Friday 5 June 2020

Nikaah (Ndoa)

بُلُوغُ الْمَرام
Buluwgh Al-Maraam


كِتَابُ اَلنِّكَاحِ
Kitabu cha Nikaah (Ndoa)


824.
عَنْ عَبْدِ اَللَّهِ بْنِ مَسْعُودٍ رَضِيَ اللهُ عَنْهُ  قَالَ لَنَا رَسُولُ اَللَّهِ صَلَّى اللهُ عَلَيْهِ وَآلِهِ وَسَلَّمْ  {يَا مَعْشَرَ اَلشَّبَابِ! مَنِ اسْتَطَاعَ مِنْكُمُ اَلْبَاءَةَ فَلْيَتَزَوَّجْ، فَإِنَّهُ أَغَضُّ لِلْبَصَرِ، وَأَحْصَنُ لِلْفَرْجِ، وَمَنْ لَمْ يَسْتَطِعْ فَعَلَيْهِ بِالصَّوْمِ، فَإِنَّهُ لَهُ وِجَاءٌ"} مُتَّفَقٌ عَلَيْهِ
Kutoka kwa ‘Abdullaah bin Mas-‘uwd (رَضِيَ اللهُ عَنْهُ) amesema Rasuli wa Allaah (صَلَّى اللهُ عَلَيْهِ وَآلِهِ وَسَلَّمْ) alituambia: “Enyi mkusanyiko wa vijana, anayeweza miongoni mwenu kumudu ndoa na aoe,[1] kwani huko kuoa huinamisha zaidi macho na huhifadhi zaidi tupu. Na asiyeweza basi ajilazimu swawm; kwani huko swawm kwake ndiko kuyavunja matamanio.” [Al-Bukhaariy, Muslim]


825.
وَعَنْ أَنَسِ بْنِ مَالِكٍ رَضِيَ اللهُ عَنْهُ {أَنَّ اَلنَّبِيَّ صَلَّى اللهُ عَلَيْهِ وَآلِهِ وَسَلَّمْ حَمِدَ اَللَّهَ، وَأَثْنَى عَلَيْهِ ، وَقَالَ: " لَكِنِّي أَنَا أُصَلِّي وَأَنَامُ، وَأَصُومُ وَأُفْطِرُ، وَأَتَزَوَّجُ اَلنِّسَاءَ، فَمَنْ رَغِبَ عَنْ سُنَّتِي فَلَيْسَ مِنِّي} مُتَّفَقٌ عَلَيْهِ
Kutoka kwa Anas bin Maalik (رَضِيَ اللهُ عَنْهُ) amesema kuwa Nabiy (صَلَّى اللهُ عَلَيْهِ وَآلِهِ وَسَلَّمْ): “Alimhimidi Allaah na akamsifu, akasema… lakini mimi naswali[2] na nalala, nafunga (swawm) na ninakula na naoa wanawake. Basi atakayechukia mwenendo wangu basi si katika mimi.” [Al-Bukhaariy, Muslim]



826.
وَعَنْهُ قَالَ: {كَانَ رَسُولُ اَللَّهِ صَلَّى اللهُ عَلَيْهِ وَآلِهِ وَسَلَّمْ  يَأْمُرُ بِالْبَاءَةِ، وَيَنْهَى عَنِ التَّبَتُّلِ نَهْيًا شَدِيدًا، وَيَقُولُ :" تَزَوَّجُوا اَلْوَدُودَ اَلْوَلُودَ . إِنِّي مُكَاثِرٌ بِكُمُ اَلْأَنْبِيَاءَ يَوْمَ اَلْقِيَامَةِ}  رَوَاهُ أَحْمَدُ، وَصَحَّحَهُ اِبْنُ حِبَّانَ
وَلَهُ شَاهِدٌ: عِنْدَ أَبِي دَاوُدَ، وَالنَّسَائِيِّ، وَابْنِ حِبَّانَ أَيْضًا مِنْ حَدِيثِ مَعْقِلِ بْنِ يَسَارٍ
Kutoka kwa Anas bin Maalik (رَضِيَ اللهُ عَنْهُ) amesema kuwa Rasuli wa Allaah (صَلَّى اللهُ عَلَيْهِ وَآلِهِ وَسَلَّمْ): “Alikua akituamrisha kuoa na akitukataza kuacha kuoa[3] makatazo makali na akisema: Oweni wanawake wanaozaaa wanaopendeza (kwa waume zao), kwa hakika mimi nitakuwa mwenye kujifakhiri (mbele ya) Manabiy kwa sababu yenu Siku ya Qiyamah.” [Imetolewa na Ahmad na akaisahihisha Ibn Hibbaan]
Na ina ushahidi kwa Abuu Daawuwd, An-Nasaaiy na Ibn Hibbaan kutoka katika Hadiyth ya Ma’qil bin Yasaar



827.
وَعَنْ أَبِي هُرَيْرَةَ رَضِيَ اللهُ عَنْهُ عَنِ النَّبِيِّ صَلَّى اللهُ عَلَيْهِ وَآلِهِ وَسَلَّمْ قَالَ:{ تُنْكَحُ اَلْمَرْأَةُ لِأَرْبَعٍ: لِمَالِهَا، وَلِحَسَبِهَا، وَلِجَمَالِهَا، وَلِدِينِهَا، فَاظْفَرْ بِذَاتِ اَلدِّينِ تَرِبَتْ يَدَاكَ} مُتَّفَقٌ عَلَيْهِ مَعَ بَقِيَّةِ اَلسَّبْعَةِ 
Kutoka kwa Abuu Hurayrah (رَضِيَ اللهُ عَنْهُ) amesema kuwa Nabiy (صَلَّى اللهُ عَلَيْهِ وَآلِهِ وَسَلَّمْ) amesema: “Mwanamke huolewa kwa mambo manne:[4] kwa mali yake, hadhi yake, uzuri wake na Dini yake. Basi oa aliyeshika Dini (vinginevyo) mikono yako itachafuka.”[5] [Al-Bukhaariy, Muslim pamoja na Maimaam saba (Al-Bukhaariy, Muslim, At-Tirmidhiy, An-Nasaaiy, Abuu Daawuwd, Ibn Maajah, Ahmad) waliobakia.



828.
وَعَنْهُ، أَنَّ اَلنَّبِيَّ صَلَّى اللهُ عَلَيْهِ وَآلِهِ وَسَلَّمْ كَانَ إِذَا رَفَّأَ إِنْسَانًا إِذَا تَزَوَّجَ قَالَ: {بَارَكَ اَللَّهُ لَكَ، وَبَارَكَ عَلَيْكَ، وَجَمَعَ بَيْنَكُمَا فِي خَيْرٍ} رَوَاهُ أَحْمَدُ، وَالْأَرْبَعَةُ، وَصَحَّحَهُ اَلتِّرْمِذِيُّ، وَابْنُ خُزَيْمَةَ، وَابْنُ حِبَّانَ
Kutoka kwa Abuu Hurayrah (رَضِيَ اللهُ عَنْهُ) amesema kuwa Nabiy (صَلَّى اللهُ عَلَيْهِ وَآلِهِ وَسَلَّمْ): “Alikuwa anapomuombea mtu du’aa njema, akimuombea:[6]
بَارَكَ اَللَّهُ لَكَ، وَبَارَكَ عَلَيْكَ، وَجَمَعَ بَيْنَكُمَا فِي خَيْرٍ



Baaraka Allaahu laka, wa baaraka ‘alayka, wa jama’a baynakumaa fiy khayr (Allaah Akubariki (katika mke wako) na Abariki juu yako (uweze kumudu gharama zake) na Awajumuishe katika kheri).” [Imetolewa na Ahmad na Al-Arba’ah (At-Tirmidhiy, An-Nasaaiy, Abuu Daawuwd, Ibn Maajah), na akaisahihisha At-Tirmidhiy, Ibn Khuzaymah na Ibn Hibbaan]



