Sunday 31 March 2013

MAJINA YA MALAIKA NA KAZI ZAO

Mwenyezi Mungu S.W.T. kajaalia kila kitu alichokiumba kina jina lake maalum ili iwe ni alama yake ya kutambulikana kwake. Na kama vile kila mwanaadamu analo jina lake basi ni hivyo hivyo kwa Malaika, kila Malaika ana jina lake, lafudhi ya majina yao hayafanani na lafudhi ya majina ya kibinaadamu, yaani wao hawana majina kama Athmani, au Ramadhani na Mariam kadhalika na hii inawezekana pengine ni kwa sababu wao wameumbwa si waume wala wake. Mwenyezi Mungu S.W.T. na Mtume wake S.A.W. wametufunulia ndani ya Qur-ani na Hadithi majina ya Malaika 12 pamoja na shughuli zao, kama ifuatavyo:-

1.JIBRIL.


Jibril ni mkubwa wa Malaika na ametajwa katika aya zaidi ya moja ndani ya Qur-ani. Mwenyezi Mungu S.W.T. kasema katika Suratil Baqarah aya ya 97, “


قُلْ مَنْ كَانَ عَدُوًّا لِجِبْرِيلَ فَإِنَّهُ نَزَّلَهُ عَلَى قَلْبِكَ بِإِذْنِ اللَّهِ مُصَدِّقًا لِمَا بَيْنَ يَدَيْهِ وَهُدًى وَبُشْرَى لِلْمُؤْمِنِينَ


Maana yake, “Sema: “Aliyekuwa ni adui wa Jibril, (kwa kuwa ndiye aliemletea Utume Nabii Muhammad asiwapelekee Mayahudi ni bure hana kosa Jibril); hakika yeye ameiteremsha Qur-ani moyoni mwako kwa idhini ya Mwenyezi Mungu (sio kafanya kwa kupendelea kwake); (Qur-ani) inayosadikisha yale yaliyokuwa kabla yake, na ni uwongozi na khabari njema kwa wanaoamini.”


Jibril A.S. ni Malaika mwenye nguvu sana, na Mwenyezi Mungu S.W.T. amemsifu katika Surat Najm aya ya 5 kwa nguvu zake, kasema,


"Amemfundisha (Malaika) Mwenye nguvu sana."


Na baadhi ya Wanavyuoni wamesema kwamba,

“Jibril A.S. kwa ushujaa na nguvu zake aliweza kuiinua miji ya watu wa Luut pamoja na kila kitu kilichomo ndani yake pamoja na watu wake ambao idadi yao inasemekana kuwa ni watu mia nne elfu, aliwainua mpaka mbinguni kwa kutumia bawa lake moja kati ya mabawa yake mia sita. Mbwa na majogoo walisikika sauti zao na Malaika wengine wakati wakilia; na kwa amri ya Mola wake aliiangamiza miji ile na kila kilichokuwemo humo kwa kuigeuza juu chini.”

Mwenyezi Mungu S.W.T. kasema katika Surat Huud aya ya 82, “

فَلَمَّا جَاءَ أَمْرُنَا جَعَلْنَا عَالِيَهَا سَافِلَهَا وَأَمْطَرْنَا عَلَيْهَا حِجَارَةً مِنْ سِجِّيلٍ مَنْضُودٍ

Maana yake, “Basi ilipofika amri yetu tuliigeuza nchi juu chini, na tukawateremshia mvua ya changarawe za udongo mgumu uliokamatana wa Motoni.”


Moja ya kazi ya Malaika huyu mwaminifu ni kupeleka wahyi kwa Mitume na Manabii wote waliotangulia. Na alimwijia mara nyingi zaidi Mtume wetu S.A.W. kuliko Mitume wengine wote, kwa ajili ya kumshushia wahyi au kumfundisha baadhi ya mambo kutoka kwa Mola wake kama vile kusali na kusoma Qur-ani. Jibril ameitwa kwa majina tofauti ndani ya Qur-ani. Na majina yenyewe ni haya yafuatayo:-

1.1.ROHO (RUUH).


