya kweli mpaka kuzama kwa jua. Kwa uthibitisho wa hayo ni pale Allah Subhaanahu Wa Taala aliposema katika Qur-an yake Tukufu : “Na kuleni na kunyweni mpaka kubainike kwenu weupe wa alfajiri katika weusi wa usiku, Kisha timizeni saumu mpaka usiku.”  (BAQARA : 187).

              Maneno hayo matukufu yanabainisha nyakati za kujizuia huko ni kuanzia alfajiri ya kweli hadi kuzama kwa jua yaani kuanza kuingia kwa usiku.

HIKMA YA FUNGA

             Miongoni mwa hikma za Funga ni kama ambavyo wanazuoni walivotufahamisha, ni kuizoesha nafsi kuwa na subra kwani jambo la kufunga linahitaji subira ya kweli kweli. Hikma nyengine ni kujua thamani ya neema za Allah Subhaanahu Wa Taala, Huwezi  kujua neema ya chakula, kinywaji, au kukutana na mke wako mpaka zitakapokuondokea neema hizo au kuzuiliwa. Mfano asiyejua njaa basi atajua njaa inakuwaje kwa kufunga, na atajua thamani ya vyakula hivyo. Hikma nyengine ni kumpiga    Shetani na kumbana kwani binaadamu anaposhiba na vyakula vikajenga mwili wake, ndipo anapokaribia katika mwili wake na kumfanya ayaendee maasi mbali mbali. Pia Funga humfanya mwanadamu kuwa na afya iliyo njema, Kwa maneno ya Mtume Swalla Allahu Alayhi Wa Sallam aliposema :”Fungeni mupate afya njema.”

AINA ZA FUNGA

                Funga zipo za aina mbili nazo ni Funga za Fardhi (Lazima) na Funga za Sunna (zisizo za Lazima).
1)FUNGA ZA SUNNAH

                Funga za Sunna ni zile Funga zote zisizokuwa na ulazima kwa muislamu kuzitekeleza. Kwa maana hiyo muislamu yeyote atakae zitekeleza atapata ujira wake maalumu uliowekwa na Allah Subhaanahu wa Taala, na vile vile muislamu yeyote asipozitekeleza hatopata ujira wala dhambi. Mfano wa Funga hizo za Sunna ni kama Funga za Jumatatu na Alhamisi ambazo Mtume wetu Muhammad Swalla Allahu Alayhi Wa Sallam alikuwa akizitekeleza.  Mfano mwengine ni Funga ya Arafa, Funga ya Ashuraa, Funga za masiku meupe na kadhalika.

2)FUNGA ZA FARDHI.

Funga za Fardhi ni funga zote zilizokuwa za lazima kwa muislamu kuzitekeleza. Kwa maana hii muislamu yeyote atakae zitekeleza atapata ujira uliowekwa na Allah Subhaanahu Wa Taala, kinyume chake kwa muislamu yeyote atakaeziwacha asizitekeleze na hali ya kuwa zinamuwajibikia atapata dhambi na khasara kubwa mbele ya Allah Subhaanahu Wa Taala.

                  Funga za Fardhi zimegawika sehemu tatu, nazo ni :-

a)Funga ya Ramadhani.
b)Funga ya Kafara.
c)Funga ya Nadhiri.

               Ramadhani ni mwezi miongoni mwa miezi kumi na mbili katika mwaka wa Hijriya, ndani ya mwezi huu kuna funga za lazima kwa kila muislam aliyewajibikiwa kufunga kwa takribani siku ishirini na tisa kwa muandamo wa mwezi, ama siku thalathini kwa kukamilisha. Kwa uthibitisho wa hayo ni pale Allah Subhaanahu Wa Taala aliposema : “Enyi mlioamini, mumefaradhishiwa kufunga kama walivyo faradhishiwa waliopita kabla yenu.”  “Ni masiku machache tu ya kuhesabika ………..” (BAQRA :   ).

Kwa hivyo kila muislamu aliyebaleghe, mwenye akili timamu, mwenye afya njema na mkaazi (mwenyeji katika mji ) ni lazima kwake kufunga katika mwezi mtukufu wa Ramadhani.

               Yaani Funga haisihi kwa kafiri, na sio lazima kwa mtoto mdogo aliyekuwa hajafikia baleghe, na sio lazima kwa asiyejiweza au mgonjwa na vile vile sio lazima kwa msafiri wakati wa safari yake ya halali iliyofikia masafa ya kupunguza sala (Marhalatain).

               Tumuombe Allah Subhaanahu Wa Taala atufikishe katika mwezi mtukufu wa Ramadhani na atuwafikishe kuitekeleza ibada hiyo kwa salama na afya njema, na atujaaliye tuwe miongoni mwa watakaofikia lengo la funga.

               Waswalla Allahu alaa sayyidna Muhammad wa Alaa Aalihi Waswahbihi Wasallam, Walhamdulillahi Rabbil Aalamiin.

Sunday 15 June 2014

HISTORIA YA FUNGA,AINA ZA FUNGA NA TOFAUTI ZA NIA ZA FUNGA ZA FARADHI NA FUNGA ZA SUNNA


Makala kutoka Raudhwah Islamic Group

             Kila sifa njema zinamstahikia Allah Mola wa viumbe vyote. Sala na salamu zimuendee Mtume wetu Muhammad (swalla Allahu alaihi wa sallam) na ahli zake na maswahaba wake.

            Makala yetu itazungumzia  Historia ya Funga,aina za funga na tofauti ya nia za funga za faradhi na funga za sunna.