829.
وَعَنْ عَبْدِ اَللَّهِ بْنِ مَسْعُودٍ رَضِيَ اللهُ عَنْهُ  قَالَ: {عَلَّمَنَا رَسُولُ اَللَّهِ صَلَّى اللهُ عَلَيْهِ وَآلِهِ وَسَلَّمْ اَلتَّشَهُّدَ فِي اَلْحَاجَةِ: " إِنَّ اَلْحَمْدَ لِلَّهِ، نَحْمَدُهُ، وَنَسْتَعِينُهُ، وَنَسْتَغْفِرُهُ، وَنَعُوذُ بِاَللَّهِ مِنْ شُرُورِ أَنْفُسِنَا، مَنْ يَهْدِهِ اَللَّهُ فَلَا مُضِلَّ لَهُ، وَأَشْهَدُ أَنْ لَا إِلَهَ إِلَّا اَللَّهُ، وَأَشْهَدُ أَنَّ مُحَمَّدًا عَبْدُهُ وَرَسُولُهُ وَيَقْرَأُ ثَلَاثَ آيَاتٍ"} رَوَاهُ أَحْمَدُ، وَالْأَرْبَعَةُ، وَحَسَّنَهُ اَلتِّرْمِذِيُّ، وَالْحَاكِمُ 
Kutoka kwa ‘Abdullaah bin Mas-‘uwd (رَضِيَ اللهُ عَنْهُ) amesema: “Rasuli wa Allaah (صَلَّى اللهُ عَلَيْهِ وَآلِهِ وَسَلَّمْ) alitufundisha kushahadia katika haja (ndoa na jambo lolote):

إِنَّ اَلْحَمْدَ لِلَّهِ، نَحْمَدُهُ، وَنَسْتَعِينُهُ، وَنَسْتَغْفِرُهُ، وَنَعُوذُ بِاَللَّهِ مِنْ شُرُورِ أَنْفُسِنَا، مَنْ يَهْدِهِ اَللَّهُ فَلَا مُضِلَّ لَهُ، وَأَشْهَدُ أَنْ لَا إِلَهَ إِلَّا اَللَّهُ، وَأَشْهَدُ أَنَّ مُحَمَّدًا عَبْدُهُ وَرَسُولُهُ

Innal-Hamda liLLaah, nahmaduhu, wa nasta’iynuhu, wa nastaghfiruhu, wa na’uwdhu biLLaahi min shuruwri anfusinaa, man yahdihi-LLaahu falaa mudhwilla lah, wa ash-hadu an laa ilaaha illa Allaah, wa ash-hadu anna Muhammadan ‘abduhu wa rasuwluhu
(Hakika Himdi anastahiki Allaah, tunamhimidi, tunamuomba msaada na tunamuomba maghfirah. Tunajikinga kwa Allaah dhidi ya shari za nafsi zetu. Anayeongozwa na Allaah hakuna wa kumpoteza na anayepotezwa Naye hakuna wa kumuongoza. Nashuhudia kuwa hapana mwabudiwa wa haki ila Allaah na nashuhudia kuwa Muhammad ni Mja wake na ni Rasuli wake) baada ya hapo anasoma Aayah tatu.” [Imetolewa na Ahmad na Al-Arba’ah (At-Tirmidhiy, An-Nasaaiy, Abuu Daawuwd, Ibn Maajah), na akaisahihisha At-Tirmidhiy na Al-Haakim]



830.
وَعَنْ جَابِرٍ رَضِيَ اللهُ عَنْهُ قَالَ: قَالَ رَسُولُ اَللَّهِ صَلَّى اللهُ عَلَيْهِ وَآلِهِ وَسَلَّمْ {إِذَا خَطَبَ أَحَدُكُمُ الْمَرْأَةَ، فَإِنْ اِسْتَطَاعَ أَنْ يَنْظُرَ مِنْهَا مَا يَدْعُوهُ إِلَى نِكَاحِهَا، فَلْيَفْعَلْ} رَوَاهُ أَحْمَدُ، وَأَبُو دَاوُدَ، وَرِجَالُهُ ثِقَاتٌ، وَصَحَّحَهُ اَلْحَاكِمُ
وَلَهُ شَاهِدٌ: عِنْدَ اَلتِّرْمِذِيِّ، وَالنَّسَائِيِّ، عَنِ الْمُغِيرَةِ. 
وَعِنْدَ اِبْنِ مَاجَهْ، وَابْنِ حِبَّانَ: مِنْ حَدِيثِ مُحَمَّدِ بْنِ مَسْلَمَةَ 
وَلِمُسْلِمٍ: عَنْ أَبِي هُرَيْرَةَ رَضِيَ اللهُ عَنْهُ {أَنَّ اَلنَّبِيَّ صَلَّى اللهُ عَلَيْهِ وَآلِهِ وَسَلَّمْ قَالَ لِرَجُلٍ تَزَوَّجَ اِمْرَأَةً: أَنَظَرْتَ إِلَيْهَا ؟ " قَالَ: لَا. قَالَ: " اِذْهَبْ فَانْظُرْ إِلَيْهَا}
Kutoka kwa Jaabir (رَضِيَ اللهُ عَنْهُ) amesema Rasuli wa Allaah (صَلَّى اللهُ عَلَيْهِ وَآلِهِ وَسَلَّمْ) amesema: “Yeyote miongoni mwenu anapomposa mwanamke, iwapo ataweza kumtazama sehemu zinazomvutia ndoa yake[7] basi afanye hivyo.” [Imetolewa na Ahmad, Abuu Daawuwd na wapokezi wake ni madhubuti, na akaisahihisha Al-Haakim]
Hadiyth hii ina ushahidi kwa At-Tirmidhiy na An-Nisaaiy kutoka kwa Al-Mughiyrah.
Ibn Maajah na Ibn Hibbaan wameipokea kutoka katika Hadiyth ya Muhammad bin Maslamah.[8]
Na kutoka katika Riwaayah ya Muslim kutoka kwa Abuu Hurayrah (رَضِيَ اللهُ عَنْهُ) amesema kuwa: “Nabiy (صَلَّى اللهُ عَلَيْهِ وَآلِهِ وَسَلَّمْ) alimuambia mtu alietaka kuoa, “Je umemuangalia?” akasema: “Hapana” Akasema: “Nenda ukamuangalie.”



831.
وَعَنِ ابْنِ عُمَرَ  رَضِيَ اَللَّهُ عَنْهُمَا قَالَ: قَالَ رَسُولُ اَللَّهِ صَلَّى اللهُ عَلَيْهِ وَآلِهِ وَسَلَّمْ {لَا يَخْطُبْ بَعْضُكُمْ عَلَى خِطْبَةِ أَخِيهِ، حَتَّى يَتْرُكَ اَلْخَاطِبُ قَبْلَهُ، أَوْ يَأْذَنَ لَهُ اَلْخَاطِبُ}  مُتَّفَقٌ عَلَيْهِ، وَاللَّفْظُ لِلْبُخَارِيِّ
Kutoka kwa Ibn ‘Umar (رَضِيَ اللهُ عَنْهُمَا) amesema Rasuli wa Allaah (صَلَّى اللهُ عَلَيْهِ وَآلِهِ وَسَلَّمْ) amesema: “Asipose yeyote miongoni mwenu juu ya posa ya nduguye[9] (Muislamu) mpaka yule mposaji aache kabla yake au amruhusu.” [Al-Bukhaariy, Muslim na tamshi hili ni la Al-Bukhaariy]