Naye ndiye "Roho ambae alitumwa kwa Bibi Maryam mama wa Nabii Issa A.S."

Kama alivyomuita Mwenyezi Mungu S.W.T. katika Surat Maryam aya ya 17, “

فَأَرْسَلْنَا إِلَيْهَا رُوحَنَا فَتَمَثَّلَ لَهَا بَشَرًا سَوِيًّا

Maana yake, “Tukampeleka Roho Yetu (Jibril A.S.) akajifananisha kwake (kwa sura ya) binaadamu alie kamili.”

1.2.ROHO MWAMINIFU (RUUHUL AMIIN).


Na katika Qur-ani anajulikana pia kama "Roho mwaminifu" Mwenyezi Mungu S.W.T. kasema katika Surat Ash-Shu`araa aya ya 193 na ya 194, “


نَزَلَ بِهِ الرُّوحُ الأمِينُ * عَلَى قَلْبِكَ لِتَكُونَ مِنْ الْمُنذِرِينَ

Maana yake, “Ameuteremsha haya Roho mwaminifu (Jibril). Juu ya moyo wako, ili uwe miongoni mwa Waonyaji.”

1.3.ROHO TAKATIFU (RUUHUL QUDUS).


Naye kaitwa na Mwenyezi Mungu S.W.T. kwa jina la "Roho takatifu" katika Suratil Nahal aya 102, “


قُلْ نَزَّلَهُ رُوحُ الْقُدُسِ مِنْ رَبِّكَ بِالْحَقِّ… 

Maana yake, “Sema: “Roho takatifu (yaani Jibril) ameiteremsha hii (Qur-ani) kutoka kwa Mola wako kwa haki…”

1.4.NAMUUS.


Na ameitwa "Namuus" kama alivyosema Waraqa bin Noufal kumwambia Mtume S.A.W. wakati wa mwanzo kabisa Jibril alipomteremshia wahyi Mtume S.A.W.. Kasema Noufal, “


"لقد جاءك النَّامُوسُ الَّذِي أَنْزَلَ اللَّهُ عَلَى مُوسَى".

Maana yake, “Amekuijia Namuus (yaani Jibril) ambaye alimteremsha Mwenyezi Mungu kwa (Nabii) Musa (A.S.).”


Naye ni Malaika mwenye heshima na cheo kikubwa sana mbele ya Mola wa walimwengu wote. Mwenyezi Mungu S.W.T. kamsifu kwa sifa za nguvu zake na cheo chake katika Surat Takwyr aya ya 20, “


ذِي قُوَّةٍ عِنْدَ ذِي الْعَرْشِ مَكِينٍ

Maana yake, “Mwenye nguvu, mwenye cheo cha heshima kwa Mwenyezi Mungu.”

2.MIKAIIL.


Mikaiil ni Malaika mwingine mwenye daraja ya juu mbele ya Mwenyezi Mungu S.W.T. kama alivyomtaja katika Suratil Baqarah aya ya 98, “


مَنْ كَانَ عَدُوًّا لِلَّهِ وَمَلائِكَتِهِ وَرُسُلِهِ وَجِبْرِيلَ وَمِيكَالَ فَإِنَّ اللَّهَ عَدُوٌّ لِلْكَافِرِينَ

Maana yake, “Aliyekuwa adui wa Mwenyezi Mungu na Malaika Wake na Mitume Wake na Jibril na Mikaiil (basi mtu huyo anatafuta kuangamia) kwani Mwenyezi Mungu ni adui wa makafiri.”