            Kwanza kabisa tukiangalia neno Funga lina maana kilugha ni kujizuilia na chochote. Kujizuilia huku inawezana ikawa kujizuilia na kupigana, kutozungumza au kutofanya  kitu chengine  chochote. Ama kisheria ni kujizuilia na vyenye kufunguza kuanzia kuchomoza kwa alfajiri ya kweli hadi kuzama kwa jua kwa nia maalum.

              Funga imefaradhishwa katika mwaka wa pili wa hijra yaani tokea kuhama kwa Mtume Swalla Allahu Alayhi wa Sallam Makka kuelekea madina, wakati walipokuwepo huko Madina ndipo ilipofaradhiswa funga,na wakati huo ilikuwa katika mwezi wa shaaban. Mwezi wa Ramadhani ni mwezi wa tisa katika miezi ya hijriyyah na ndio mwezi uliobora kulilko miezi mengine yote kwa sababu mwezi huu umekusanya kila aina ya kheri na neema za Allah Subhaanahu Wataala na ndio maana Mtume Muhammad Swalla Allahu Alayhi Wa Sallam akasema katika kusisitiza ibada katika mwezi huu : “ameangamia yule ambae ataudiriki mwezi wa Ramadhani wote na asisamehewe madhambi yake.” Maneno hayo ya Mtume Swala Allahu Alayhi Wa Sallam yanaonesha wazi kuwa mwezi huu ni mwezi mtukufu kuliko miezi mengine.

             Umeitwa mwezi wa Ramadhani kwa sababu kuna kauli inasema, “zama walipokuwa wanawake waarabu katika siku za joto kali, wakauita mwezi huu jina hilo la Ramadhani kwa kauli yao mina RAMDHWAI yaani ni joto kali. Vile vile kuna kauli nyengine inasema umeitwa Ramadhani kwa sababu unaunguza madhambi, (maneno haya utayapata katika kitabu cha Takriratu-ssadidah fii masailil-Mufiidah, Ukurasa wa 433).

               Asili ya Funga tunaipata pale Allah Subhaanahu Wataala Aliposema katika kitabu chake kitukufu : “Enyi mlioamini, Mmefaradhishiwa kufunga kama walivofaradhishiwa waliopita kabla yenu, Ili mupate kumcha Mungu.” (Baqara : 183).  Maneno haya matukufu yanatuonesha wazi kuwa Funga ni Ibada ambayo ilikuwepo katika nyumati nyingi zilizopita kabla yetu, kwa maana ummati huu wa Mtume Muhammad Swalla Allahu Alayhi wa Sallam hatujaletewa jambo geni katika dini yetu ya uislamu isipokuwa mitume iliyopita pamoja na watu wao walifaradhishiwa pia kufunga na wakatekeleza. Kwa mfano historia inatwambia pale ambapo Nabii Mussa na watu wake walipookolewa na Allah kutokana na Firauni alolaaniwa, alitoka Nabii Mussa Alayhi Salaam kwenda kwenye jabali kuzungumza na mola wake na huko Nabii Mussa Alayhi Salaam alifunga siku Arubaini (40). Kwa hiyo asili ya Funga inatoka katika nyumati zilizopita kabla ya Ummati wetu huu.

                 Funga imegawika katika Makundi mawili makuu, nayo ni :-
1)WAJIBU : Yaani ni lazima kuzifunga, na hapa zipo aina sita, nazo ni :-
a)Funga ya Ramadhani.
b)Funga ya kulipa.
c)Funga ya Nadhiri.
d)Funga ya Hajji na Umra badala ya kuchinja.
e)Funga ya  kuomba mvua anapoamrisha kadhi.
f)Funga ya kafara.
2)SUNNAH : Yaani ni hiyari kuitekeleza, Na hii imegawika sehemu tatu, nazo ni :-
a)Zinazokuja kwa kila mwaka.
b)Zinazokuja kwa kila mwezi.
c)Zinazokuja kwa kila wiki.
3)MAKRUH : Yaani kuchukiza, na hii ipo sehemu moja nayo ni kufunga siku ya ijumaa peke yake.
4)HARAMU : yaani ni makosa kuitekeleza, Na hii imegawika sehemu mbili, nazo ni :-
a)Haramu pamoja na kusihi Funga hiyo.
b)Haramu pamoja na kutokusihi funga hiyo.
Sehemu ya pili katika haramu inagawika sehemu tano, nazo ni :-
1)Kufunga siku ya Eid-el-Fitri.
2)Kufunga siku ya Eid-el-Hajj au Eid-el-Adhha.
3)Kufunga siku ya kushiriki yaani (Ayyamu Tashrik).
4)Kufunga nusu ya pili katika mwezi wa Shaabaan.
5)Kufunga siku ya shakka yaani (yaumu shakka).
                
               Tumalizie makala yetu hii kwa kuangalia tafauti za nia za Faradhi na nia za Sunnah, kwa sababu amali yoyote ni lazima kuwe na nia ndani yake, kama alivosema Mtume Swalla Allahu Alayhi wa Sallam : “Hakika kila amali ina nia yake, na hakika kila mtu na anavyonuia,………” (BUKHARY NA MUSLIM).    Kwa hiyo na funga nayo ina nia zake kama amali nyengine zote.

TOFAUTI ZA NIA ZA FUNGA ZA FARADHI NA FUNGA ZA SUNNAH

1- NIA YA FUNGA YA FARADHI :Unaingia wakati wake tokea kuzama kwa jua mpaka kchomoza kwa alfajiri, inalazimika uitie usiku. NIA YA FUNGA YA SUNNA Unaingia wakati wake tokea kuzama kwa jua mpaka kupindukia kwa jua (yaani kuingia kwa wakati wa Adhuhuri), na sio lazima uitie usiku.

