Wednesday 4 June 2014

KUSAMEHEANA NA FAIDA ZAKE


Kila sifa njema zinamstahikia Allah Mola wa viumbe vyote. Sala na salamu zimuendee Mtume wetu Muhammad (swalla Allahu alaihi wa sallam) na ahli zake na maswahaba wake.

Kwa hakika mwanadamu ni kiumbe dhaifu sana. Na udhaifu wake huanza kuonesha kwa mola wake kwa kumuasi. Hakuna kiumbe yeyote yule anaeweza kuishi katika ulimwengu huu bila ya kumuasi Allah (subhanahu wataala). Ila Allah (subhanahu wataala) akatuwekea milango ya tawba wazi ili wale wenye kumkosea Allah waweze kurudi kwake na waombe msamaha. Vile vile udhaifu wa binaadamu anauonesha tena baina yake na binaadamu wenzake. Hakuna mwanaadamu  anaeweza kukaa na mwanadamu mwenzake bila ya kumkosea. Sote tunakoseana. Ila suala linakuja je baada ya kukosana tuache tu ? Hapana. Lazima baada ya kukosana tuombane msamaha na tusameheane ili tuyaondoshe yale yaliyomo ndani ya nyoyo zetu. Kufanya hivyo kutatufanya sisi tuweze kuishi kwa uzuri. Jambo la kusameheana baina ya watu limezungumziwa na Allah (subhanahu wataala) pale aliposema ndani ya Quraan “na wanajizuia ghadhabu, na wasamehevu kwa watu; na Mwenyezi Mungu huwapenda wafanyao wema”(3:134). Kuzuia ghadhabu zako na kumsamehe yule aliyekukosea ni katika wema na mwenye kufanya wema basi hupendwa na Allah (subhanahu wataala). Je kweli hatutaki kupendwa na Allah ? Na usipopendwa na Allah vipi utaishi katika ulimwengu huu? Vipi utaikabili akhera yako? Pia katika aya nyengine Allah (subhanahu wataala)anasema “Shikamana na kusamehe, na amrisha mema, na jitenge na majahili (wajinga)” (Al-Araaf 7: 199) .

Ugomvi uko kila sehemu na takriban kwa watu wengi sana ila tukimbilie kusameheana ili turejeshe mapenzi baina yetu. Kusamehe kuko kwa namna tatu kuu, namna ya kwanza ni kumsamehe ndugu yako yule aliyekuomba msamaha kutokana na lile alilolifanya. Pili ni kumsamehe ndugu yako hata kama hajakuomba msamaha. Na tatu ambako kuliko kuwa bora zaidi ni kumuomba wewe msamaha ndugu yako aliyekukosea wewe baada ya kuona hajui kosa lake au kwa kujua na akashindwa kukuomba msamaha.

Ndugu yangu muislamu unapomkosea ndugu yako basi kimbilia kumuomba radhi kutokana na lile ulolifanya. Kumuomba radhi muislamu mwenzako hakukushushi cheo wala hadhi. Bali hukupandisha darja zaidi na kuonesha utu na uungwana uliokuwa nao kutokana na kuufahamu vizuri uislamu wako. Pia anapokuja ndugu yako kukuomba msamaha usimrudishe bila ya kumsamehe kwa sababu sisi tunamuasi mangapi Allah tunajua kama haya ni makosa na tunamuasi ila tukirudi kwake anatusamehe. Hivyo basi na sisi tusimpe sheytwan nafasi katika kutufarakanisha.  Na wala usiwe mwenye kujinadi kwa watu kuwa wewe ni bora na ndio maana unaombwa radhi. Yote hayo tuyafanye kwa ajili Allah (subhanahu wataala). Ukiyafanya kwa ajili ya Allah hutokuwa na kiburi,wala majivuno ndani na nje ya nafsi yako.

Je ni zipi faida za waislamu kusameheana baina yetu?

1-Kupendwa na Allah (subhanahu wataala)

Allah (subhanahu wataala) anasema ndani ya Quraan “na wanajizuia ghadhabu, na wasamehevu kwa watu; na Mwenyezi Mungu huwapenda wafanyao wema”(3:134). Kuzuia ghadhabu zako na kumsamehe yule aliyekukosea ni katika wema na mwenye kufanya wema basi hupendwa na Allah (subhanahu wataala).  Na bila ya shaka muumini ndani ya ulimwengu huu huhitaji mapenzi na radhi za Allah. Hivyo katika njia ya kuzipata radhi za Allah ni kusameheana baina yetu.