832.
وَعَنْ سَهْلِ بْنِ سَعْدٍ اَلسَّاعِدِيِّ  رَضِيَ اَللَّهُ عَنْهُمَا قَالَ: {جَاءَتِ امْرَأَةٌ إِلَى رَسُولِ اَللَّهِ صَلَّى اللهُ عَلَيْهِ وَآلِهِ وَسَلَّمْ فَقَالَتْ: يَا رَسُولَ اَللَّهِ! جِئْتُ أَهَبُ لَكَ نَفْسِي، فَنَظَرَ إِلَيْهَا رَسُولُ اَللَّهِ صَلَّى اللهُ عَلَيْهِ وَآلِهِ وَسَلَّمْ  فَصَعَّدَ اَلنَّظَرَ فِيهَا، وَصَوَّبَهُ، ثُمَّ طَأْطَأَ رَسُولُ اَللَّهِ صَلَّى اللهُ عَلَيْهِ وَآلِهِ وَسَلَّمْ رَأْسَهُ، فَلَمَّا رَأَتْ اَلْمَرْأَةُ أَنَّهُ لَمْ يَقْضِ فِيهَا شَيْئًا جَلَسَتْ، فَقَامَ رَجُلٌ مِنْ أَصْحَابِهِ
فَقَالَ: يَا رَسُولَ اَللَّهِ! إِنْ لَمْ يَكُنْ لَكَ بِهَا حَاجَةٌ فَزَوِّجْنِيهَا .
قَالَ: " فَهَلْ عِنْدكَ مِنْ شَيْءٍ ؟ " .
فَقَالَ: لَا، وَاَللَّهِ يَا رَسُولَ اَللَّهِ .
فَقَالَ: " اِذْهَبْ إِلَى أَهْلِكَ، فَانْظُرْ هَلْ تَجِدُ شَيْئًا ؟ " فَذَهَبَ، ثُمَّ رَجَعَ ؟
فَقَالَ: لَا، وَاَللَّهِ يَا رَسُولَ اَللَّهِ، مَا وَجَدْتُ شَيْئًا.
فَقَالَ رَسُولُ اَللَّهِ صَلَّى اللهُ عَلَيْهِ وَآلِهِ وَسَلَّمْ " انْظُرْ وَلَوْ خَاتَمًا مِنْ حَدِيدٍ"، فَذَهَبَ، ثُمَّ رَجَعَ
فَقَالَ: لَا وَاَللَّهِ ، يَا رَسُولَ اَللَّهِ ، وَلَا خَاتَمًا مِنْ حَدِيدٍ، وَلَكِنْ هَذَا إِزَارِي قَالَ سَهْلٌ: مَالُهُ رِدَاءٌ  فَلَهَا نِصْفُهُ .
فَقَالَ رَسُولُ اَللَّهِ صَلَّى اللهُ عَلَيْهِ وَآلِهِ وَسَلَّمْ مَا تَصْنَعُ بِإِزَارِكَ ؟ إِنْ لَبِسْتَهُ لَمْ يَكُنْ عَلَيْهَا مِنْهُ شَيْءٌ، وَإِنْ لَبِسَتْهُ لَمْ يَكُنْ عَلَيْكَ شَيْءٌ " فَجَلَسَ اَلرَّجُلُ، وَحَتَّى إِذَا طَالَ مَجْلِسُهُ قَامَ، فَرَآهُ رَسُولُ اَللَّهِ صَلَّى اللهُ عَلَيْهِ وَآلِهِ وَسَلَّمْ  مُوَلِّيًا، فَأَمَرَ بِهِ، فَدُعِيَ لَهُ، فَلَمَّا جَاءَ .
قَالَ: "مَاذَا مَعَكَ مِنَ الْقُرْآنِ  ؟ " .
قَالَ: مَعِي سُورَةُ كَذَا، وَسُورَةُ كَذَا، عَدَّدَهَا .
فَقَالَ: "تَقْرَؤُهُنَّ عَنْ ظَهْرِ قَلْبِكَ ؟ " .
قَالَ: نَعَمْ، قَالَ : "اِذْهَبْ، فَقَدَ مَلَّكْتُكَهَا بِمَا مَعَكَ مِنَ الْقُرْآنِ} مُتَّفَقٌ عَلَيْهِ، وَاللَّفْظُ لِمُسْلِمٍ  .
وَفِي رِوَايَةٍ لَهُ: {اِنْطَلِقْ، فَقَدْ زَوَّجْتُكَهَا، فَعَلِّمْهَا مِنَ الْقُرْآنِ}
وَفِي رِوَايَةٍ لِلْبُخَارِيِّ: {أَمْكَنَّاكَهَا بِمَا مَعَكَ مِنَ الْقُرْآنِ}  
وَلِأَبِي دَاوُدَ: عَنْ أَبِي هُرَيْرَةَ قَالَ:{مَا تَحْفَظُ ؟ " .قَالَ: سُورَةَ اَلْبَقَرَةِ، وَاَلَّتِي تَلِيهَا . قَالَ: " قُمْ . فَعَلِّمْهَا عِشْرِينَ آيَةً}
Kutoka kwa Sahl bin Sa’d As-Saa’idiyy (رَضِيَ اللهُ عَنْهُ) amesema: “Alikuja  mwanamke hadi kwa Rasuli wa Allaah (صَلَّى اللهُ عَلَيْهِ وَآلِهِ وَسَلَّمْ) akasema: “Ee Rasuli wa Allaah! Nimekuja kukupa nafsi yangu.” Rasuli wa Allaah (صَلَّى اللهُ عَلَيْهِ وَآلِهِ وَسَلَّمْ) akamtazama juu mpaka chini kisha akainamisha kichwa chake. Yule mwanamke alipoona kuwa hakumuambia lolote aliketi. Mtu mmoja katika Maswahaba akasema: “Ee Rasuli wa Allaah, ikiwa huna haja naye niozeshe mimi.” Nabiy (صَلَّى اللهُ عَلَيْهِ وَآلِهِ وَسَلَّمْ) akasema: “Una kitu?” Akasema: “Sina Wa-Allaahi Ee Rasuli wa Allaah!” Akasema: “Nenda kwa jamaa zako utazame kama utapata kitu.” Akaenda kisha akarudi, akasema: “Wa-Allaahi sikupata kitu!” Rasuli wa Allaah (صَلَّى اللهُ عَلَيْهِ وَآلِهِ وَسَلَّمْ) akasema: “Tafuta hata kama ni pete ya chuma.” Akaenda kisha akarudi, akasema: “Wa-Allaahi Ee Rasuli wa Allaah! Sikupata hata pete ya chuma! Lakini nina hiki kikoi changu.”  Sahli (mpokezi wa Hadiyth) amesema: Alikuwa hana shuka. Rasuli wa Allaah (صَلَّى اللهُ عَلَيْهِ وَآلِهِ وَسَلَّمْ) akasema: “Atakifanya nini  kikoi chako? Ukikivaa yeye hatakuwa na kitu, naye akikivaa wewe hutakuwa na kitu.” Yule mtu akaketi kwa kitambo kirefu kisha akainuka. Rasuli wa Allaah (صَلَّى اللهُ عَلَيْهِ وَآلِهِ وَسَلَّمْ) akamuona akienda zake, akaamrisha aitwe, alipokuja akasema: “Umehifadhi kiasi gani cha Qur-aan?” Akasema: “Nimehifadhi Suwrah kadha wa kadhaa.” akazihesabu Suwrah alizohifadhi, akasema: “Umezihifadhi kwa moyo?” Akasema: “Ndiyo” Akasema: “Nimekuoza kwa ulichohifadhi katika Qur-aan.”[10] [Al-Bukhaariy, Muslim na tamshi hili ni la Muslim]
Na katika Riwaayah ya Abuu Daawuwd aliyoipokea kutoka kwa Abuu Hurayrah: “Nabiy (صَلَّى اللهُ عَلَيْهِ وَآلِهِ وَسَلَّمْ) alimuuliza umehifadhi nini?” Akasema: “Suwratul-Baqarah na inayofuatia.” Akasema Nabiy (صَلَّى اللهُ عَلَيْهِ وَآلِهِ وَسَلَّمْ): “Nenda ukamfundishe Aayah ishirini.”