  2. NIA YA FUNGA YA FARADHI : Ni lazima uibainishe kama ni ya Ramadhani au ya Nadhiri n.k. NIA YA FUNGA YA SUNNA Sio lazima kuibainisha isipokuwa Funga yenye wakati maalumu kama Arafa kwa makubaliano ya wanavyuoni.

3.  NIA YA FUNGA YA FARADHI Haifai kuzikusanya Faradhi mbili kwa pamoja katika siku moja au kwa nia moja. NIA YA FUNGA YA SUNNA Inafaa kukusanya Sunna mbili na zaidi katika siku moja au kwa nia moja.
               Haya yote utayapata katika kitabu cha (TAKRIRATU SSADIDAH FII MASAILIL MUFIIDAH) Ukurasa wa 440.
              Bila shaka mambo ya kuyazungumza katika mwezi huu wa Ramadhani ni mengi sana na wala hatutayamaliza, ila kwa haya machache na mengine utakayoyapata katika makala nyengine tumuombe Allah Subhaanahu wa Taala atuwafikishe kuyatekeleza ili tufikie ujira wa wamchao Allah.

Makala imeandaliwa na Raudhwah Islamic Group

Saturday 14 June 2014

NI UPI MOTO WA ALLAH-SEHEMU YA PILI

Makala kutoka Raudhwah Islamic Group

AINA ZA ADHABU NDANI YA MOTO

Baada ya kutoka hukmu ya kila mmoja, watu wa motoni wataingizwa sehemu zao na kila mtu na namna yake ya kuingizwa. Allah ameeleza vipi wataingizwa watu wa motoni katika makaazi yao hayo. Wako watakaofungwa na minyororo na kutupwa jahannam, kama anavyosema katika suratul-Haaqah 30-32“Mkamateni na mfungeni. Kisha mtupeni motoni. Tena katika mnyororo wenye urefu wa dhiraa sabiini”. Na wako watakaokokotwa kifudifudi mpaka Jahannam,kama anavyosema Allah katika suratul-Qamar aya ya 48 “Siku watakayokokotwa kifudifudi (huku wakiambiwa)onjeni mguso wa jahannam”

.Na wako watakaochukuliwa kwa nywele za utosi na nyayo zao kama anavosema Allah katika suratul-Rahman aya ya 41 “Watajulikana waovu kwa alama zao,basi watakamatwa kwa nywele zao za utosi na nyayo zao (watumbukizwe jahannam)”.

Na humo ndani ya jahannam watakutana na adhabu mbalimbali, ikiwemo kupigwa marungu ya chuma ya moto amesema Allah “Na kwa ajili yao (yatakuwepo)marungu ya chuma”(Hajj: 21). Pia wapo watakaobabuliwa nyuso zao na moto, kama anavyosema Allah katika suratul-muuminuun aya ya 104 na Maarij 16. Na Allah anasema kua kila zinapoungua ngozi zao tutawabadilishia ngozi nyengine badala ya zile ili wapate kuwonja adhabu.(Nisai : 56). Pia ndani ya jahannam kuna nyoka ambae akimgonga mtu basi machungu yake hayamalizki muda wa miaka 40.(hadith hasan imepokelewa na Imam Ahmad).

Adhabu za jahannam ni nyingi, na ni adhabu juu ya adhabu, kiasi kwamba watu wake watatamani kufa, na watanadi kumwambia mshika funguo za Moto Maalik “Ewe Maalik na atufishe Mola wako (tumalizane na hii adhabu).watajibiwa bila shaka mtaka humohumo” (Zukhruf 77).

Na katika aya nyengine wataambiwa nyamazeni na wala msizungumze nami . Na katika hadith sahihi inayosimuliwa na Abdullah bin Qays kua “Watalia watu wa jahannam mpaka machozi yao yataisha, na baadae ianze kutoka damu kiasi kwamba lau kama italetwa jahazi basi itatembea juu ya damu hiyo.” Subhanallah hakuna anaeweza kustahmili adhabu za jahannam ata kwa sekunde moja.Mtu mwenye adhabu ya chini katika jahannam ,kama hadith ilokuwemo katika Riyadhu-Swalihin walowafikiana bukhari na Muslim kua adhabu yake ni kua ataekewa vijiwe vya moto chini ya viatu vyake na utatokota ubongo kutokana na joto la moto wa chini ya viatu” basi ni vipi kwa adhabu ya juu? Na ni vipi kwa wale wanafik watakaokua katika daraja ya chini ya moto? (Allah atuhifadhi) .

CHAKULA CHA WATU WA MOTONI

Vyakula vyao vimetajwa kua ni:
1-Dhari’i: Hii ni miba ichomayo koo na imetajwa katika Suratul Ghaashiyah aya ya 6.

2-Ghisliin: Amesema Allah kuhusiana na Ghisliin “ Hawatokua na chakula humo ila Usaha”. Suratu Haaqah aya ya 36. Hivyo ghisliin ni usaha ambao utawatoka wenyewe watu wa motoni kutokana na adhabu kali na kisha watakula usaha wao huo.

3-Zaquum: Ni mti mchungu huu ambao unaota katika jahannam, umoto wake umefananishwa na shaba iloyayushwa ambayo itachemkia tumboni. Matunda yake yanatisha kama vichwa vya mashetani. Umetajwa katika suratu-Dukhaan aya ya 43-45 na Suratu Swaaffaat aya 62-66 na suratul_waaqiah 52-53.

4-Ghuswah: Ni aina nyengine ya chakula cha watu wa motoni. Allah amekitaja katika suratul-Muzammil “Na chakula kikwamacho na adhabu iumizayo” 13.