2- Kujenga mapenzi ,umoja baina ya familia na kuunga udugu.

Katika matatizo makubwa yanayokumbuka familia zetu sasa hivi ni kukithiri kwa ugomvi ndani ya familia. Na bahati mbaya zaidi watu wengi hawatafuti njia za kusuluhisha bali huzidisha zaidi na kuchochea ugomvi ule. Ugomvi husababishwa aidha kwa mali,wake, watoto n.k. Ndugu zangu wa kiislamu panapotokea ugomvi baina ya familia basi pasuluhishwe ugomvi huo. Ili ugomvi huo uondoshwe. Kuweko kwa ugomvi ndani ya familia kutapelekea kukosa mapenzi baina yao, kukosa kuhurumiana baina yao na mwisho kutapelekea kukatika kwa familia ile. Na je tunajua ni ipi adhabu ya mwenye kukata ukoo ? Mtume (swalla Allahu alayhi wasallam) anasema “Haingii peponi mwenye kukata udugu”  Bukhary na Muslim. Kwa hakika tunaitaka pepo ya Allah hivyo basi tuwe wepesi kuombana msamahan na tusameheane. Na ikiwa moja kati yenu hajaomba msamaha kwa kukhofia kutoipata pepo ya Allah basi muumini wa kweli anatakiwa akamfuate ndugu yake waombane msamahana wasameheane ili waweze kuondosha tofauti baina yao.

3- Kujenga na kurejesha mapenzi baina ya wanandoa.

Ndoa nazo zina dhoruba ya ugomvi wa kila mara. Panapotokezea ugomvi baina ya  wanandoa kitu muhimu zaidi ni subra. Baada ya kuwepo subra basi waombane radhi baina ya mke na mume. Kwa hakika mke au mume anapoombwa radhi na mwenzake huwa na furaha na hulainika moyo wake. Kulainika kwa moyo wake kunapelekea kutuliza ugomvi ule na kurejesha tena mapenzi baina yao. Nasaha zangu kwa wanandoa kusiwe na hata mmoja kati yao ambae atakuwa anaona tabu kumuomba samahani mwenzake. Na wala mume asijione kuwa yeye tu ndie anaestahiki kuombwa radhi. Mume akikosea amuombe radhi mkewe na mke akikosea amuombe radhi mume. Je unajua utamu wa neno samahani kwa mke au mume pale wanapokosana. Hebu jaribu kutumia fursa ya kuombana radhi kila punapokosana ili muifanye ndoa yenu iwe imara. Na inapendeza zaidi mmoja wao akimuomba mwenzake samahani huku akimpa zawadi kwa uwezo alojaaliwa bila ya kujikalifisha, au mke kumpikia mume chakula kizuri. Na wewe unaeombwa samahani usirejeshe samahani kurudi tupu msamehe kwani kusameheana ni wema katika uislamu na unapata thawabu kwa wema huo.

4- Kujenga mapenzi baina ya majirani na kupelekea kuishi kwa amani katika nyumba zetu.

Majirani wale waliokosana wasameheane kwa yale yaliyotokezea. Na msamehe jirani ikiwa amekuomba radhi au hajakuomba radhi. Jirani ana haki kubwa sana ndani ya uislamu na muislamu ajue pale jirani yake anapokosa kusalimika kutokana na maneno yake au vitimbi vyake basi hatoingia peponi kwa ushahidi wa hadithi ya Mtume (swalla Allahu alayhi wasallam)  Mtume (swalla Allaahu alayhi wasallam) aliulizwa,“Mwanamke fulani namkumbuka kwa wingi wa Swalah zake, Saumu zake na sadaka zake azitoazo lakini anawaudhi jirani zake kwa ulimi wake.Mtume (swalla Allaahu alayhi wasallam) akajibu, ‘Kwa hakika yeye ni mtu wa motoni”. Imepokea na Imam Ahmad  . Hivyo ndugu yangu wa kiislamu msamehe jirani yako kwa kosa alilokufanyia kwa kujua au kutokujua, kwa kukuomba radhi au kutokuomba radhi.