Naye amewakilishwa kwa ajili ya mvua na mimea kwa amri ya Mola wake. Mwenyezi Mungu S.W.T. kasema katika Suratil A`araaf aya ya 57, “

وَهُوَ الَّذِي يُرْسِلُ الرِّيَاحَ بُشْرًا بَيْنَ يَدَيْ رَحْمَتِهِ حَتَّى إِذَا أَقَلَّتْ سَحَابًا ثِقَالا سُقْنَاهُ لِبَلَدٍ مَيِّتٍ فَأَنزَلْنَا بِهِ الْمَاءَ فَأَخْرَجْنَا بِهِ مِنْ كُلِّ الثَّمَرَاتِ كَذَلِكَ نُخْرِجُ الْمَوْتَى لَعَلَّكُمْ تَذَكَّرُونَ


Maana yake, “Na Yeye Ndiye anayepeleka pepo (za kuvuma) kuwa ni bishara (khabari njema) kabla ya kufika Rehema Yake (mvua). Hata hizo pepo zinapobeba mawingu mazito tunayachunga mpaka kwenye nchi iliyo kufa. Kisha tunateremsha kwayo maji, ndio kama hivyo tukatolesha kila aina ya matunda. Basi hali kadhalika tunavyo wafufua wafu, ili mpate kukumbuka.

3.ISRAFIIL.


Israfiil ni jina la Malaika ambaye atakayepuliza baragumu siku ya Kiyama. Naye ni mmoja wa Malaika ambaye aliyekuwa akitajwa sana na Mtume wetu S.A.W. katika dua yake kila anapoamka usiku kuabudu. Alikuwa Mtume S.A.W. anamtaja yeye pamoja na Jibril na Mikaiil, kasema katika Hadithi iliyopokelewa na Aisha R.A.A.H. na iliyotolewa na Abu Daud, “

"اللَّهُمَّ رَبَّ جِبْرِيلَ وَمِيكَائِيلَ وَإِسْرَافِيلَ أَنْتَ تَحْكُمُ بَيْنَ عِبَادِكَ فِيمَا كَانُوا فِيهِ يَخْتَلِفُونَ ، اهْدِنِي لِمَا اخْتُلِفَ فِيهِ مِنَ الْحَقِّ بِإِذْنِكَ إِنَّكَ تَهْدِي مَنْ تَشَاءُ إِلَى صِرَاطٍ مُسْتَقِيمٍ".

Maana yake, “Ewe Mwenyezi Mungu! Mola wa Jibril na Mikaiil na Israfiil Wewe Ndiye unayehukumu baina ya waja Wako katika yale waliokuwa wakikhitilafiana, niongoze kwendea haki katika yale waliokhitilafiana kwa idhini Yako, unamuongoza umtakae kwendea njia iliyonyooka.”

4.MAALIK.


Maalik ni jina la Malaika mkubwa wa Malaika walio walinzi wa Motoni. Mwenyezi Mungu S.W.T. kasema katika Surat Zzukhruf aya ya 77, “

وَنَادَوْا يَا مَالِكُ لِيَقْضِ عَلَيْنَا رَبُّكَ قَالَ إِنَّكُمْ مَاكِثُونَ

Maana yake, “Nao watapiga kelele (kumwambia yule Malaika anayewaadhibu waseme) “Ee Maalik! Naatufishe Mola wako!” (Maalik) aseme “Bila shaka mtakaa humu humu (Motoni).”

5.RIDHWAAN.


Ridhwaan ni jina la Malaika ambae kazi yake ni mlinzi wa Peponi. Mwanachuoni Ibn Kathiir kasema, “

"وخازن الجنة ملك يقال له رضوان ، جاء مصرحا به في بعض الأحاديث".

Maana yake, “Na mlinzi wa Peponi ni Malaika anaeitwa Ridhwaan, ameitwa (kwa jina) Musarrihan katika baadhi ya Hadithi.”

6.MUNKAR NA NAKIIR.