833.
وَعَنْ عَامِرِ بْنِ عَبْدِ اَللَّهِ بْنِ اَلزُّبَيْرِ، عَنْ أَبِيهِ، أَنَّ رَسُولَ اَللَّهِ صَلَّى اللهُ عَلَيْهِ وَآلِهِ وَسَلَّمْ  قَالَ:{أَعْلِنُوا اَلنِّكَاحَ} رَوَاهُ أَحْمَدُ ، وَصَحَّحَهُ اَلْحَاكِمُ
Kutoka kwa ‘Aamir bin ‘Abdillaah bin Az-Zubayr[11] kutoka kwa baba yake amesema kuwa Rasuli wa Allaah (صَلَّى اللهُ عَلَيْهِ وَآلِهِ وَسَلَّمْ) amesema: “Tangazeni ndoa.”[12] [Imetolewa na Ahmad na akaisahihisha Al-Haakim]



834.
وَعَنْ أَبِي بُرْدَةَ بْنِ أَبِي مُوسَى، عَنْ أَبِيهِ قَالَ: قَالَ رَسُولُ اَللَّهِ صَلَّى اللهُ عَلَيْهِ وَآلِهِ وَسَلَّمْ  {لَا نِكَاحَ إِلَّا بِوَلِيٍّ} رَوَاهُ أَحْمَدُ وَالْأَرْبَعَةُ وَصَحَّحَهُ اِبْنُ اَلْمَدِينِيِّ، وَاَلتِّرْمِذِيُّ، وَابْنُ حِبَّانَ، وَأُعِلَّ بِالْإِرْسَالِ
Kutoka kwa Abuu Burdah bin Abiy Muwsaa kutoka kwa baba yake amesema Rasuli wa Allaah (صَلَّى اللهُ عَلَيْهِ وَآلِهِ وَسَلَّمْ) amesema: “Ndoa haiswihi ila kwa walii.”[13] [Imetolewa na Ahmad na Al-Arba’ah (At-Tirmidhiy, An-Nasaaiy, Abuu Daawuwd, Ibn Maajah) na akaisahihisha Ibn Al-Madiyniyy, At-Tirmidhiy na Ibn Hibbaan, na wengine wameiona na ila kwa kuwa ni Mursal]



835.
وَعَنْ عَائِشَةَ رَضِيَ اَللَّهُ عَنْهَا قَالَتْ: قَالَ رَسُولُ اَللَّهِ صَلَّى اللهُ عَلَيْهِ وَآلِهِ وَسَلَّمْ {أَيُّمَا اِمْرَأَةٍ نَكَحَتْ بِغَيْرِ إِذْنِ وَلِيِّهَا، فَنِكَاحُهَا بَاطِلٌ، فَإِنْ دَخَلَ بِهَا فَلَهَا اَلْمَهْرُ بِمَا اِسْتَحَلَّ مِنْ فَرْجِهَا، فَإِنِ اشْتَجَرُوا فَالسُّلْطَانُ وَلِيُّ مَنْ لَا وَلِيَّ لَهُ} أَخْرَجَهُ اَلْأَرْبَعَةُ إِلَّا النَّسَائِيَّ، وَصَحَّحَهُ أَبُو عَوَانَةَ، وَابْنُ حِبَّانَ وَالْحَاكِمُ
Kutoka kwa ‘Aaishah (رَضِيَ اللَّهُ عَنْهَا) amesema Rasuli wa Allaah (صَلَّى اللهُ عَلَيْهِ وَآلِهِ وَسَلَّمْ) amesema: “Mwanamke yeyote anayeolewa bila idhini ya walii wake ndoa yake ni batili. (Mume) akimuingilia mwanamke huyo ana haki ya kupata mahari kwa alichohalalishia tupu yake. Wakishindana,[14] basi sultani (mtawala) ni walii wa asiyekuwa na walii.” [Imetolewa na Al-Arba’ah (At-Tirmidhiy, Abuu Daawuwd, Ibn Maajah) isipokuwa An-Nasaaiy, na akaisahihisha Abuw ‘Awaanah, Ibn Hibbaan na Al-Haakim] 



836.
وَعَنْ أَبِي هُرَيْرَةَ رَضِيَ اللهُ عَنْهُ أَنَّ رَسُولَ اَللَّهِ صَلَّى اللهُ عَلَيْهِ وَآلِهِ وَسَلَّمْ قَالَ: {لَا تُنْكَحُ اَلْأَيِّمُ حَتَّى تُسْتَأْمَرَ، وَلَا تُنْكَحُ اَلْبِكْرُ حَتَّى تُسْـتَأْذَنَ" قَالُوا : يَا رَسُولَ اَللَّهِ، وَكَيْفَ إِذْنُهَا ؟ قَالَ: " أَنْ تَسْكُتَ} مُتَّفَقٌ عَلَيْهِ
Kutoka kwa Abuu Hurayrah (رَضِيَ اللهُ عَنْهُ) amesema kuwa Rasuli wa Allaah (صَلَّى اللهُ عَلَيْهِ وَآلِهِ وَسَلَّمْ) amesema: “Asiolewe mke mkuu mpaka atakwe amri, wala asiolewe mwanamwali mpaka atakwe idhini.[15] Maswahaba wakasema: Ee Rasuli wa Allaah! Ni vipi idhini yake (huyo mwali)? Akasema: Ni kunyamaza.” [Al-Bukhaariy, Muslim]



837.
وَعَنْ اِبْنِ عَبَّاسٍ رَضِيَ اللهُ عَنْهُمَا  أَنَّ اَلنَّبِيَّ صَلَّى اللهُ عَلَيْهِ وَآلِهِ وَسَلَّمْ  قَالَ {اَلثَّيِّبُ أَحَقُّ بِنَفْسِهَا مِنْ وَلِيِّهَا ، وَالْبِكْرُ تُسْتَأْمَرُ ، وَإِذْنُهَا سُكُوتُهَا} رَوَاهُ مُسْلِمٌ 
وَفِي لَفْظٍ:{لَيْسَ لِلْوَلِيِّ مَعَ اَلثَّيِّبِ أَمْرٌ، وَالْيَتِيمَةُ تُسْتَأْمَرُ} رَوَاهُ أَبُو دَاوُدَ، وَالنَّسَائِيُّ، وَصَحَّحَهُ اِبْنُ حِبَّانَ
Kutoka kwa Ibn ‘Abbaas (رَضِيَ اللهُ عَنْهُمَا) amesema kuwa Nabiy (صَلَّى اللهُ عَلَيْهِ وَآلِهِ وَسَلَّمْ) amesema: “Mke mkuu ana haki zaidi kwa nafsi yake kuliko walii wake,[16] na mwanamwali hutakwa idhini, na idhini yake ni kunyamaza.” [Imetolewa na Muslim]
Katika tamshi lingine inasema: “Walii hana amri kwa mke mkuu. Yatima huombwa idhini.” [Imetolewa na Abuu Daawuwd na An-Nasaaiy na akaisahihisha Ibn Hibbaan]