D :VINYWAJI VYA WATU WA MOTONI

Kabla ya kutaja vinywaji vya watu wa motoni, tukumbuke kua baada ya watu wa motoni kuingizwa jahannam watashikwa na kiu kali kutokana na joto la jahannam, hivyo watawapigia kelele watu wa peponi na kuwaambia kama anavyotusimulia Allah “Watu wa motoni watawanadia watu wa peponi: Tumiminieni maji au kile alichokuruzukuni Allah watasema (watu wa peponi kuwajibu):Hakika Allah ameviharamisha kwa kwa makafiri. Ambao waliifanya dini yao kua ni upuuzi na mchezo,na yakawadanganya maisha ya dunia. Basi leo tutawasahau (na kuwaacha humohumo motoni)kama walivyosahau mkutano wa siku hii” (Aaraf). Baada ya joto la jahannam kuzidi wataoneshwa maji yachemkayo, kisha watayaendea lakini hawatoweza kunywa kwa umoto wake, watataka kurudi tena mahali walipokua na wakirudi, watazidiwa na kiu watataka kwenda kwenye yale maji na huo ndo utakua mzunguko wao. Amesema Allah katika suratu Rahman 44 “Watakua wakizunguka baina ya (Jahannam)na baina ya maji ya moto yachemkayo”. Amesema Allah kuhusiana na maji hayo katika suratu-Muhammad 15“……na kunyweshwa maji yachemkayo yatakayokata chango zao” 15 na wapo ambao maji hayo yatatoa ngozi zao na yalokuwemo kwenye matumbo yao kama anavyosema Allah katika suratul-hajj.
Ama vinywaji vyengine ni:

1- Maji ya usaha. Amesema Allah katika suratu –Ibrahiim aya ya 16-17“ Na atanyeshwa humo maji ya usaha. Awe anayagugumiza na asiweze kuyameza. Na mauti yatamjia kutoka kila mahali na hatokufa”. 16-17.

2- Maji ya shaba. Amesema Allah kuhusiana na maji haya katka suratul-Kahfi “ Na watakapoomba msaada (kutokana na kiu kali)watapewa maji kama ya shaba iliyoyayushwa itakayounguza nyuso zao, kinywaji kibaya kilioje hicho”

Ama kwa upande wa hadithi: Inasimuliwa kua watu wa jahannam wakiyasogelea maji kwa ajili ya kuyanywa basi itatoka ngozi ya uso na kuingia katika chombo chenye maji yale kutokana na shida ya vuke la moto.

MAVAZI YA WATU WA MOTONI

Motoni watu watavishwa Qatirani, nazo ni nguo za Lami. Amesema Allah katka Suratu-Ibrahiim aya ya 50 “Nguo zao zitakua ni lami,na moto utazijia nyuso zao (uzibabue)”. Na maana nyengine ya Qatirani ni shaba iloyounguzwa mpaka ikapiga wekundu.

ADHABU NYENGINEZO ZA WATU WA MOTONI

1- Kutomuona Allah: Watu wa motoni hawatomuoni muumba wao, Kwani Allah ni nuru na nuru yake haionekani na waovu. Amesema Allah katika suratu-Mutaffin “Sivyo hivyo,siku hiyo kwa Mola wao watazuiwa (kumuona). Kama ilivyokua watu wema moja ya starehe zao ni Kumuona Allah basi na watu wa motoni moja ya adhabu yao ni kutomuona Allah.

2- Kuishi Milele: Kama tulivyoona katika makala kuhusu pepo ya Allah, kua baada ya watu kuingia sehemu zao stahiki, yataletwa mauti kwa sura ya kondoo na kuchinjwa kuonesha kua hakuna kufa katika jahannam,na inatosha adhabu kua adhabu kwa kitendo chake kua ni milele. Amesema Allah “Kisha hatokufa humo wala kuwa hai” A’laa 13. Basi itakua ni majuto kwa watu wa jahannam kwani wajua hawatoki tena.

UTANABAHISHO

Ili Mja aweze kuepukana na jahannam, ni lazima mezani yake ya mema izidi ya maovu. Kila binaadamu ni mkosa, lakini mbora wa wakosaji ni yule anaetubia. Ni muhimu kuzidisha kuleta istighfaar hasa katika mwezi wa Ramadhan, ili tukienda kwa Allah iwe tumesamehewa. Allah anasamehe makosa yote madamu yataletewa toba yake ya kweli kabla ya roho kufika shingoni na jua kuchomoza magharibi, na kuna makosa baada ya kufa Allah hayatoyasamehe na adhabu yake ni kali. Pia makosa ambayo Mtume ameyataja kua ni yenye kuporomosha amali haya ni makosa yaloandaliwa adhabu kali na moja wapo ni Kumshirikisha Allah. Amesema Allah katika suratul Maidah 72 “…hakika atakaemshirikisha Allah basi Allah amemharamishia pepo, na makaazi yake ni motoni..”

Jengine ni Kuua, amesema Allah katika suratu Nisai 93 “Na mwenye kumuua muislamu kwa kukusudia, basi malipo yake ni jahannam,atakaa humo milele,na Allah amemghadhibikia na amemlaani na amaemwandalia adhabu kali”

Jengine ni Kula mali ya yatima, Amesema Allah “Hakika wale wanaokula mali ya mayatima kwa dhulma bila shaka wanakula moto matumboni mwao na wataingia katika moto uwakao”.