Munkar na Nakiir ni Malaika wawili ambao amewataja Mtume S.A.W. katika Hadithi sahihi kuwa ni Malaika waliowakilishwa kuuliza watu maswali kaburini. Nao wana umbo la kutisha na sauti kali sana. Mwenyezi Mungu S.W.T. atuepushe na adhabu ya kaburi. Kila mmoja wetu baada ya kufa kwake anapozikwa kaburini mwake humwijia Malaika hawa wawili na kumuuliza maswali kama vile. "Nani Mungu wako? Nani Mtume wako? Na nini dini yako?" Ikiwa mtu huyo hapa duniani alikuwa mtiifu kwa Mwenyezi Mungu S.W.T. na Mtume Wake S.A.W. ataweza kujibu maswali hayo kwa urahisi lakini ikiwa ni kinyume ya hivyo maswali hayo yatakuwa magumu kwake, hivyo inatupasa tujitayarishe kwa maswali hayo ya kaburini. Na urahisi wa kujibu kwake inategemea na jinsi mtu alivyoishi katika maisha yake hapa duniani. Yaani mtu mwema au muovu?

7.HARUUT NA MARUUT.


Nayo haya ni majina ya Malaika wawili aliowatuma Mwenyezi Mungu S.W.T. kwa watu wa Baabil (Babylon hivi sasa ni nchi ya Iraq) ili wawafanyie mtihani wa kuwafundisha uchawi. Na walikuwa hawamfundishi mtu yeyote yule ila baada ya kumuonya kwao kwamba ukitaka tukufunze basi utakufuru. Mwenyezi Mungu S.W.T. kasema katika Suratil Baqarah aya ya 102, “


وَمَا كَفَرَ سُلَيْمَانُ وَلَكِنَّ الشَّيَاطِينَ كَفَرُوا يُعَلِّمُونَ النَّاسَ السِّحْرَ وَمَا أُنزِلَ عَلَى الْمَلَكَيْنِ بِبَابِلَ هَارُوتَ وَمَارُوتَ وَمَا يُعَلِّمَانِ مِنْ أَحَدٍ حَتَّى يَقُولا إِنَّمَا نَحْنُ فِتْنَةٌ فَلا تَكْفُرْ… 


Maana yake, “Na (Nabii) Suleiman hakukufuru, bali Mashetani ndio waliokufuru, wakiwafundisha watu uchawi (waliokuwa wakiujua wenyewe tangu zamani) na (uchawi) ulioteremshwa kwa Malaika wawili, Haruut na Maruut, katika mji wa Baabil. Na wala (Malaika hao) hawakumfundisha mtu yeyote mpaka wamwambie: “Hakika sisi ni mtihani, basi usikufuru…”

8.IZRAIL.


Na hili ndilo jina alilopewa Malaika wa mauti, jina hili halikutajwa ndani ya Qur-ani wala halikutajwa katika Hadithi sahihi, lakini hii ni kauli ya Wanavyuoni kwa jina hili.

9.RAQIIB NA ATIID.


Hayo ni majina ya Malaika wawili, ambao wamewakilishwa na Mwenyezi Mungu S.W.T. kwa ajili ya kuandika kauli na vitendo vya watu. Na maana ya majina haya Raqiib na Atiid ni kuwa wamehudhuria, mashahidi kwa vile daima hawaachani wako pamoja na watu ila kwa baadhi ya mambo fulani, kama vile mtu akiwa na janaba au akiwa uchi au akiingia msalani (chooni). Mwenyezi Mungu S.W.T. kasema katika Suratil Qaaf aya ya 17 na ya 18, “


إِذْ يَتَلَقَّى الْمُتَلَقِّيَانِ عَنْ الْيَمِينِ وَعَنْ الشِّمَالِ قَعِيدٌ * مَا يَلْفِظُ مِنْ قَوْلٍ إِلا لَدَيْهِ رَقِيبٌ عَتِيدٌ

Maana yake, “Wanapopokea wapokeaji wawili, anaekaa kuliani na (anaekaa) kushotoni, (Malaika). Hatoi kauli yoyote isipokuwa karibu nae yuko mngojeaji (mwangalizi) tayari (kuandika).”

No comments:

Post a Comment