838.
وَعَنْ أَبِي هُرَيْرَةَ رَضِيَ اللهُ عَنْهُ  قَالَ: قَالَ رَسُولُ اَللَّهِ صَلَّى اللهُ عَلَيْهِ وَآلِهِ وَسَلَّمْ {لَا تُزَوِّجُ اَلْمَرْأَةُ اَلْمَرْأَةَ، وَلَا تُزَوِّجُ اَلْمَرْأَةُ نَفْسَهَا} رَوَاهُ اِبْنُ مَاجَهْ، وَاَلدَّارَقُطْنِيُّ، وَرِجَالُهُ ثِقَاتٌ 
Kutoka kwa Abuu Hurayrah (رَضِيَ اللهُ عَنْهُ) amesema Rasuli wa Allaah (صَلَّى اللهُ عَلَيْهِ وَآلِهِ وَسَلَّمْ) amesema: “Mwanamke hamuozeshi mwanamke, wala mwanamke hajiozeshi mwenyewe.”[17] [Imetolewa na Ibn Maajah na Ad-Daaraqutwniy na wapokezi wake ni madhubuti]



839.
وَعَنْ نَافِعٍ ، عَنْ اِبْنِ عُمَرَ قَالَ:{نَهَى رَسُولُ اَللَّهِ صَلَّى اللهُ عَلَيْهِ وَآلِهِ وَسَلَّمْ عَنِ الشِّغَارِ، وَالشِّغَارُ: أَنْ يُزَوِّجَ اَلرَّجُلُ اِبْنَتَهُ عَلَى أَنْ يُزَوِّجَهُ اَلْآخَرُ اِبْنَتَهُ، وَلَيْسَ بَيْنَهُمَا صَدَاقٌ} مُتَّفَقٌ عَلَيْهِ  
وَاتَّفَقَا مِنْ وَجْهٍ آخَرَ عَلَى أَنَّ تَفْسِيرَ اَلشِّغَارِ مِنْ كَلَامِ نَافِعٍ
Kutoka kwa Naafi’ naye kutoka kwa Ibn ‘Umar (رَضِيَ اللهُ عَنْهُمَا) amesema: “Rasuli wa Allaah (صَلَّى اللهُ عَلَيْهِ وَآلِهِ وَسَلَّمْ) amekataza ndoa ya Ash-Shighaar. Ash-Shighaar ni mtu kumuoza binti yake ili yule mwingine naye amuoze binti yake bila mahari baina yao.” [Al-Bukhaariy, Muslim]
Wameafikiana (Al-Bukhaariy na Muslim) wa njia nyingine kuwa tafsiri ya Ash-Shighaar iliyoelezwa ni maneno ya Naafi’]



840.
وَعَنِ ابْنِ عَبَّاسٍ رَضِيَ اَللَّهُ عَنْهُمَا{أَنَّ جَارِيَةً بِكْرًا أَتَتِ النَّبِيَّ صَلَّى اللهُ عَلَيْهِ وَآلِهِ وَسَلَّمْ  فَذَكَرَتْ: أَنَّ أَبَاهَا زَوَّجَهَا وَهِيَ كَارِهَةٌ، فَخَيَّرَهَا اَلنَّبِيُّ صَلَّى اللهُ عَلَيْهِ وَآلِهِ وَسَلَّمْ} رَوَاهُ أَحْمَدُ، وَأَبُو دَاوُدَ، وَابْنُ مَاجَهْ، وَأُعِلَّ بِالْإِرْسَالِ
Kutoka kwa Ibn ‘Abbaas (رَضِيَ اللهُ عَنْهُمَا) amesema: “Kuna binti mmoja bikra (mwanamwali) alimuendea Nabiy (صَلَّى اللهُ عَلَيْهِ وَآلِهِ وَسَلَّمْ) akamueleza kuwa baba yake alimuozesha naye (binti huyo) akiwa amechukia. Nabiy (صَلَّى اللهُ عَلَيْهِ وَآلِهِ وَسَلَّمْ) akamkhiyarisha.”[18] [Imetolewa na Ahmad, Abuu Daawuwd na Ibn Maajah na imedhoofishwa kwa kuwa ni Mursal]



841.
وَعَنْ اَلْحَسَنِ، عَنْ سَمُرَةَ، عَنِ اَلنَّبِيِّ صَلَّى اللهُ عَلَيْهِ وَآلِهِ وَسَلَّمْ قَالَ: {أَيُّمَا اِمْرَأَةٍ زَوَّجَهَا وَلِيَّانِ، فَهِيَ لِلْأَوَّلِ مِنْهُمَا} رَوَاهُ أَحْمَدُ، وَالْأَرْبَعَةُ، وَحَسَّنَهُ اَلتِّرْمِذِيُّ 
Kutoka kwa Hasan naye kutoka kwa Samurah (رَضِيَ اللهُ عَنْهُ) amesema kuwa Nabiy (صَلَّى اللهُ عَلَيْهِ وَآلِهِ وَسَلَّمْ) amesema: “Mwanamke yeyote aliyeozeshwa na mawalii wawili, basi yeye ni mke wa mume aliyeozeshwa na walii wa kwanza.”[19] [Imetolewa na Ahmad na Al-Arba’ah (At-Tirmidhiy, An-Nasaaiy, Abuu Daawuwd, Ibn Maajah) na akaisahihisha At-Tirmidhiy]



842.
وَعَنْ جَابِرٍ قَالَ: قَالَ رَسُولُ اَللَّهِ صَلَّى اللهُ عَلَيْهِ وَآلِهِ وَسَلَّمْ {أَيُّمَا عَبْدٍ تَزَوَّجَ بِغَيْرِ إِذْنِ مَوَالِيهِ أَوْ أَهْلِهِ، فَهُوَ عَاهِرٌ} رَوَاهُ أَحْمَدُ، وَأَبُو دَاوُدَ، وَاَلتِّرْمِذِيُّ وَصَحَّحَهُ، وَكَذَلِكَ اِبْنُ حِبَّانَ
Kutoka kwa Jaabir (رَضِيَ اللهُ عَنْهُ) amesema Rasuli wa Allaah (صَلَّى اللهُ عَلَيْهِ وَآلِهِ وَسَلَّمْ) amesema: “Mtumwa yeyote[20] anayeoa bila idhini ya mabwana zake au jamaa zake huyo ni mzinifu.” [Imetolewa na Ahmad, Abuu Daawuwd na At-Tirmidhiy na ameisahihisha vile vile Ibn Hibbaan]



843.
وَعَنْ أَبِي هُرَيْرَةَ رَضِيَ اللهُ عَنْهُ  أَنَّ اَلنَّبِيَّ صَلَّى اللهُ عَلَيْهِ وَآلِهِ وَسَلَّمْ  قَالَ: {لَا يُجْمَعُ بَيْنَ اَلْمَرْأَةِ وَعَمَّتِهَا، وَلَا بَيْنَ اَلْمَرْأَةِ وَخَالَتِهَا} مُتَّفَقٌ عَلَيْهِ 
Kutoka kwa Abuu Hurayrah (رَضِيَ اللهُ عَنْهُ) amesema kuwa Nabiy (صَلَّى اللهُ عَلَيْهِ وَآلِهِ وَسَلَّمْ) amesema: “Asikusanye (asioe) mtu baina ya mwanamke na shangazi yake wala baina ya mwanamke na mama yake mdogo.” [Al-Bukhaariy, Muslim]



844.
وَعَنْ عُثْمَانَ رَضِيَ اللهُ عَنْهُ  قَالَ: قَالَ رَسُولُ اَللَّهِ صَلَّى اللهُ عَلَيْهِ وَآلِهِ وَسَلَّمْ {لَا يَنْكِحُ اَلْمُحْرِمُ، وَلَا يُنْكَحُ} رَوَاهُ مُسْلِمٌ . وَفِي رِوَايَةٍ لَهُ: {وَلَا يَخْطُبُ}
وَزَادَ اِبْنُ حِبَّانَ: {وَلَا يُخْطَبُ عَلَيْهِ}
Kutoka kwa ‘Uthmaan (رَضِيَ اللهُ عَنْهُ) amesema Rasuli wa Allaah (صَلَّى اللهُ عَلَيْهِ وَآلِهِ وَسَلَّمْ) amesema: “Mwenye kuhirimia[21] haoi wala kuozesha.” [Imetolewa na Muslim]
Na katika Riwaayah nyingine: “…wala kuposa.”
Na Ibn Hibbaan ameongeza: “…wala haposewi.”