Amesema Mtume swalla Allahu alayhi wasalam mambo yatakayowaingiza watu kwa wingi jahannam ni ulimi na utupu na katika hadith nyengine akasema atakaenidhamini kinyama kilochokuwepo baina ya taya zake mbili (yani ulimi)na kinyama kilichoko baina ya mapaja yake mawili (yani utupu)basi nami namdhamnini Jannah (Hadith sahih). Hivyo ili mtu aepukane na jahannam basi na achunge matamanio ya ulimi wake na utupu wake.

Ama madhambi mengine amesema Mtume wa Allah “ Makundi mawili sikuyaonapo,nayo ni makundi ya motoni,akayataja kua ni wanawake wanaotembea uchi,na vichwa vyao vimekaa kama nundu za ngamia. Akimaanisha wanawake wanaojisuka wakanyanyua nywele zao na wakatia wanayoyatia ili ifanyike nundu, hili ni kundi la motoni na tunaomba madada zetu na mama zetu wa kiislamu wakifanya haya. Je hawaijui hii hadithi au ni kumuendekeza sheitwaan na nafsi zao?
Na pia Mtume swalla Allahu alayhi wasalam amesema”Ameoneshwa moto na akawakuta wengi wao walokuwemo humo ni wanawake..”hivyo akawataka wazidishe kutoa sadaka.

Ili mtu aepukane na jahaanam ni muhimu kuzidisha amali zifuatazo:
Kuzidisha kutoa sadaka kwani amesema Mtume wa Allah “Sadaka huondoa makosa kama moto unavokula kuni.(Hadith sahih).
Kuzidisha Kufunga funga za Sunnah : Amesema Mtume wa Allah katka hadith “Atakaefunga siku moja kwa ajili ya Allah basi Allah atamueka mbali na jahannam umbali wa mwendo wa miaka 70.(Bukhari).

Kulia kwa ajili ya Allah kwani amesema Mtume rehma na amani ziwe juu yake “Jicho lenye kulia kwa ajili ya Allah halitogusa jahannam mpaka maziwa yarudi kwenye chuchu yake.(Hadith Sahih).

Allah atuepushe na Jahannam na atuwafikishe kufanya matendo ili tupate pepo yake. Innahu waliyyu dhaalika walqqadir alayhi.

MAKALA IMEANDALIWA NA RAUDHWAH ISLAMIC GROUP

NI UPI MOTO WA ALLAH -SEHEMU YA KWANZA


Makala kutoka Raudhwah Islamic Group

Kila sifa njema zinamstahikia Allah Mola wa viumbe vyote. Swala na salamu zimuendee Mtume wetu Muhammad (swalla Allahu alaihi wa sallam) na ahli zake na maswahaba wake.

Kua na khofu ni katika jambo la kimaumbile kwa wanaadamu. Na hakuna mwanadamu asiekua na khofu , kwani kila mtu anacho kinachomkhofisha kwa mfano tajiri atakhofu kufilisika au kiongozi kuadhirika na khofu nyenginezo, lakini muislamu wa kweli hakuna kitu ambacho anakikhofu zaidi ya kukhofu adhabu za Allah (subhanahu wataala). Anajua kua Allah ameandaa adhabu kali kwa atakaemuasi. Muumini wa kweli anajua lengo lake ni kuepukana na adhabu hiyo ya jahannam, na hayo ndio mafanikio ya kweli ,kama anavyosema Allah (subhanahu wataala) “ Atakaevushwa na moto na akaingizwa peponi basi huyo amefuzu” (3:185). Allah (subhanahu wataala), ameeleza kua yeye ni mkali wa kuadhibu, na adhabu zake hakuna kiumbe aliewahi kumuadhibu kiumbe mwenzake, na kifungo chake ndani ya jahananam hakuna aliwahi kumfunga mwenziwe hapa duniani.

Amesema“Basi siku hiyo hatoadhibu yoyote namna ya adhabu yake.(25) Na wala hatafunga yoyote mfano wa kifungo chake.(26)” (Suratul Fajri). Jee aya hizi tumezizingatia? Maana tunaona adhabu mbalimbali wanazoadhibiwa watu duniani, iwe waislamu na wasiokua waislamu,hadi wengine kufikia kujiua kwa uchungu wa adhabu, lakini yote hayo hayafui dafu mbele ya Adhabu za Allah. Allah ameuleza moto kiasi kwamba, amesema Mtume (swalla Allahu alaihi wa sallam) yake kua ,hatolala mwenye kuukimbia,akimaanisha kua mtu atakaesikia habari zake, basi atafanya juhudi aepukane na jahannam. Hii kuonesha kua adhabu zake ni kali mno. Tumekatazwa kuadhibiana kwa moto duniani kwani adhabu ya moto ni adhabu yenye kufedhehesha na ni ya Allah pekee. Allah ameandaa malipo mabaya kwa watakaofanya ubaya.

Ameyakariri hayo Allah (subhanahu wataala) takriban katika kila sura ndani ya Qur-an, ili kuwatisha watu na Moto. Kila anapotaja pepo hutaja na moto, ili watu wapate kutafakari. Lakini jee tumeyazingatia haya? Allah ameuumba moto na tayari upo,na uko karibu na mmoja wetu kuliko nyuzi za viatu vyake (Hadith), na unazidi kukolea siku hadi siku kwa ajili ya kuwachoma watu watakaoingia humo. Mara Moja moto ulishtaki kwa Allah (subhanahu wataala), kua unaanza kujila wenyewe kwa wenyewe kutokana na makali yake. Allah akauruhusu kupumua mara mbili kwa mwaka, katika kipindi cha joto na kipindi cha baridi. Inasimuliwa katika hadithi kua Allah alivyouumba moto aliukoleza miaka 1000 ukawa mwekundu kuliko chochote, akaukoleza tena miaka 1000 mengine, ukawa mweupe kuliko chochote, na akaukoleza tena miaka 1000 ukawa mweusi, na sasa ni mweusi kama weusi wa shimo lenye kina kirefu. Amesema Rasuul (swalla Allahu alaihi wa sallam) kua Moto wa duniani ni moja kati ya sehemu 70 za Jahannam(Bukhari na Muslim). Tukumbuke kua kuni za moto huo ni watu na mawe, kama anavyosema Allah “Enyi mloamini jiokoeni nafsi zenu na watu wenu, kutokana na moto kuni zake ni watu na mawe” (Tahrym : 6).

