Sunday 29 June 2014

MALIPO YA MWENYE KUFUNGA SIKU YA QIYAMAH


Makala imeandaliwa na Raudhwah Islamic Group

Kila sifa njema zinamstahikia Allah (subuhanahu wata‘ala) Muumba wa wanaadamu na viliyomo duniani na akhera na baina yake na akavikadiria maisha yao. Swala na salamu zimuendee Mtume wetu Muhammad (swalla Allahu alaihi wa sallam).
Ndugu wa Kiislamu, Allah (subuhanahu wata‘ala) ametuwekea namna mbali mbali za ibada ili kutujenga kiroho na kimwili kuwa ndani ya twa‘a yake wakati wote. Swaum (funga) ni moja ya ibada hizo na ni nguzo ya nne katika Uislamu kama anavyosema Mtume (swalla Allahu alaihi wa sallam): “Uislamu umejengwa kwa nguzo tano: Kushuhudia kuwa hapana Mola apasae kuabudiwa isipokuwa Allah na Muhammad ni mja wake na mjumbe wake, Kusimamisha Swala, Kutoa zaka, Kufunga Ramadhaan, na Kwenda Makka kuhiji kwa mwenye uwezo.” Bukhary na Muslim.
Na imethibiti kufaradhishwa kwake ndani ya mwezi wa Ramadhaan pale Allah Aliposema: “Enyi mlio amini! Mmefaradhishiwa Saumu, kama waliyo faradhishiwa walio kuwa kabla yenu ili mpate kuwa wachaMungu.” [Al-Baqara 2 : 183].
Swaum ni ‘amali yenye kumpatia mja malipo mengi makubwa makubwa wakati ambao amefunga kwa matendo mbali mbali ya ibada anayoyafanya akiwa ndani ya mwezi mtukufu wa Ramadhaan. Kwa leo in sha Allah, tutazungumzia malipo ambayo Allah (subuhanahu wata‘ala) amemuandalia mfungaji siku ya Qiyamah.
Swaum ni kiombezi. Swaum itakuja kumuombea shifaa mwenye kufunga siku ya Qiyama kama ilivyothibiti hadithi kutoka kwa Abdullah ibh Amr (radhi za Allah ziwe juu yake), Amesema Mtume (swalla Allahu alaihi wa sallam): “Funga na Quran ni  viombezi viwili vya mja wa Allah siku ya Qiyamah, Funga itasema: Ewe Mola, nilimzuia na chakula na matamanio wakati wa mchana, niruhusu nimuombee. Na uombezi wao utakubaliwa.” Ahmad.
Swaum ni sababu ya kumuingiza mtu Peponi. Mwenye kufunga na akaitimiza funga yake na akajiepusha na maovu na machafu yanayopunguza fadhila za swaum, Allah amemuandalia pepo kwa ajili yake. Abuu Umamah amesema: “Nilienda kwa Mtume (swalla Allahu alaihi wa sallam) nikamwambia: Niamrishe ‘amali ambayo itaniwezesha kuingia peponi. Akasema: “Jilazimishe na kufunga kwani hakuna iliyo sawa na hiyo.” Baadae nikaja tena kwake na Akasema: “Jilazimishe na kufunga.” Ahmad, An-Nasai na Al-Hakim.
Allah atawafadhilisha wenye kufunga kwa kuwaingiza Peponi kupitia mlango maalum uitwao Rayyaan. Amesimulia Sahl ibn Sa‘ad (radhi za Allah ziwe juu yake) kuwa Mtume (swalla Allahu alaihi wa sallam) amesema: “Kuna mlango wa kuingilia Peponi uitwao Rayyaan, siku ya Qiyama utasema: wako wapi walokuwa wakifunga? Akishapita wa mwisho kuingia (mlango) utafungwa.” Bukhary na Muslim.

Swaum humsaidia mfungaji kuwekwa mbali na mashimo ya moto wa Jahannam. Imesimuliwa na Abu Said al-Kudry (radhi za Allah ziwe juu yake) kuwa Mtume (swalla Allahu alaihi wa sallam) amesema: “Hakuna mja atakaefunga siku moja katika njia ya Allah isipokuwa Allah atamuondoshea moto umbali wa miaka sabiin na uso wake.” Imepokewa na kundi la watu wa hadithi isipokuwa Abu Daud.
Swaum ni ‘amal yenye malipo makubwa kiasi kwamba Allah (subuhanahu wata‘ala) amesema kuwa ‘amali hii ni kwa ajili yake na yeye ndiye atakayeilipa pasi na kubainisha ukubwa wa malipo yake. Kutoka kwa Abu Hurayrah (radhi za Allah ziwe juu yake), Mtume (swalla Allahu alaihi wa sallam) amesema: Allah amesema: Kila ‘amali anayoifanya mwanaadam ni kwa ajili yake isipokuwa funga, kwani hiyo ni kwa ajili yangu, na Nitatoa malipo kwa ajili yake (funga). Funga ni ngao, ikiwa mtu amefunga asitumie lugha chafu, asinyanyue sauti yake, au kufanya vitendo viovu. Ikiwa mtu atamtolea maneno au kupigana naye aseme “mimi nimefunga” ... ” Muslim, Ahmad na An-Nasai.
Ndugu wa Kiislamu, hayo  ni katika baadhi ya Aliyotuandalia Allah (subuhanahu wata‘ala) endapo tutaitekeleza ibada hii kwa usahihi wake na kujiepusha na yale yote yenye kupunguza fadhila za swaum kama kucheza game wakati mtu amefunga au karata au kutizama filamu na tamthilia zinazokwenda kinyume na maadili ya Uislamu.
Tunamuomba Allah (subuhanahu wata‘ala) atuwezeshe kuifunga Ramadhani hii na zijazo kwa namna anayoiridhia na kuifurahia na atuwezeshe kupata malipo yote aliyowaandalia wafungaji. Amin.

No comments:

Post a Comment