845.
وَعَنِ ابْنِ عَبَّاسٍ رَضِيَ اَللَّهُ عَنْهُمَا قَالَ: {تَزَوَّجَ اَلنَّبِيُّ صَلَّى اللهُ عَلَيْهِ وَآلِهِ وَسَلَّمْ مَيْمُونَةَ وَهُوَ مُحْرِمٌ} مُتَّفَقٌ عَلَيْهِ
وَلِمُسْلِمٍ: عَنْ مَيْمُونَةَ نَفْسِهَا {أَنَّ اَلنَّبِيَّ صَلَّى اللهُ عَلَيْهِ وَآلِهِ وَسَلَّمْ تَزَوَّجَهَا وَهُوَ حَلَالٌ}
Kutoka kwa Ibn ‘Abbaas (رَضِيَ اللهُ عَنْهُمَا) amesema: “Nabiy (صَلَّى اللهُ عَلَيْهِ وَآلِهِ وَسَلَّمْ) alimoa Maymuwnah hali ya kuwa amehirimia.” [Al-Bukhaariy, Muslim]
Na katika Riwaayah ya Muslim kutoka kwa Maymuwnah mwenyewe amesema kuwa: “Nabiy (صَلَّى اللهُ عَلَيْهِ وَآلِهِ وَسَلَّمْ) alimuoa hali ya kuwa ametoka kuhirimia.”



846.
وَعَنْ عُقْبَةَ بْنِ عَامِرٍ رَضِيَ اللهُ عَنْهُ  قَالَ: قَالَ رَسُولُ اَللَّهِ صَلَّى اللهُ عَلَيْهِ وَآلِهِ وَسَلَّمْ {إِنَّ أَحَقَّ اَلشُّرُوطِ أَنْ يُوَفَّى بِهِ، مَا اِسْتَحْلَلْتُمْ بِهِ اَلْفُرُوجَ} مُتَّفَقٌ عَلَيْهِ 
Kutoka kwa ‘Uqbah bin ‘Aamir (رَضِيَ اللهُ عَنْهُ) amesema Rasuli wa Allaah (صَلَّى اللهُ عَلَيْهِ وَآلِهِ وَسَلَّمْ) amesema: “Hakika masharti yalio na haki zaidi kutekelezwa[22] ni yale mnayohalalishia tupu.”[23] [Al-Bukhaariy, Muslim]



847.
وَعَنْ سَلَمَةَ بْنِ الْأَكْوَعِ رَضِيَ اللهُ عَنْهُ  قَالَ: {رَخَّصَ رَسُولُ اَللَّهِ صَلَّى اللهُ عَلَيْهِ وَآلِهِ وَسَلَّمْ  عَامَ أَوْطَاسٍ فِي اَلْمُتْعَةِ، ثَلَاثَةَ أَيَّامٍ، ثُمَّ نَهَى عَنْهَا} رَوَاهُ مُسْلِمٌ
Kutoka kwa Salamah bin Al-Akwa’ (رَضِيَ اللهُ عَنْهُ) amesema: “Rasuli wa Allaah (صَلَّى اللهُ عَلَيْهِ وَآلِهِ وَسَلَّمْ) aliruhusu mwaka wa Vita vya Awtwaas ndoa ya Mut’ah[24] siku tatu kisha akaikataza.” [Imetolewa na Muslim]



848.
وَعَنْ عَلَيٍّ رَضِيَ اللهُ عَنْهُ قَالَ: {نَهَى رَسُولُ اَللَّهِ صَلَّى اللهُ عَلَيْهِ وَآلِهِ وَسَلَّمْ عَنْ اَلْمُتْعَةِ عَامَ خَيْبَرَ} مُتَّفَقٌ عَلَيْهِ
Kutoka kwa ‘Aliy (رَضِيَ اللهُ عَنْهُ) amesema: “Rasuli wa Allaah (صَلَّى اللهُ عَلَيْهِ وَآلِهِ وَسَلَّمْ) amekataza ndoa ya Mut’ah mwaka wa Vita vya Khaybar.” [Al-Bukhaariy, Muslim]



849.
وَعنْهُ أَنَّ رَسولَ الله صلى الله عليه وسلم {نَهَى عَنْ مُتْعَةِ النِّسَاءِ وَعَنْ  أَكْلِ الْحُمُرِ الأَهْلِيَّةِ يَوْمَ خَيْبَرَ}  أخْرَجَهُ السَّبْعَةُ إلاَّ أبا داوُد
Kutoka kwa ‘Aliy (رَضِيَ اللهُ عَنْهُ) amesema kuwa: “Rasuli wa Allaah (صَلَّى اللهُ عَلَيْهِ وَآلِهِ وَسَلَّمْ) amekataza Mut’ah ya wanawake na kula nyama ya punda wa mjini siku ya vita vya Khaybar.” [Imetolewa na As-Sab’ah (Al-Bukhaariy, Muslim, At-Tirmidhiy, An-Nasaaiy, Ibn Maajah, Ahmad) isipokuwa Abuu Daawuwd]



850.
عَنِ الرَّبِيعِ بْنِ سَبْرَةَ، عَنْ أَبِيهِ، رضي الله عنه أنَّ رَسولَ اللَّهِ صلى الله عليه وسلم قال:
{إنِّي كُنْت أَذِنْت لَكُمْ فِي الاِسْتِمْتَاعِ مِنَ النَّساء، وَإِنَّ اللَّهَ قَدْ حَرَّمَ ذلك  إِلَى يَوْمِ الْقِيَامَةِ، فَمَنْ كَانَ عِنْدَهُ مِنْهُنَّ شَىْءٌ فَلْيُخَلِّ سَبِيلَهَا وَلاَ تَأْخُذُوا مِمَّا آتَيْتُمُوهُنَّ شَيْئًا}‏ أخْرَجَهُ مُسْلِمٌ وَأَبُو دَاوُدَ وَالنَّسَائِيُّ و اِبْنِ مَاجَهْ و أَحْمَدُ و اِبْنُ حِبَّانَ
Kutoka kwa Ar-Rabiy’ bin Sabrah[25] kutoka kwa baba yake amesema kuwa Rasuli wa Allaah (صَلَّى اللهُ عَلَيْهِ وَآلِهِ وَسَلَّمْ) amesema: “Nilikuwa nimewaruhusu ndoa ya Mut’ah ya wanawake, kwa hakika Allaah Ameiharamisha ndoa hiyo mpaka siku ya Qiyaamah. Ambaye ana mke wa mut’ah basi amuache aende zake wala msichukue chochote mlichowapa.” [Imetolewa na Muslim, Abuu Daawuwd, An-Nasaaiy, Ibn Maajah, Ahmad na Ibn Hibbaan]



851.
وَعَنِ ابْنِ مَسْعُودٍ رَضِيَ اللهُ عَنْهُ قَالَ: {لَعَنَ رَسُولُ اَللَّهِ صَلَّى اللهُ عَلَيْهِ وَآلِهِ وَسَلَّمْ  اَلْمُحَلِّلَ وَالْمُحَلَّلَ لَهُ} رَوَاهُ أَحْمَدُ، وَالنَّسَائِيُّ، وَاَلتِّرْمِذِيُّ وَصَحَّحَهُ 
وَفِي اَلْبَابِ: عَنْ عَلِيٍّ أَخْرَجَهُ اَلْأَرْبَعَةُ إِلَّا النَّسَائِيَّ
Kutoka kwa Ibn Mas-‘uwd (رَضِيَ اللهُ عَنْهُ) amesema: “Rasuli wa Allaah (صَلَّى اللهُ عَلَيْهِ وَآلِهِ وَسَلَّمْ) amemlaani mwenye kuhalalisha na mwenye kuhalalishwa.”[26] ‘Mwenye kuhalalisha’ ni mtu kumuoa mwanamke aliyeachwa na mume mwingine talaka tatu kwa niyyah ya kumhalalishia yule mume wa kwanza baada ya yeye kumtaliki baada ya kujamiiana naye. [Imetolewa na Ahmad na An-Nasaaiy na At-Tirmidhiy akaisahihisha]
Katika mlango huu kuna Hadiyth iliyopokewa kutoka kwa ‘Aliy iliyopokewa na Maimaam wane (At-Tirmidhiy, Abuu Daawuwd, Ibn Maajah) isipokuwa An-Nasaaiy.