Na watu hao wataengezwa maumbile yao yawe makubwa, ili adhabu iwafaidi, kama anavyosema Rasuul (swalla Allahu alaihi wa sallam) katika hadith iliyopokelewa na Abi-Hurayra kua “Baina ya mabega mawili ya makafiri ni mwendo wa siku tatu, kwa aliepanda mnyama anaekwenda mbio” (Bukhari) .Na katika hadith sahihi kua jua litaingizwa ndani ya jahannam siku ya qiyamah,basi vipi litakua joto lake ikiwa hivi sasa liko mbali kilomita na ma kilomita vipi likiwa limo ndani ya tanuri la jahannam na watu wamo ndani yake? Habari za jahannam ni nzito ambazo hazielezeki kwa maneno wala hazifirikiki kwa akili, kwani ni adhabu juu ya adhabu. (Allah atuhifadhi).

Moto umetajwa kua una milango saba (suratul-Hijri), na umetajwa takriban mara 66 ndani ya Qur-an, na na kumetajwa majina yake,sifa ya watu watakaoingia humo, aina za adhabu zao,chakula chao,vinywaji vyao,mavazi yao na adhabu nyenginezo. Moto una darakaat yani daraja za kwenda chini, na kila daraka ya chini ndio yenye adhabu kali kuliko ya juu yake,na daraka ya chini kabisa ni ya wanafik kama anavyosema Allah katika suratu-Nisai “Hakika wanaafiki watakuwa katika t'abaka ya chini kabisa Motoni,…”(4:145). (Allah atuhifadhi).

A : MAJINA YA MOTO

Moto umetajwa kwa majina takriban tisa ndani ya Qur-an nayo ni:

1- JAHANNAM: Huu ndio moto mkubwa na uwakao vikali, wameandaliwa makafiri. Umetajwa mara nyingi katika Qur-an. Amesema Allah katika suratu-Qaaf kuonesha ukali wa moto huu “Siku tukapoiambia jahannam : Jee umejaa? Itasema Jee kuna nyongeza?”.

2- Saqar: Huu ni moto ambao wataingia ndani yake watu wasioswali,na wengineo.Amesema Allah kuhadithia watu wa peponi watakapowauliza watu wa motoni “Nini kilichokuingizeni katika SAQAR, watasema tulikua si wenye kusali.”(Mudathir 42-43). Akasema tena kuelezea moto huu “Na ni nini kitakachokujuulisha huo (saqar)?,(27) Haubakishi wala hauwachi,(28) unababua ngozi maramoja,(29)Juu yake kuna walinzi 19.(30)” Suratu Mudathir.

3- Ladhaaa: Amesema Allah katka Suratul-Maarij kuhusiana na moto huu: “Kwa hakika huo ni moto uwakao barabara,(15) unaobabua maramoja ngozi ya mwili (16)”

4- Hutwamah: Huu ni moto watakaoingia ndani yake wasengenyaji,na wenye kurundika mali bila ya kutumia katika kheri. Allah ameutaja katika suratul-Humazah. “Bila shaka atavurumishwa katika moto wa Hutwamah(4)”.

5- Sairaa: Umetajwa katika sehemu nyingi ndani ya Qur-an kama katika suratul-mulk na nyenginezo

6- Jahiim: Ni moto uwakao vikali na umetajwa katika sehemu nyingi ndani ya Qur-an kama katika Suratu Shuraa ya ya 91 na nyenginezo

7- Haawiyah: umetajwa katika Suratul-Qariah aya 9-11

8- Daarul-Bawaar: Umetajwa katika suratu-ibrahiim aya ya 28.

9- Nnaar : Pia umetajwa sehemu nyingi ukiambatanishwa na majina mengine au kutajwa pekee yake.Mfano ndani ya Suratul Baqara aya ya 275.

Usikose muendelezo wa mada hii nzito yenye kumtia khofu muislamu kuogopa adhabu za Allah. Allah atukinge na adhabu ya moto. Aaamin.

MAKALA IMEANDALIWA NA RAUDHWAH ISLAMIC GROUP

Thursday 12 June 2014

NI IPI PEPO YA ALLAH (SUBHANAHU WATAALA) - SEHEMU YA PILI

Makala kutoka Raudhwah Islamic Group

CHAKULA CHA WATU WA PEPONI

Anasema Allah subhanah katika suratu swaffat aya ya 41-42 “Hao ndio watakaopewa rizki maalum.(41) Matunda (ya kila namna) na wataheshimiwa(42)”. Na kasema katika suratul waaqiah aya ya 21 “ Na ndege kama watakavotamani wenyewe” . Vitu hivyo vitawajia palepale walipo kama anavyosema Allah “Na vivuli vyake vitakua karibu yao na mashada ya matunda yake yataning’inia mpaka chini (walipo)”. Inasimuliwa kua peponi kutakua na mti ambao kivuli chake atatembea mpandaji mnyama kwa muda wa miaka 100 ,na hajakimaliza.Na katika Hadithi ya Mtume (swalla Allahu alayhi wasallam) iliyokua sahihi ilopokelewa na Imam Muslim na Abu-Daud anaeleza kua watu wa peponi watakula, na hawatoenda chooni si kufanya haja ndogo wala kubwa,na jasho lao litakua ni miski.