5- Kusameheana baina ya waislamu wawili kunapelekea kujiepusha na makatazo ya Allah

Kusameheana vipi kutatufanya tujiepushe na makatazo ya Allah ? Mtume (swalla Allahu alayhi wasallam) anasema “ Si halali kwa muislamu amhame ndugu yake wa kiislamu zaidi ya siku tatu, hata wanapokutana huyu anamgeuzia (uso) huyu na huyu anamgeuzia (uso) huyu. Na aliye mbora wao ni yule anayeanza kutoa salaam”.Bukhari na Muslim.  Na katika riwaya nyengine "Atakayemhama (mwenzake) zaidi ya siku tatu akafariki, basi ataingia motoni" Abuu Daud. Hivyo basi ndugu zangu wa kiislamu kwanza tuwe wenye kuombana radhi pale tunapokosana na pia tuwe wenye kusameheana na ikiwa ndugu yako amekukosea na kama hajakuomba radhi basi msamehe ili uwe mbali na kumuasi Allah (subhanahu wataala).

6- Kupata kivuli cha Allah (subhanahu wataala)

Haya yameelezwa na Mtume (swalla Allahu alayhi wasallam) pale alipowafundisha waislamu awe mwenye kumvumulia ndugu yake muislamu kutokana na deni au amsamehe basi atapata kivuli siku ambayo hakutokuwa na kivuli ila cha Allah. Imepokelewa kutoka kwa Abu Hurayrah(radhi za Allah ziwe juu yake) amesema: “Mtume  wa Allaah (swalla Allahu alayhi wasallam) amesema: "Atakayemuakhirishia mwenye usiri (wa kulipa deni) au akamsamehe, Allah Atamfunika kivuli Siku ya Qiyaamah chini ya kivuli cha Arshi yake, siku ambayo hakutakuwa na kivuli isipokuwa kivuli Chake. Attirmidhy. Na Allah (subhanahu wataala) anasema “Na ikiwa (mdaiwa) ni mwenye hali ngumu, basi (mdai) angoje muda wa kufarijika (anayemdai).  Na  mkitoa swadaqah (deni mnalodai)  basi ni kheri kwenu mkiwa mnajua” (2:280).

Mwisho kabisa nimalizie mada yangu kwa kisa kinachotufunza kuhusu kusameheana.

Vijana watatu walikwenda mbele ya Khalifa  wa  Waislamu Umar bin Al Khattab (Radhiya Llahu anhu) wakiwa wamemkamata mtu waliyemfunga kamba. Wakasema kumwambia Umar (Radhiya Llahu anhu):

"Mtu huyu amemuuwa baba yetu na amekiri juu ya jambo hilo, isipokuwa ametuomba tumpe siku tatu ili aweze kusafiri kwa wanawe kwa ajili ya kuwajulisha juu ya hazina aliyoifukia mahala ambapo hapana anayepajuwa isipokuwa yeye peke yake". Sahaba mmoja aitwae Abu Dhar Al Ghafariy (Radhiya Llahu anhu) akamdhamini mtu huyo juu ya kuelewa kwake vizuri kuwa iwapo mtu huyo hatorudi basi atauliwa yeye badala yake. Mtu huyo hakurudi mpaka baada ya kukaribia sana kumalizika muda wa siku tatu hizo, na watu wakawa na wasi wasi asije Abu Dhar (Radhiya Llahu anhu) akauliwa badala yake.

Dakika za mwisho za siku ya tatu akawasili mtu huyo akiwa amejaa vumbi na huku uso wake ukionesha dalili za kuchoka sana. Umar (Radhiya Llahu anhu)akamuuliza: "Ilikuwaje ukarudi wakati ungeweza kukimbia?" Akajibu: "Nilihofia pasije pakasemwa kuwa; Watu wenye ahadi za kweli hawapo tena."

Kisha Umar (Radhiya Llahu anhu)akamgeukia Abu Dhar (Radhiya Llahu anhu)na kumuuliza: "Na wewe ilikuwaje ukakubali kumdhamini mtu huyu wakati humjuwi?" Abu Dhar (Radhiya Llahu anhu)akasema: "Nilihofia pasije pakasemwa; Wakarimu na wenye moyo wa kishujaa hawapo tena."

Ndipo wale vijana watatu wakasema: "Na sisi tumemsamehe mtu huyu ili pasije pakasemwa; 'Hawapo tena watu wenye kusamehe juu ya kuwa na uwezo wa kulipa kisasi."

Familia,majirani,marafiki au baina ya waislamu ombaneni msamaha na kila mmoja amsamehe mwenzake kwa yaliyopita. Na yafanyeni hayo kwa ajili ya Allah (subhanahu wataala).

Allah atujaalie tuwe kuyafahamu haya yote tuliyoyaeleza. Na tuchukue manufaa yake kwa kusameheana baina yetu ili tuweze kuishi kwa mapenzi na salama baina yetu. Aaamin

No comments:

Post a Comment