852.
وَعَنْ أَبِي هُرَيْرَةَ رَضِيَ اللهُ عَنْهُ  قَالَ: قَالَ رَسُولُ اَللَّهِ صَلَّى اللهُ عَلَيْهِ وَآلِهِ وَسَلَّمْ {لَا يَنْكِحُ اَلزَّانِي اَلْمَجْلُودُ إِلَّا مِثْلَهُ} رَوَاهُ أَحْمَدُ، وَأَبُو دَاوُدَ، وَرِجَالُهُ ثِقَاتٌ 
Kutoka kwa Abuu Hurayrah (رَضِيَ اللهُ عَنْهُ) amesema Rasuli wa Allaah (صَلَّى اللهُ عَلَيْهِ وَآلِهِ وَسَلَّمْ) amesema: “Mzinifu aliyepigwa mijeledi asioe isipokuwa mfano wake.”[27] [Imetolewa na Ahmad na Abuu Daawuwd na wapokezi wake ni waaminifu (madhubuti)



853.
وَعَنْ عَائِشَةَ رَضِيَ اَللَّهُ عَنْهَا، قَالَتْ: {طَلَّقَ رَجُلٌ اِمْرَأَتَهُ ثَلَاثًا، فَتَزَوَّجَهَا رَجُلٌ، ثُمَّ طَلَّقَهَا قَبْلَ أَنْ يَدْخُلَ بِهَا، فَأَرَادَ زَوْجُهَا أَنْ يَتَزَوَّجَهَا، فَسُئِلَ رَسُولُ اَللَّهِ صَلَّى اللهُ عَلَيْهِ وَآلِهِ وَسَلَّمْ عَنْ ذَلِكَ، فَقَالَ: "لَا. حَتَّى يَذُوقَ اَلْآخَرُ مِنْ عُسَيْلَتِهَا مَا ذَاقَ اَلْأَوَّلُ} مُتَّفَقٌ عَلَيْهِ، وَاللَّفْظُ لِمُسْلِمٍ
Kutoka kwa ‘Aaishah (رَضِيَ اللَّهُ عَنْهَا) amesema: “Mtu mmoja alimtaliki mkewe mara tatu, yule mke akaolewa na mwanamme mwingine, kisha akamuacha kabla ya kumuingilia, yule mume wake wa kwanza akataka kumuoa, akamuuliza Rasuli wa Allaah (صَلَّى اللهُ عَلَيْهِ وَآلِهِ وَسَلَّمْ) kuhusu jambo hilo. Rasuli wa Allaah (صَلَّى اللهُ عَلَيْهِ وَآلِهِ وَسَلَّمْ) akasema: “Hapana mpaka mwingine aonje asali yake ile aliyoionja wa kwanza.” (yaani baada ya kuoa mpaka mujamiiane).[28] [Al-Bukhaariy, Muslim na tamshi hili ni la Muslim]


[1] Hii ina maanisha ikiwa mmoja wenu ana uwezo na nguvu za kuoa (kimwili na kimali) na aoe. Wanazuoni wengine wanaona kuwa ni jambo la lazima na wengine wanaona ni jambo lenye kupendeza tu.

[2] Hii ina maana kuzidisha sana katika ‘Ibaadah hakutakiwi. Jambo hilo linamfanya mtu kuchoka na kumfanya asiweze kutekeleza Swalaah za faradhi. Mtu anaweza kutoka katika Uislamu anapofikiria kuwa Swalaah zake anazoswali (na kuzidisha sana) ni bora kuliko Swalaah alizoswali Nabiy (صَلَّى اللهُ عَلَيْهِ وَآلِهِ وَسَلَّمْ).

[3] At-Tabattul ina maana ya kutokuoa, mtu kudhani kuwa kuacha kwake kuoa ni aina ya ‘Ibaadah na kudhani kuwa kuoa kwake ni zuio la kufanya kwake ‘Ibaadah. Tabattul kwa Wanazuoni wote ni jambo lisilofaa na ni tendo lililoharamishwa. Hata hivyo, kutokuoa kwa sababu zisizozuilika ni jambo lingine kabisa.

[4] Nabiy (صَلَّى اللهُ عَلَيْهِ وَآلِهِ وَسَلَّمْ) amesema kuwa kuna mambo manne yanayomfanya na kumshawishi mtu kuoa. Katika mambo haya manne Muislamu anatakiwa achague mwanamke mwenye Dini. Ikiwa mwanamke ataolewa kwa sifa nyinginezo, kuna uwezekano wa mtu kupotoka na kuacha Dini. Sababu nyingine ya kuchagua Dini ni kuwa mwanamke huyo ndie mwalimu wa mwanzo kwa watoto, hivyo kwa Dini yake atawaongoza watoto katika njia iliyonyooka.

[5] Maana ya neno hili: “Mikono yako itachafuka” Waarabu hulisema kwa njia ya kulaumu, wala siyo kwa kupendelea maana yake halisi ya kumtakia mtu shari. Maana ya Hadiyth hii ni kuwa: kwa kawaida watu huoa mwanamke mwenye sifa hizi nne, basi wewe fanya hima umuoe aliyeshika Dini.

[6] Nabiy (صَلَّى اللهُ عَلَيْهِ وَآلِهِ وَسَلَّمْ) alikuwa na tabia ya kuwaombea waliofunga ndoa kwa du’aa nzuri nzuri katika umoja wao, mapenzi na kuwaombea Baraka katika maisha yao.

[7] Hizi ni zile sehemu zenye kuonekana kwa nje, kama vile; urefu, uso, mikono na mfano wa hayo.

[8] Alikuwa miongoni mwa Maswahaba wa Answaar, ukoo wa Haarith. Alihudhuria vita vyote isipokuwa vita vya Tabuwk. Alisilimu kupitia kwa Musw’ab bin ‘Umayr. Alikufa akiwa na umri wa miaka 77 katika mwaka wa 43 Hijriyyah.

[9] Katazo hili limewekwa ili ile posa ya kwanza ya nduguye ithibiti. Ikiwa msichana alishaposwa na mtu mwingine, mtu wa pili asipeleke posa. Hata hivyo ikiwa posa ya kwanza imekataliwa au kuvunjika, basi ni ruhusa posa nyingine iende.

[10] Hadiyth hii inaweka wazi mambo mengi: Miongoni mwa hayo ni kufundisha Qur-aan kunaweza kuwa ndio mahari ya mtu. Kingine kilichowekwa wazi hapa ni kuwa kiwango cha mahari hakijawekwa. Watu wengine wanatoa dalili ya Hadiyth kuwa kiwango cha chini cha mahari ni Dirham kumi. Hili si sahihi na Hadiyth hiyo haina msingi huo.