Allah mara nyingi akitaja chakula cha jannah hutaja matunda aina kwa aina kama alivyotaja katika Suratu Rahman kua kutakua na makomamanaga na mengineo, hii ni kutokana na kua wanaadamu wengi wanafadhilisha nyama na matunda kuliko aina nyengine za vyakula ,lakini tukumbuke kua kuna neema ambazo macho hazijawahi kuona wala akili kuwahi kuzifikiri hivyo yawezekana kuna aina nyengine nyingi za vyakula ambazo wahusika watakutana nazo (Allah atujaalie miongoni mwao).

VINYWAJI VYA WATU WA PEPONI

Anasema Allah(subhanahu wataala) kuelezea vinywaji vya watu wa peponi kwa mjumuiko katika Suratu-Muhammad aya ya 15, “Mfano wa pepo waloahidiwa wacha-Mungu, imo mito ya maji isiyovunda,na mito ya maziwa isiyoharibika ladha yake,na mito ya ulevi wenye ladha kwa wanywaji,na mito ya asali ilosafishwa...”. Mito yote hiyo asili yake inaanzia katika pepo ya juu ya Firdaus na baadae kushuka katika pepo nyenginezo za chini . Pia kutakua na kinywaji cha Tasneem kimetajwa katika Suratul-Mutaffin kinywaji ambacho watapata watu wa Firdaus waliokua karibu zaidi na Allah ambacho hakijachanganywa na chochote ama waliobaki watapata ambacho kimechanganyika na kitu chengine.

Vinywaji hivyo vitasambazwa na vijana ambao wanang’ara kama anavyosema Allah “Na humo watanyweshwa kinywaji kilochanganyika na tangawizi. Huo ni mto ulokuwemo humo unaitwa Salsabil.Na watawazungukia(kuwatumikia) vijana wasiochakaa,ukiwaona utafkiri lulu zilotawanywa” (Dahri 17-19). Na vyombo vyao kama anavyosema Allah”Na watapitishiwa vyombo vya fedha na vikombe vya vigae. Vigae vya fedha kujazwe humo kwa kipimo”(Suratu Dahr :15-16)

MAVAZI YA WATU WA PEPONI: Watu wa peponi watavishwa nguo za Hariri ambazo zina thamani ya hali ya juu,na Allah ameharamisha kuvaliwa duniani ili akawape waja wake wema Peponi. Amesema Allah “Juu yao wana nguo za Hariri laini, za kijani kibichi na za Hariri nzito. Na watavishwa vikukuu vya fedha..” (Dahri 21). Na katika hadith ilopokelwa na Imam Muslim ua nguo hizo hazitochakaa.

NYUMBA ZA WATU WA PEPONI

Makaazi ya watu wa peponi kama anavosema Rasuul kua matofali ya nyumba zao itakua ni dhahabu na fedha na saruji yake ni Miski,na mchanga wake ni zafarani na changarawe zake ni lulu na yaaquut (Imepokelewa na Tirmidhy na Ahmad).

Humo wataishi katika maghorofa kama anavosema Allah katika suratu Furqaan 75. Pia kutakua na mahema ambayo Rasuul amaeyasifu kua yanatokana na lulu ilo kavu na urefu wake ni maili 60…(Mutaafaqun alayhi). Ndani ya majumba hayo kutakua na mapambo mbalimbali kama anavosema Allah katika suratul-Ghaashiyah 13-16 “Humo kuna viti vya fahari vilivyonyanyuka juu. Na gilasi zilizopangwa.

Na mito ilopangwa safu kwa safu. Na mazulia yalotandikwa”. Na katika suratu Dahr amesema “Na wataegemea humo viti vya enzi hawataona humo jua wala baridi”. Na akasema tena katika suratu-Rahman 76 “wataegemea katika mito ya kijani kibichi, na wakae juu ya mazulia mazuri”

STAREHE NYENGINEZO ZA WATU WA PEPONI

Ukiachilia mbali vyakula,vinywaji,mavazi na wanawake wa jannah, pia peponi kutakua na vipando kama anavyosimulia swahaba Abdul- Rahman bin Saidah kua: Nilikua napenda farasi nikamuuliza Mjumbe wa Allah: Je peponi kutakua na farasi? Akajibu “Ikiwa Allah atakuingiza peponi ewe Abdul-Rahman utakua na Farasi wako anaetokana na yaaqut na atakua na mbawa mbili anaruka utakako” Imepokelewa na Twabraniy.

Pia peponi kutakua na soko kama anavyosimulia Anas radhia Allahu anhu “Hakika peponi kutakua na soko, wataliendea watu kila siku ya ijumaa,utavuma upepo kutoka kaskazini, na utawapata katika nyuso zao na nguo zao, na utawazidisha uzuri ,watarejea kwa wake zao hali ya kua wamezidi uzuri. Watu wao watawaambia:”Tunaapa kwa jina la Allah hakika mumetuzidi uzuri na wao watawajibu na sisi tunaapa hakika nyinyi ndio mlotuzidi uzuri”Imepokelewa na Imam Muslim
Ama neema nyengine ambazo ndio neema Muhimu watakazopewa watu wa peponi ni:

Kumuona Allah(subhanahu wataala): Anasema Allah katika Suratul-Qiyaamah “Nyuso siku hiyo zitang’aa. Zitamtazama Mola wao”. Akasema Mtume (swalla Allahu alayhi wasallam) katika hadithi inayosimuliwa na Abu-hurayra (Radhi za Allah ziwe juu yake) ,na kuwafikiwa na Bukhari na Muslim kua watu walimuuliza Rasuul. Je tutamuona Mola wetu? Rasuul akawajibu mtamuona kama mnavyouna mbaa mwezi”

Radhi za Allah(subhanahu wataala): Anasimulia Mtume wa Allah(swalla Allahu alayhi wasallam) katika hadithi iliyopokelewa na Bukhari na Muslim na kusimuliwa na Abu-Said Khudry kua watu wa peponi baada ya kuingia, Allah atawauliza jee mumeridhika? Watasema: Kwa nini tusiridhike na umetupa ulichokua hujampa yoyote? .. Allah atwaambia:” Nimekuhalalishieni radhi zangu na sitokukasirikieni milele”. Ni furaha ilioje kwa watu wa peponi kwani waliokua wakimkimblia awaridhie amewahakikishia radhi zake milele na milele.

Kuishi Milele: Anasema Allah(subhanahu wataala) katika Suratul-kahfi “Hakika waloamini wakafanya matendo mema makaazi yao yatakua ni pepo za Firdaus. Watakaa humo milele hawatotaka kuondoka” 107-108. Yatosha kukaa milele ni starehe kwani hakuna kuwaza kua neema iko siku itaondoka kama zitakavyoondoka neema za duniani.

Sifa za watakaoingia humo kama anavyosema Rasuul (swalla Allahu alayhi wasallam) kua ucha-Mungu na kua na tabia njema ndio vitakavyowaingiza watu wengi peponi.

HITIMISHO

Mara moja walikaa watu watatu muislamu,mkirsto na yahudi,na kila mmoja akawa anajisifia kua pepo ni yake na imeandaliwa kwa ajili yake. Mkirsto akajisifia kua Mtume wake Issa ni Ruhu-llah na kwamba atakuja duniani kueneza haki,ama yahudi akajisifia kua amaeletewa Mitume wengi na wengi ni mitume mitukufu hivyo pepo ni yake,na muislamu nae akajisifia kua mtume Muhammad(swalla Allahu alayhi wasallam) ndie kipenzi cha Allah na ndio Mtume wa mwisho hivyo pepo ni yake.

Allah akateremsha aya isemayo: “(hiyo pepo) Si kwa matamanio yenu (waislamu) wala si kwa matamanio ya watu wa kitabu (mayahudi na manasara),Atakaefanya uovu basi atalipwa….” Wanavyuon wa Qur-an na baadhi ya masahaba akiwemo sayyidna Ally(radhi za Allah ziwe juu yao) wanasema hii ndio aya yenye kutisha zaidi ndani ya Qur-an,kwani yaonesha wazi iko tofauti na fikra za waislamu wa zama zetu.

Tunadhani kua tukiwa na majina ya kina Muhammad na Ahmad na Khalid basi tutaingia peponi kisa ni waislamu,na hatutoadhibiwa kwa makosa yetu.Tutambue kua pepo haikuwekwa kwa kila anaejiita muislamu, lakini pepo imewekwa kwa walioamni kikweli, na wakafanya matendo mema. Hakuna hata sehemu moja katika Qur-an iliyotaja kua kila atakaeitwa muislamu ataingia peponi tu bila ya kuadhibiwa kwa makosa yake kwanza, lakini sehemu zote Allah(subhanahu wataala) anasema Wale watakaoamini na wakatenda yalo Mema. Amesema Allah(subhanahu wataala) katika Suratu Sabai 37 “Na si mali zenu wala watoto wenu watakaokukurubisheni kwetu katika daraja za (peponi) ila alieamini na akafanya matendo mema,basi hao watapata ujira mkubwa na wa ziada kwa yale waliyoyatenda..”.

Kufanya matendo mema kunakusudiwa mengi,lakini kubwa lao ni kuepukana kuedekeza matamanio ya nafsi, kwani pepo imezungushiwa yale yanayochukiwa na nafsi. Muislamu anahitajika kufanya aliyoamrishwa na Allah, kuanzia nguzo za kiislamu na mengineo ambayo tumetakiwa kuyafanya kama vile sadaka,kupigania dini ya Allah na mengine mengi, kama alivyousiwa swahaba Muadh katika Hadithi ndefu ya Rasuul, na akahitimishiwa kwa kuwaambia, ili uweze kumiliki kufanya yote hayo ni lazima aweze kuumiliki ulimi wake, kwani Ulimi na utupu ndo vitakavowakosesha watu Pepo kulingana na Hadith Sahih ya Rasuul .

Hivyo basi milango ya pepo huachwa wazi ramadhan kwa kila anaetaka kuingia, na ya moto hufungwa.Tufanye juhudi ya kuipata pepo kwani Allah kila akimaliza kutaja neema za peponi husema :Kutokana na hayo washindane na wenye kushindana” na mahali pengine akasema ;Kutokana na hayo(yani starehe za peponi) na wafanye wenye kufanya. Amesema Mtume wa Allah “Hakika bidhaa ya Allah ni ghali, Hakika bidhaa ya Allah ni pepo” basi na tuikimbilie hiyo bidhaa kabla ya kudoda kwani ikidoda hainunuliki tena na ndio itakua ni siku ya majuto.

Allah atuwafikishe katika kheri na ataruzuku pepo na vyenye kutukurubisha kwenye pepo Innahu waliyyu dhaalika wal-Qaadir alayhi.

Makala imeandaliwa na Raudhwah Islamic Group