[11] Huyu ni ‘Aamir bin ‘Abdillaah bin Az-Zubayr bin Al-‘Awwaam Al-Asadi Al-Qurayshi Al-Madaniy. Alikuwa ni Taabi’ na alisikia Hadiyth kutoka kwa baba yake na wengineo. Alikuwa madhubuti na Mwenye taqwa alifariki mwaka wa 124 Hijriyyah.

[12] Sherehe za harusi ni bora zitangazwe ili kuondoa fedheha ya aina yoyote na kadhalika kwa sababu zinginezo. Kuna njia nyingi za matangazo aina hii. Mashahidi katika tukio la ndoa ni matangazo vile. Kutangaza katika kadamnasi ya watu ni aina nyingine ya matangazo.

[13] Hadiyth hii imetajwa na takriban Maswahaba thelathini wa Rasuli wa Allaah (صَلَّى اللهُ عَلَيْهِ وَآلِهِ وَسَلَّمْ). Baadhi ya wapokezi wake ni thiqah (madhubuti). Walii (msimamizi) wa kwanza wa familia ni baba na babu, kisha kaka zake, baada ya hapo baba zake wadogo. Kama kuna rai tofauti kwa mawalii, yeyote aliye karibu zaidi, rai yake itafuatwa zaidi, ikiwa mawalii hao wanalingana kama vile makaka na baba wadogo, kinachofanyika ni mtawala aliyopo ndiye atakayekuwa msimamizi. Vile vile ikiwa kuna wasimamizi wawili wameozesha mwanamke mmoja sehemu mbili tofauti, ndoa ya kwanza iliyofungwa itakuwa ni sahihi na ya pili itakuwa si sahihi. Ikiwa mwanamke aliyeozwa anakubaliana na msimamizi mmoja na kutofautiana na mwingine, rai ya mwanamke itatangulizwa.

[14] Yaani wale mawalii (wasimamizi wa mke) watakaposhindana wakamzuia mwanamke asiolewe, basi uwalii atakuwa nao sultani/mtawala.

[15] Ridhaa ya mwanamke ni jambo la msingi katika ndoa. Ikiwa walii au hata baba anamuozesha binti yake bila ya ridhaa yake, binti ana haki ya kubatilisha ile ndoa na kukataa. Ayyim katika lugha ya kiarabu ni mwanamke aliyekwishawahi kuingiliwa, anaweza kuwa mjane au aliyeachwa. Mzinifu mwanamke ambaye hajaolewa ni Ayyim, lakini kulingana na Shariy’ah siyo Ayyim. Ayyim ni lazima athibitishe ndoa yake kwa kutamka, vinginevyo ndoa haitosihi. Ama bikra ambaye hajabaleghe, ridhaa yake siyo muhimu bali ni ruhusa ya walii wake.

[16] Hii ina maana ya kuwa Ayyim hawezi kuozwa bila ya ridhaa yake, lakini haina maana kuwa anaweza kuolewa bila ya walii. Ikiwa kuna rai tofauti kati ya Ayyim na walii kuhusu mchumba wake na uchaguzi wa mwanamke ukawa ni kutoka katika jamaa zake wa karibu na hakuwa na uhusiano wowote nae mbaya, wakati huo walii atalazimishwa kukubaliana na Ayyim, kama walii hatokubali hilo mwanamke anaweza kuomba msaada wa mtawala wa kumuozesha. Dhul Arhaam (ndugu upande wa mama) hawezi kuwa walii.

[17] Kuhusu ndoa mwanamke hawezi kuwa msimamizi au walii, hawezi kujioza wala hawezi kuozesha mwanamke mwingine.

[18] Ina maana bila ridhaa ya mwanamke, awe bikra au mkuu (Ayyim), hawezi kuozwa, akiolewa bila ya ridhaa yake, ana haki ya kukataa na kuvunja, hata ikiwa ni baba yake au kaka yake ndiye msimamizi wa ndoa ile.

[19] Ikiwa mawalii wawili wamemuozesha mwanamke kwa waume wawili basi ndoa itakayopita ni ya yule mume aliyoozeshwa na walii wa kwanza na ndoa ya pili itakuwa sio sahihi. Ama kama ndoa hizo zitakuwa zimefungwa kwa wakati mmoja, zote zitakuwa ni batili. Kuna rai mbalimbali katika hili.

[20] Kwa ndoa ya mtumwa ni wajibu kupatikana radhi za bwana wake, bila ya ruhusa yake, ndoa haitafungwa. Ikiwa mtumwa hajui ukweli huu kuwa ruhusa ya bwana inatakiwa ni muhimu na akamuingilia mkewe, hatoadhibiwa kwa hilo, lakini kama alikuwa anajua basi ataadhibiwa.

[21] Mtu akiwa katika hali ya Ihraam, kuoa au kuozesha hairuhusiwi. Hii ni kulingana na Wanazuoni takribani wote. Ama kuhusu Hadiyth iliyopokewa na Ibn ‘Abbaas (رَضِيَ اللهُ عَنْهُمَا) sanad yake ni sahihi, lakini alikosea kusema kuwa Nabiy (صَلَّى اللهُ عَلَيْهِ وَآلِهِ وَسَلَّمْ) alimuoa Maymuwnah alipokuwa katika Ihraam. Maymuwnah mwenyewe amethibitisha hili katika Hadiyth iliyofuatia.

[22] Ina maana suala la mahari ni la msingi katika ndoa.

[23] Maana ya Hadiyth hii ni kuwa masharti yaliyo na haki zaidi kutekelezwa ni masharti ya ndoa, bora yasipite mipaka, Al-Khatwaab amesema: ‘Masharti katika ndoa, yako tofauti, muna masharti yanayopasa kutimizwa kwa itifaki ya ‘Ulamaa, nayo ni Aliyoamrisha Allaah ya kushikamana kwa wema au kwa kuachana kwa ihsani, na kwa maana hii Ulamaa wengine wameisherehesha Hadiyth hii. Kuna na masharti yasiyofaa kutekelezwa aslan kama vile mwanamke kuweka sharti mke mwenza atalikiwe. Kuna masharti yaliyo na khitilafu miongoni mwa ‘Ulamaa, kama vile kushaurisha asimuolee mke mwingine’

[24] Mut’ah ni ndoa ya muda maalumu. Aina hii ya ndoa ilikuwepo katika zama za Jaahiliyyah. Kuna wakati Uislamu ulikataza na wakati uliruhusu kwa masharti maalumu, mwishowe ndoa hii iliharamishwa katika Hijjatul-Wada’ (Hijjah ya mwisho ya Nabiy (صَلَّى اللهُ عَلَيْهِ وَآلِهِ وَسَلَّمْ))

[25] Ar-Rabiy’ bin Sabrah bin Ma’bad Al-Juhani Al-Madaniy alikuwa ni mtu madhubuti kulingana na An-Nasaaiy na Al-‘Ajli.

[26] Al-Muhallil “mwenye kuhalalisha” ni mtu kumuoa mwanamke aliyeachwa na mume mwingine talaka tatu kwa niyyah ya kumhalalishia yule mume wa kwanza baada na yeye kumtaliki baada ya kujamiana naye. Ndoa iliyosimama kwa malengo haya ni haramu, iwe ni kwa muda uliotajwa au isiwe hivyo.

[27] Hii ina maana mwenye taqwa asimuoe mwanamke ambaye ameshatuhumiwa na kuthibitishwa kuwa ni mzinifu na vivyo hivyo mwanamke mwenye taqwa asiolewe na mwanamme mzinifu.

[28] Ina maana mwanamke aliyeachwa talaka tatu akiolewa na mtu mwingine na akawa keshaingiliwa na mume yule kisha mume akamuacha au akafariki hapo ndipo anaweza tena kuolewa na yule mume wake wa mwanzo. Kama hajakutana naye kimwili na mume wake wa pili hawezi kuolewa na yule mume wake wa mwanzo.